Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliyoitoa wakati wa Ufunguzi Rasmi wa Bunge la Kumi na Tatu, Tarehe 14 Novemba, 2025

Hon. Kakulu Burchard Kakulu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbagala

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hotuba ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliyoitoa wakati wa Ufunguzi Rasmi wa Bunge la Kumi na Tatu, Tarehe 14 Novemba, 2025

MHE. KAKULU B. KAKULU: Mheshimiwa Naibu Spika, kama walivyotangulia wenzangu, nichukue nafasi hii kwanza kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutufikisha siku ya leo tukiwa salama, tukikutana tena kama Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; moja, kwa ajili ya kuyachakata na kuyachambua maoni ya Mheshimiwa Rais ili tukayatafsiri kwa usahihi mbele ya Watanzania waliotuchagua na kuwaaminisha kwamba bado kuna nafasi kubwa ya kuijenga nchi yetu nzuri iitwayo Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, nikupongeze wewe na Mheshimiwa Spika pamoja na Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kuaminiwa katika nafasi mlizoaminiwa kuhudumia nchi yetu. Sambamba, pongezi hizi ziende kwa Mawaziri wetu walioteuliwa kuhudumia katika Baraza la Mawaziri.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninawapongeza pia Wabunge wenzangu waliochaguliwa kuhudumu katika Bunge hili. Nitoe shukrani zangu za dhati kwa wananchi wenzangu wa Jimbo la Mbagala walionichagua kwa kura nyingi kuwawakilisha katika Bunge la Jamhuri ya Muungano. Ahadi yangu kwao ni kuwahudumia kwa uaminifu kwa uzalendo na kwa utii.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nitajielekeza kwa uchache katika maeneo machache. Kwanza katika kutafsiri maoni ya Mheshimiwa Rais aliyoyatoa kupitia hotuba yake kwa Bunge lako Tukufu. Mheshimiwa Rais alichora mchoro wa uhakika katika maono yake kuhusu sekta ya viwanda na sekta ya kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu utajielekeza kwenye maeneo hayo, kuonesha kwamba viwanda vyetu ambavyo tunakusudia kuvijenga kupitia kongani zitakazofunguliwa katika kila wilaya na katika kila halmashauri zetu, na namna zitavyoenda kufungamanishwa na sekta yetu ya viwanda ambaye ndiye mlishaji mkubwa sana wa viwanda vyetu na sekta yetu ya usindikaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa kilimo chetu bado kinategemea sana kilimo cha mkono na kilimo cha kujikimu. Maono ya Mheshimiwa Rais ni kwenda kukitafsiri na kukipa nyongeza na kukiongezea uwezo kilimo chetu ili kiweze kuhudumia viwanda vyetu kwa uhakika, kituhakikishie usalama wa chakula pamoja na kutupatia mapato kupitia fedha za kigeni.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuanza, sekta yetu ya kilimo kwa sasa inachangia pato letu kwa Taifa angalau kwa 26.3%. Lengo ni kuifanya ichangie zaidi kwa sababu ndiyo sekta inayoajiri watu wengi. Mabadiliko kidogo katika sekta hii angalau ikiwa katika asilimia nane mpaka 10% ina uwezo wa kupunguza umaskini kwa zaidi ya nusu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tukiunganisha sekta yetu ya viwanda na sekta yetu ya kilimo kwa kuzingatia maono ya Mheshimiwa Rais aliyotupa kupitia hotuba yake, tuna uwezo wa kutoa ajira za kutosha kwa vijana wetu ambao ndio tunakusudia kuwahudumia kwa kweli, kwa sababu ndio wanaounda sehemu kubwa ya nchi yetu kwa sasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninapenda nichukue nafasi hii kuwaonesha vijana wa nchi hii kwamba bado kuna nafasi ya kuihudumia nchi hii kwa kuitunza na kwa kuitumikia kwa uzalendo. Kilimo chetu pekee tukikifanya vizuri, zile kongani zetu za viwanda katika wilaya zetu 139 na halmashauri zetu 184 tuna uwezo wa kuzalisha ajira za kutosha ambazo zitapunguza presha kubwa iliyopo katika soko la ajira.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, katika kutekeleza maono ya Mheshimiwa Rais, tunaenda kufungua Kongani ya Viwanda ya Kwala. Kongani ya Viwanda ya Kwala peke yake itazalisha ajira zaidi ya 600,000. Kongani ya Buzwagi pekee inaenda kuzalisha zaidi ya ajira 300,000. Kongani ya Bagamoyo inakuja, hebu jaribu kufikiria tutakapofungua kongani katika wilaya zote 139, hali ya ajira na mfumuko wa ajira kwa ajili ya vijana itakuwa ya namna gani? Yote haya, kwa vyovyote vile wanufaika wakubwa ni vijana wenzetu ambao ndio tunakusudia wapate ajira za kutosha katika kongani hizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaamini kwa speed ya Mheshimiwa Rais katika kipindi cha miaka mitano ijayo, matarajio yetu tunakusudia kuyaona mabadiliko makubwa kupitia kongani hizi ambazo zitafunganishwa na sekta yetu ya kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ombi langu kwa wasaidizi wa karibu wa Mheshimiwa Rais kupitia Baraza aliloliteua likiongozwa na Waziri Mkuu, ni kumsaidia Mheshimiwa Rais kuitafsiri barabara ndoto yake hii na maono yake haya ili vijana waweze kupata furaha kwa sababu wanaye Rais ambaye anawaamini, anawategemea na tunawaamini vijana wote kama walinzi na watetezi muhimu wa nchi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitajielekeza kwenye jambo lingine muhimu sana hasa katika kipindi cha miaka minne iliyopita ambacho Mheshimiwa Rais wetu ametuhudumia kama Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa wengi ambao tuna shukrani, kwa kweli Mheshimiwa Rais amefanya kazi kubwa, kubwa sana. Kwa mfano, kwenye jimbo langu pekee ninalotoka, katika halmashauri ya Temeke ninayotoka peke yake, zaidi ya shilingi 323,000,000,000 zililetwa katika kipindi cha miaka minne na zimetekeleza na kusababisha mapinduzi makubwa sana katika sekta ya afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika jimbo ninalotoka peke yake Jimbo la Mbagala vituo vitatu vya afya katika kipindi cha miaka minne peke yake, Hospitali ya Zakhem tunakamilisha kuijenga. Tunaenda kujenga hospitali nyingine kwa ngazi ya wilaya katika kata moja pale Toangoma ya ghorofa sita. Tunaenda kusababisha mapinduzi makubwa kwenye sekta ya elimu kama ambavyo tumefanya katika kipindi kilichopita.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye jimbo langu peke yake zaidi ya shilingi 123,000,000,000 zililetwa katika kipindi cha miaka minne. Jimbo moja tu lenye kata sita peke yake, pamoja na kwamba lina wakazi zaidi ya 500,000.

