Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa Mwaka wa Fedha 2025/2026

Hon. Charles Muguta Kajege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mwibara

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa Mwaka wa Fedha 2025/2026

MHE. CHARLES M. KAJEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwa kunipa nafasi hii. Kwanza nimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa jitihada zake za kukuza Sekta yetu ya Utalii Nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina masuala machache; la kwanza ni kuhusu vizimba. Katika hotuba ya wizara inaonesha katika mwaka ujao wa fedha watajenga vizimba vitatu tu katika Wilaya ya Bunda; hivi vizimba ni vichache sana. Kwa mfano nikiangalia ukubwa wa Jimbo langu, urefu wa ufukwe peke yake katika Ziwa Viktoria ni zaidi ya kilometa 100, lakini vilevile tuna zaidi ya mialo 40. Sasa, hivi vizimba vitatu vitajengwa wapi? Nilikuwa ninaomba Serikali ifikirie kujenga zaidi ya vizimba 40 katika jimbo langu (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kingine ni kuhusu fidia au kifuta jasho, ninasema ni fidia. Kwanza haitoki mapema, lakini vilevile ni kidogo sana kama walivyozungumza wenzangu. Ninamwomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuhitimisha hoja yake atueleze kwamba ni hatua gani sasa Serikali inachukua ili kuhakikisha kwamba wale wananchi ambao wanapata madhara na wao wanapata kifuta jasho kwanza mapema, lakini vilevile kiwe ambacho kinawasaidia katika maisha yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine ni kuhusu vituo vya askari. Kutokana na mashambulizi ya wanyamapori katika jimbo langu nilikuwa ninaomba sasa tupate vituo vya askari wanyamapori katika maeneo yafuatayo: Kwa mfano, Buzigwe, kila mara kumekuwa na tatizo la mamba, ninaomba kuwe na kituo kingine Buzigwe; kingine katika Vijiji vya Mayolo; Kasaunga; Kisolya; Nampindi; Bulomba; Nchigondo; Mugala; Isikilo; na Namuhula. Hivi vyote ni vijiji ambavyo kila wakati kila mwaka kunakuwa na matukio ya mamba au matukio ya tembo kukanyaga watu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nitumie muda wangu kuunga mkono hoja, lakini nitapenda Mheshimiwa Waziri atakapokuja kufunga hoja yake aje na majibu yatakayotosheleza ili nisiweze kukamata shilingi. Ahsante sana. (Makofi)