Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

Hon. Moshi Selemani Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tanganyika

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kunipa nafasi ya kuweza kuchangia. Awali ya yote nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na Katibu Mkuu wa Wizara kwa kazi nzuri wanazozifanya. Tunaishukuru Serikali kwa kuleta miradi mingi ya maendeleo ndani ya Wilaya ya Tanganyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nianze kuipongeza Serikali kwa kutenga fedha shilingi bilioni sita kwa ajili ya upembuzi wa kutoa maji Ziwa Tanganyika kuyaleta Makao Makuu ya Mkoa wa Katavi. Mradi huu kwetu sisi ni mradi muhimu ambao utakuja kutatua kero ya maji ndani ya Mkoa wa Katavi kwenye eneo langu takribani vijiji 20 watanufaika na mradi huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe sana Mheshimiwa Waziri, kasi uliyonayo na ukizingatia wewe ndiye tulienda pamoja kuangalia kile chanzo cha maji kwenye Ziwa Tanganyika, ni vizuri sasa mkaelekeza nguvu ili kutatua kero ya maji kwenye eneo hilo la Mkoa wa Katavi kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri nikuombe sana kwenye Mradi wa Kalema – Kapalamsenga, Kijiji cha Itetemia na Itunya huu mradi ni mradi wa muda mrefu takribani shilingi bilioni 1.3 zilitengwa, hatua ya awali ilishafanyika utandazaji wa mabomba ulishakamilika umebaki hatua ya kujenga tenki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa bahati mbaya sana mkandarasi aliyepewa mradi huu alipolipwa shilingi milioni 181 aliondoka jumla, ameutelekeza ule mradi. Niiombe Serikali imfuatilie mkandarasi ili aweze kujenga lile tenki wananchi waweze kunufaika. Mradi huu umechukua muda mrefu, sasa ni mwaka wa tatu haujakamilika. Niombe sana Mheshimiwa Waziri hili ni jambo ambalo ukilitekeleza utakuwa umetusaidia sana wananchi wa Wilaya ya Tanganyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi mwingine ni mradi wa Kijiji cha Katobo, mradi ambao una thamani ya shilingi bilioni 1.7. Mradi huu unategemea kuhudumia Vijiji vya Kambanga, Igalula na Ifukutwa. Mradi huu ulishatengewa fedha, lakini bado fedha hazijafika kwa wakati, tunaomba mradi huu uwekee maanani na utenge mazingira ya kuhakikisha mradi unakamilika kwa wakati ili wananchi waweze kunufaika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mradi wa Mji wa Majalila; Mji wa Majalila ni mji ambao unakua chanzo chake cha maji kilishazidiwa kwa kuwa tuna idadi zaidi ya watu 10,000 wanategemea kupata huduma ya mradi wa maji. Niombe sana Mheshimiwa Waziri mahitaji ya mradi huu tunahitaji ujenzi wa tenki ambalo litakuwa na uwezo wa kuchukua lita milioni moja ili uweze ku-supply kwenye maeneo yale ambayo wananchi wanahitaji kupata huduma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi huu utahitaji fedha takribani shilingi bilioni 1.1 kwa ajili ya kuchimba kisima kipya na kujenga tenki ambalo litasaidia kupeleka huduma kwa wananchi na kutatua kero ya wananchi kwenye maeneo hayo. Eneo hili ni muhimu ndiyo Makao Makuu ya Wilaya, Hospitali ya Wilaya wanakosa maji, wananchi wanakosa huduma kwa sababu maji yaliyopo sasa hivi hayatoshelezi kulingana na idadi na taasisi za Serikali kuwa nyingi kwenye maeneo hayo. Niombe sana hili ulifanyie kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo ningependa kuishauri Serikali, naungana mkono na namuunga mkono ndugu yangu Mheshimiwa Mnzava, Mheshimiwa lazima tujenge msingi wa kuvuna maji. Mheshimiwa Rais wa Kwanza, Mwalimu Nyerere alijenga mabwawa karibu kila kona ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la kwangu kwenye Kijiji cha Majalila kulikuwa na Bwawa la maji ambalo lilikuwepo na lilitoa huduma kubwa sana, lakini sasa hivi tuna majengo mengi ya Serikali ambayo yanajengwa mkishirikiana na Wizara ya TAMISEMI mnauwezo kabisa kila nyumba ya Serikali inayojengwa iwekewe mazingira ya uvunaji wa maji itasaidia sana kutatua kero ya maji katika maeneo mengi katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo hili halijafanyiwa kazi ipasavyo, ni vyema tukatunza vyanzo vya maji, lakini tukajenga msingi ambao kupitia fedha zile zinazoidhinishwa kwenye Wizara mbalimbali, kwenye majengo ya Serikali yanaweza kabisa yakatufanya sisi nchi yetu tukatatua tatizo la maji ambalo lipo karibu kila kona. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa nasisitiza tunahitaji Mradi wa Maji wa Ziwa Tanganyika uweze kuwanufaisha wananchi wa Mkoa wa Katavi, Mkoa wa Kigoma na Mkoa wa Rukwa ambao kimsingi hawajanufaika na upatikanaji wa maji kutokana na resource ya maji zilizopo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naunga mkono. (Makofi)