Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Mbulu Vijijini
Contributions
nil
Answers
nil
Commettees
0
Ministries
nil
MHE. DKT. EMANUEL Q. NUWAS: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu aliyetupa nafasi na afya njema kuweza kuwepo leo na kuweza kupata nafasi ya kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia, nikushukuru wewe kwa kunipa nafasi hii ya kuweza kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Rais wetu. Pia, ninapenda kutoa shukrani kwa wanananchi wa Jimbo la Mbulu Vijijini ambao wamenipa kura za ndiyo, na kumpa Mheshimiwa Rais Samia kura za kutosha asilimia kubwa sana. Ninapenda kuwapa shukrani za dhati na kwamba nipo hapa tayari kwa ajili ya kuwawakilisha katika miaka mitano ijayo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ninapenda kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa hotuba yake nzuri aliyoitoa wakati wa ufunguzi wa Bunge letu tarehe 14 Novemba, 2025, ambayo tunaendelea kuichangia au kuitolea maoni mbalimbali.
Mheshimiwa Naibu Spika, leo tunajua kwamba Mheshimiwa Rais wetu, kipenzi chetu na mama yetu ambaye ni hodari sana amesherehekea siku ya kuzaliwa kwake na amesema leo ni 27 ya kijani. Ninaomba tuendelee kumuunga mkono kuhakikisha kwamba tunashiriki zoezi la upandaji miti ambalo linakwenda kuboresha mazingira katika maeneo yetu tunayoishi na tuwape hamasa wananchi wetu ambao tunawawakilisha. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba pia nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa ustahimilivu wake, ujasiri wake na ushupavu wake kuipitisha nchi yetu katika kipindi kigumu cha misukosuko na leo ikiwa tulivu hasa kwa kadhia iliyotokea tarehe 29 na tarehe zilizofuata.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli tumeona katika hotuba yake upendo wa kweli na ujasiri wa kweli na ustahimilivu wa kweli hasa kwa kuhakikisha kwamba anaendelea kutambua walioathirika kwa kuwapa pole, na vilevile kuwaalika katika azma nzima ya kuja pamoja kama Watanzania kwa njia ya maridhianno na kuendelea kuongea kwa pamoja na kutatua changamoto zetu kwa njia ya majadiliano. Hii ni tunu muhimu sana kulindwa hasa kama jamii moja ya Watanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia, Mheshimiwa Rais ameunda Tume ya Uchunguzi, na pengine tuendelee kusubiri majibu yake ili tuweze kuyapokea yale yatokanayo na kuendelea kujenga nchi yetu kwa mustakabali wa kizazi chetu cha sasa na kinachofuata.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa ahadi zake alizozitoa na ambazo ameshaanza kuzitekeleza. Tunaona leo Bima ya Afya kwa Wote inaanza na hasa tunaona upendo wa Rais kwa kuyazingatia makundi ambayo yako kwenye hatari ya kukosa matibabu wakati wanapougua kutokana na changamoto ya kiuchumi hasa wazee wetu wa miaka 60 kwenda juu, watoto wadogo na wakinamama wajawazito ambao tumeona wanaathirika kwa vifo vingi pamoja na wale watoto wachanga.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo bado nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri ambayo ameifanya na uwekezaji mkubwa ambao ameweka kwenye sekta ya afya kwa kuhakikisha kwamba vifo vya wakinamama wajawazito vimepungua zaidi kwa asilimia kubwa sana na vifo vya watoto wachanga na bima ya afya inaendelea kupunguza tatizo hili katika nchi yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunajua kwamba Mheshimiwa Rais aliahidi mikopo kwa wajasiriamali na hii tayari ameshaanza kuitekeleza kwa kutoa zaidi ya shilingi bilioni 10.5. Hii imeendelea kuwa ni hatua kubwa na muhimu ya Mheshimiwa Rais kutekeleza ahadi zake alizoahidi kwa Watanzania wakati wa uchaguzi.
