Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

Hon. Eng. Ramadhani Hamza Singano

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bumbuli

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

MHE. RAMADHANI H. SINGANO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa fursa hii ya kuchangia hotuba ya bajeti ya Wizara ya Maji ambayo iko mbele yetu. Kwa dhati ya moyo wangu nimshukuru Mwenyezi Mungu Subhanahu Wa Ta'ala kwa kutuwezesha wote kukutana leo hapa, siyo uwezo wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie fursa hii kumshukuru Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mama yetu kipenzi, Mama Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze na kuwashukuru watu wa Wizara ya Maji, Waziri Aweso na Naibu wake Engineer Kundo, lakini nisimsahau Katibu Mkuu na watendaji wake wote wa Wizara ya Maji mpaka level za chini. Niwashukuru RUWASA, niwashukuru watu wa mamlaka zote, lakini na wale wa Bodi za Maji za mabonde ambao ndiwo wanabeba maono, maana wao ndio wanalinda vyanzo vya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waswahili wana misemo yao; wapishi wa pilau pamoja na viungo vingi lakini walaji wa pilau wakasema kachumbari iwepo ile ladha ipatikane vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hotuba nzuri ya Waziri iliyogusa kila sehemu, iliyoleta matumaini kwa Watanzania mpaka walioko kule Bumbuli wakinisikiliza saa hizi, basi mimi nimeona kuna maeneo machache niyachangie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende moja kwa moja kwenye maombi ya mradi mkubwa pale Soni unaotakiwa kuhudumia vijijini tisa kwa Kata ya Mbuzii na Soni. Ninaamini na vile viporo kama saba watakuwa vimevizingatia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende sasa kwenye kushauri na kuchangia maeneo mengine muhimu. Moja ya eneo muhimu leo kwa sababu ya mabadiliko ya tabianchi katika sayari yetu, tumeona twende na vyanzo vya kudumu ambavyo ni mabwawa, lakini vyanzo hivi ili viweze kudumu lazima tusiwasahau wale watu walioko katika Bodi za Maji za Mabonde kwa sababu ndio watalinda vyanzo, ndio watasababisha hata tope kuelekea kwenye mabwawa haya lisije likaenda kupunguza vina tukahifadhi maji machache.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende eneo lingine la Gridi ya Maji ya Taifa (National Water Grid). National Water Grid tunategemea maziwa makuu, Ziwa Victoria, Ziwa Tanganyika na Ziwa Nyasa kwa sababu haya maji yake ni matamu lakini kipaumbele ni Ziwa Victoria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ziwa Victoria kidogo ni la kipekee, yale mengine yako kwenye bonde la ufa, lakini pale ni ardhi tu ilititia, land subsidence ikatengeneza ziwa lile lina historia ya tofauti, lakini ziwa lile lina taarifa mbili nilitaka niziweke wazi. Moja, ni taarifa ya kijiolojia inayosema ziwa lile lilitengenezwa miaka laki nne iliyopita na baada ya miaka laki moja iliyopita lilipata mabadiliko ya kukauka kabisa na tukio la mwisho ni miaka 27,000 iliyopita na hali ya hewa ikabadilika, ziwa hilo likajaa miaka 14,000 hadi 15,000 iliyopita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kuanzia miaka ya 1920 na 1950 mpaka miaka ya 2000, tunachoshuhudia kihaidrolojia tunasema ni zile fluctuation au mabadiliko madogo madogo ya mita moja na mita mbili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mabadiliko haya ya tabianchi siyo mabadiliko madogo, ni mabadiliko ya kuzingatia, lakini tunachojiamini, nimepitia Mkataba wa UN wa nchi ambazo ziko kwenye Maziwa Makuu hasa Ziwa Victoria. Nimepitia makubaliano ambayo ni ya mwaka 2011 ya nchi kumi, nimepitia pia na Itifaki ya Basin ya Mto Nile, lakini article zote ukizingalia zinatupa matumaini kwamba National Water Grid inaenda kutekelezeka bila wasiwasi. Kwa nini? Ni kwa sababu ukiangalia kuna kitu wanaita renewable water resources, maji ambayo ni rahisi kuyapata kwa wepesi kwa ajili ya matumizi. Hii ni bilioni 13 mita kumi kwa ziwa zima, lakini upande wa Tanzania tuna bilioni 6.6.