Mheshimiwa Naibu Spika, watu wenye shukrani kama tulivyo Waheshimiwa Wabunge na Watanzania, tunao wajibu wa kumshukuru Mheshimiwa Rais na kumpa moyo, aendelee kuhudumia nchi yetu, kwa sababu tunaamaini katika kipindi cha miaka mitano inayokuja, matarajio makubwa ni kuona mapinduzi makubwa kwenye sekta zote kuanzia nishati, miundombinu, kilimo, na ajira kwa vijana. Yote haya lengo ni moja tu, kuhakikisha uchumi wetu unastawi na uweze kuwahudumia wananchi wetu ambao wanaongezeka kwa kasi kidogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo langu kwa vijana kama kijana mwenzao, ni kuwaomba wawe wazalendo kwa nchi yetu. Sisi sote tumetembea safari ndefu kufika tulikofika. Mimi miaka 32 iliyopita nilihamia Dar es Salaam nikiwa na miaka karibu 18. Leo hii tunapozungumza nimeaminiwa na Watanzania wenzangu katika eneo la Mbagala na kuwa mwakilishi wao baada ya kukaa hapo kwa miaka 32.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nchi yetu ni nzuri, kila mahali ulipo unayo nafasi ya kuhudumia watu. Nchi yetu hii ni kiasi tu kama kijana kupanga maono yako vizuri, kuwa mtii kwa nchi yako, kupenda nchi yako, kufanya kazi kwa bidii, kujituma na kuwa mtii kwa mamlaka ya nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hayo machache niliyochangia, ninaomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)