Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

Hon. Eng. Ramadhani Hamza Singano

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bumbuli

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

MHE. RAMADHANI H. SINGANO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru sana kwa nafasi hii kwa kupata muda wa kuchangia wakati huu. Awali ya yote, nimshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ndio mwingi wa rehema na anayetujalia hata uwepo wetu hapa. Suala la mazingira na Muungano ni mambo muhimu sana lakini nimshukuru sana kwa dhati ya moyo wangu Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama yetu kipenzi Mama Samia Suluhu Hassan kwa kuwa kinara wa mazingira. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona hata ile Sera ya Mazingira ya Mwaka 1997 wakati akiwa huko kwa maono yake mazuri tayari 2021 tumepata sera mpya ambayo imeboresha zaidi masuala mazima ya mabadiliko ya tabianchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru pia Mheshimiwa na kumpongeza Mheshimiwa Makamu wa Rais ambaye Hotuba hii ambayo ni jambo tunalolijadili liko chini ya Wizara yake Mheshimiwa Balozi Dkt. Emmanuel John Nchimbi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru pia Mheshimiwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba kwa jinsi anavyoendelea kuitafsiri tabasamu ya Mama Samia Suluhu Hassan hasa anapopita kwa Watanzania na hili tumelishuhudia katika ziara zake mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru sana pia Waziri wa Ofisi hii ya Mazingira na Muungano ndugu yangu Mheshimiwa Injinia Masauni na Mheshimiwa Naibu Waziri wake ndugu yangu Mheshimiwa Ruben Kwagilwa jinsi anavyomsaidia Waziri wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa nilikuwa mtendaji niwashukuru watendaji wote wa NEMC kuanzia wa juu mpaka wa chini kwa kazi nzuri wanayoifanya na kumwezesha Mheshimiwa Waziri naye atuletee taarifa iliyonona na iliyopendeza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mazingira ni suala mtambuka na ni suala ambalo limeongelewa pia katika vitabu vya Dini. Imenukuliwa katika Kitabu cha Isaya ya 32:19: “kwamba lakini mvua ya mawe itakunya (kwa maana itanyesha kwa lugha nyingine) wakati ambao wakati wa kupunguza miti ya msituni na huo mji utadhalilika.” Hii ni dalili kwamba tunapochafua mazingira kuna madhara yanajitokeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama mvua nyingi itanyesha na mji udhalilike, maana yake kinyume chake kuna wakati tunapata ukame pia. Hata katika Quran imenukuliwa katika Surat Nuur aya ya 40 Mwenyezi Mungu anasema, akiyazungumzia mazingira, “Dhwaharal fasad fiilbarri walbahar bimaaakasabat ay’yin naas.” Ufisadi, uharibifu umeongezeka mno kuanzia bara na baharini kuanzia nchi kavu na majini kwa sababu ya mikono ya watu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika andiko lingine Mwenyezi Mungu anasema katika Surat Yunus aya ya 44, “Inna Allah laayadhrumu nnasa shaian walaakinna nnasa anfusahum yadhwirimun.” Hakika Mwenyezi Mungu hajawahi kuwadhulumu watu bali nafsi zao wenyewe, maamuzi yao mabaya wenyewe, ndiyo yanawaletea madhara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende moja kwa moja kwenye michango yangu ambayo nimeikusudia wakati huu. Jambo la kwanza ni jambo la kuboresha tozo katika Wizara hii ikiwepo na taasisi yake ya NEMC. Niungane na wenzangu waliotangulia wakiizungumzia ile polluter pays principle kwamba anayechafua mazingira lazima ashikwe tozo au mazingira yakichafuliwa lazima yalipiwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huwa najiuliza mpaka najikuna kichwa. NEMC ana dude kubwa tumempa la kusimamia mazingira. NEMC ndiyo anawakagua watu wa migodi, NEMC ndiyo anawakagua watu wa gesi, NEMC ndiyo anawakagua wachimba mafuta na ana gharama kubwa hapo anaingia; kwa nini asiwe na tozo la uhakika? Kwani akipata asilimia moja moja tu si anayafanya mazingira yanakaa vizuri?