Mheshimiwa Mwenyekiti, matumizi yetu yote ya Basin ya Ziwa Victoria ambako ndiko tunatoa maji ni 0.38 billion metre cubic ambavyo ya ziwa tu ni 0.2 billion metre cubic. Kwa maana ile bilioni 6.6 bado hatujaigusa. Kwa hiyo, tuko kwenye comfort zone. Bado tunaweza tukatoa bomba lingine tuka Ziwa Victoria kwa mageuzi makubwa haya ambayo watu wa Wizara ya Maji wamefanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina mambo manne sasa ya kushauri kitaalamu. Jambo la kwanza, kwa sababu kinachotusababisha tuone tuko salama ni zile takwimu za ziwa zilizochukuliwa tangu mwaka 1964. Sasa hali hii iendelee ili tuweze kufanya ufuatiliaji mzuri, lakini la pili tutakapotengeneza intake sasa kwa ajili ya National Water Grid takwimu hizi zitumike vizuri tusije tukafika mahala mabomba yakajaa hewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nishauri jambo lingine kwamba level hizi za ziwa zitumike kushauri watu wa ardhi msigawe makazi pembezoni mwa ziwa bila kufuata level hii. Imekuwa kuna hoteli kubwa za kitalii kuna wakati zinazama kwenye ziwa, hii haileti tija. Watu wafanye mipango endelevu ya kushirikiana, Wizara ya Ardhi unagawaje eneo lenye chanzo cha maji bila ku-consult wenzako bila kuwasiliana na wenzako?

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niseme sasa, vile vidakamaji kwenye maeneo ambayo ni intake vilindwe sasa kwa umadhubuti ili isifike mahala kule tulikoweka intake zetu kunaanza kuingia tope na vina vya ziwa vinapotea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nishauri eneo lingine la ulinzi wa vyanzo au uchafuzi wa vyanzo. Tukubali kwamba kuna elimu ndogo kwa jamii. Bado Wizara inahitaji kuwezesha kwenye eneo hili ili kuwaelimisha watu. Ni kweli watu wanaongezeka, lakini sasa ifike mahala tuangalie mbadala inakuwa ni nini. Elimu kwa jamii, ushirikishwaji wa jamii na utekelezaji wa sheria na kanuni lazima uzingatiwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende haraka haraka, nina mambo mengi, lakini mengine nimeshayafikisha kwenye meza ya Waziri kwa sababu nimeona kabisa kuna maeneo sita nyeti nimeyachambua kwa kina nisingeweza kuyachangia hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni motisha kwa watendaji wetu. Watendaji wakikumbukwa wana kawaida ya kuongeza ari, kawaida ya uwajibikaji na kujitoa kwa dhati. Ninaposema wapewe motisha simaanishi fedha. Mtumishi anapopewa cheti tu cha utambuzi kwamba umefanya kazi nzuri, kwenye National Grid wewe ulikuwepo, basi mtumishi huyu anakuwa na furaha kubwa sana. Vilevile, mafunzo ya kujiendeleza kielimu, lakini na kupewa kipaumbele kwa miradi mingine ya kimkakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni eneo la mfuko maalumu kwa ajili ya utafiti. Leo kuna maeneo hatuwezi kupata mito wala maziwa inabidi tutumie maji yaliyoko chini ya ardhi na lazima tutangulize utafiti. Eneo hili lina pwaya, kwa hiyo, mkipata hela mnaanza kukimbizana tena, kumbe mngeweza kufanya. Nimefurahi Waziri alivyosema tayari wanaenda kutengeneza master plan.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine tunataka maeneo ya kujenga mabwawa tuyajue mapema...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa kwa mchango wako.

MHE. RAMADHANI H. SINGANO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru na ninaomba nimalizie nukta moja kwamba niombe tena kuwe na ufuatiliaji wa kudumu wa zile takwimu za maji, mwenendo na ubora, lakini na tope linaloekea kwenye mabwawa litatusaidia kwenye intake zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, ninakushukuru sana. (Makofi)