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi akipata asilimia moja ya madini, akapata ya mafuta (wale wanaochimba visima vya mafuta) kwa sababu yeye ndiyo mkaguzi, akapata kwenye visima vya gesi hamwoni kwamba NEMC anaenda kufanya jambo kubwa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kama percent zote hizi asilimia zote hizi zinaenda Wizara ya Fedha basi kama wanachukua moja kwa nini wasigawane na NEMC? Upo msemo mmoja wa kanuni ya dini unasema, “maa laa yatiibul wajibu ilaabihi fahuwal waajib.” Kinachosababisha wajibu utimie ndio wajibu wa kwanza kabla ya wajibu wenyewe. Sasa kama tunataka NEMC awepo pale lazima tozo lake tulizungumzie vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama shida ni sheria kwa nini isije hapa tukaisimamia Waheshimiwa Wabunge mpaka ikakaa sawa matozo haya yakamsaidia. Sioni kwa nini NEMC asipate tozo ya uhakika kwa sababu vyanzo vipo ni suala tu la kuweka sawa sheria kama ndiyo yenye shida. Hapa Mheshimiwa nimwombe Waziri hili alichukue kwa herufi kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo wanaweza wakaongeza mapato ni kwenye biashara hii ya kaboni ya hewa ukaa (biashara ya carbon ambayo pia ndiyo hewa ukaa). Tunaitumia carbon kwa sababu ndiyo reference. Nchi 192 zilikaa katika itifaki ya Kyoto ya Mwaka 1997. Nyingine zilikataa, lakini mwaka 2015 kwenye yale Makubaliano ya Paris zote zilikubaliana hapa ndio msingi wa hewa ukaa ilipoanzia. Ni biashara kubwa ambayo elimu ni ndogo katika maeneo tunayoyaishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru kwamba ipo mifano ya kuangalia katika Wilaya za Tanganyika na Nyanda za Juu Kusini kwa sababu tayari wameshaanza kupata pato hili. Kwa hiyo hili lielekezwe kwenye maeneo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nishauri jambo lingine kwamba hewa hukaa katika maeneo ya baharini ni zao kubwa sana kwa sababu miti ya mikoko huwezi ukailinganisha na misitu ya kawaida. Katika bahari, zao la hewa ukaa linaweza likawa ni mara tano au mara 10 zaidi ukisoma makala nyingi za kimazingira. Kwa hiyo, ina maana mpaka sasa hivi tumepoteza dola nyingi sana na trilioni nyingi sana za mazingira. Nishauri pia kwamba elimu ya hewa ukaa inatakiwa ifike kwa viongozi wa chini mpaka wa vijiji kwa sababu hawa ndiyo wabeba maono ya wale wananchi wa kawaida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nishauri lugha zitumike nyepesi. Unaweza ukatumia carbon credit isieleweke, lakini kwa nini usiseme, “fedha zinazopatikana kwa utunzaji mzuri wa misitu na matumizi ya hewa safi? Kwa nini lugha kama hizo zisitumike ili kuhakikisha wananchi wanang'amua vizuri na kufikia malengo tunayoyakusudia?

Mheshimiwa Mwenyekiti, elimu isipopatikana basi pato la hewa ukaa au pato la biashara ya carbon tutalisikia na hatutafikia malengo. Kwa kuwa kuna wenzetu ambao wameshaanza, basi wengine wakajifunze huko ili tuhakikishe kwamba tunaendana na maono ya Mama Samia Suluhu Hassan.

Mheshimiwa Mwenyekiti, muda ni mdogo, lakini NEMC inakotokea imesonga mbele sana lazima tuisifie. Nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri. Aliwahi kusema mwanafalsafa Dkt. Kwame Nkrumah wa Ghana akasema, “those who would judge us merely by the heights we have achieved, would do well to remember the depth from which we started.” Wale wanaotupima kwa kimo tulichofikia wangefanya vizuri zaidi kama wangeanzia kwenye kina tulipoanzia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa haya machache ninaomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana kwa nafasi ya kuchangia. (Makofi)