Mheshimiwa Naibu Spika, hii mikopo ya wajasiriamali ambayo ameitoa kupitia benki mbalimbali imekwenda kuwazingatia wazee/wakinababa wengi ambao wamekuwa wakilalamika katika mikutano yetu mbalimbali kwamba mbona vijana na wakinamama wamepewa kipaumbele? Je, wazee wanazingatiwa wapi? Ninaona hii mikopo imewakumbuka. Kwa hiyo, tumpongeze Mheshimiwa Rais kwa jinsi ambavyo ameleta hoja hii na amewazingatia wazee wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze pia kwa ajira ambazo amezitoa kwa walimu na watumishi wa sekta ya afya. Tunaamini elimu yetu itaimarika. Pia, huduma za afya zitakwenda kuimarika katika maeneo ya vituo vyetu vya afya, zahanati, hospitali zetu za wilaya, hospitali za mikoa na za Taifa.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba niweze kuchangia kwenye sekta ya kilimo kwa uchache. Sekta yetu ya kilimo ni sekta muhimu sana na ni sekta ambayo inatulisha Watanzania wengi lakini pia imeajiri Watanzania wengi. Tunashukuru Mheshimiwa Rais amesema kilimo ni uwekezaji na ni biashara kama biashara nyingine. Maana yake ipate msukumo wa pekee hasa katika kuitengea bajeti na vilevile katika kuiwekea utaalamu wa kutosha ili wananchi waweze kufaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kilimo cha umwagiliaji Mheshimiwa Rais amekizungumzia kwamba ataenda kuongeza ekari za kilimo cha umwagiliaji kutoka 3.46 milioni hadi milioni sita. Hii ni hatua kubwa sana na itakwenda kuajiri vijana wengi.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile, ninapenda kushukuru kwa niaba ya Wananchi wa Jimbo la Mbulu Vijijini. Tumepata visima sita ambavyo vimechimbwa kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji ambacho kitakwenda kuajiri wakulima katika zaidi ya ekari 300, lakini vilevile tumepata bwawa kubwa ambalo litakwenda kuwasaidia wakulima wa kilimo cha umwagiliaji kwa vitunguu maji, vitunguu saumu, mahindi na mazao mengine na itakwenda kuongeza uzalishaji wa malighafi kwa ajili ya viwanda pamoja na kuajiri vijana walio wengi.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika eneo hili la kilimo tunaona Rais amesisitiza umuhimu wa uwepo wa mikopo kwa ajili ya wakulima. Tuna Benki yetu ya Maendeleo ya Kilimo na pia tuna Benki ya Ushirika. Kwa hili kwa kweli tunaipongeza Serikali, lakini tuna maombi hapa kwamba benki hizi zishuke kwa wakulima ambao wengi wako vijijini na ziweze kuwafikia. Hizi benki bado ziko mijini hazijawafikia wakulima walio wengi na hasa wale walio katika maeneo ya vijijini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niombe pia, tumepata ruzuku kwenye maeneo ya mbolea, lakini pia na mbegu. Bado maeneo mengi yamepata kwa bei nzuri sana hasa ile elekezi ya Serikali, lakini tunajua bado tunao wauzaji wa mbegu hizi na wauzaji wa mbolea ambao bado wanaihujumu Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tunaomba usimamizi uendelee kuimarishwa ili kuhakikisha kwamba ruzuku ambayo Serikali imeweka kwenye mbolea na mbegu inaweza kuwafikia wakulima bila kuibiwa hasa na matajiri ambao wana tamaa zao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba katika eneo hili la kilimo Serikali hasa Wizara yetu ya Kilimo iendelee kuboresha uwekezaji katika eneo la kuongeza thamani katika mazao ambayo wakulima wetu wanazalisha ili tuzalishe ajira na bidhaa ambazo zinaweza kwenda kuuzwa na zikaweza kuongeza ajira, kutengeneza malighafi kwa ajili ya viwanda, vilevile kuongeza kipato kwa wakulima wetu, lakini pia kuongeza kodi kwa ajili ya Serikali yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ninachangia eneo la mifugo kwa ufupi sana. Tunajua kwamba nayo ni sekta muhimu sana na wananchi wangu wa Jimbo la Mbulu Vijijini ni wakulima na wafugaji. Mwaka jana, 2025 mwishoni tulipata adha kubwa sana kwa wafugaji wengi sana kupoteza mifugo hasa kutokana na ukame, vilevile magonjwa yatokanayo na kupe.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninapenda kusema kwamba Mheshimiwa Rais katika hotuba yake ameelekeza kwamba tuendelee kujenga kuelekea katika ufugaji wa kisasa ambao unakwenda kusaidia katika uongezaji wa eneo la ufugaji na vilevile kuhakikisha maji yanapatikana kwa ajili ya mifugo. Pia, kuhakikisha kuna majosho ya kutosha katika maeneo ya ufugaji na chanjo kupatikana. Vilevile, kuhakikisha tunakuwa na mifugo iliyo bora ambayo inafugwa na wafugaji wetu ili iwe na tija hasa kwa ajili ya soko la ndani na soko la nje.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunajua yako maeneo ambayo yametengwa kwa ajili ya wafugaji, lakini yapo maeneo ambayo hayatajatengwa. Yale maeneo ambayo yametengwa, tunaomba Serikali iweze kusaidia sasa kuweka miundombinu muhimu hasa majosho, pia, kuhakikisha supplies mbalimbali kwa ajili ya kusafisha ng’ombe, kuchanja ng’ombe na kuwapa utaalam unaofaa ili tuweze kupata mazao yaliyo bora hasa katika eneo hili la mifugo. Vilevile, wafugaji wakumbukwe katika eneo la mikopo kwa sababu ni wazalishaji muhimu sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba niende kwenye eneo la barabara. Ninashukuru sana kwamba Mheshimiwa Rais amezungumza katika hotuba yake na ametoa dhamira ya kweli na hakika kwamba kuna haja ya kuongeza bajeti katika eneo la barabara hasa kwenye TARURA. Vilevile, ninaomba na TANROADS nayo ikumbukwe.
Mheshimiwa Naibu Spika, hii barabara ni miundombinu muhimu sana hasa katika maendeleo kwa sekta zote na kwa maeneo ya vijijini, wakulima, wafugaji na wajasiriamali hawawezi kuzalisha na kufikisha mazao yao katika masoko bila kuwa na barabara iliyo imara, nzuri na inayopitika majira yote ya mvua na masika.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba bajeti ya eneo hili iongezwe na hasa katika jimbo langu. Ninaomba sana ile barabara inayojengwa kwa kiwango cha lami kutoka Mbulu – Garbabi (kilometa 25), Labay – Haydom (kilometa 25), lakini vilevile kutoka Dareda – Dongobesh, Haydom – Mogitu na Haydom – Singida. Hii ni miundombinu muhimu sana kuunganisha mikoa na wilaya na wananchi wetu watakwenda kufaidi sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ninashukuru kwa upande wa umeme tumepata vitongoji 9,000 na jimbo langu limepata vitongoji 59 na vingine vinaendelea kupata kwa kuwa uhitaji ni mkubwa…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa muda wako umekwisha, malizia.
MHE. DKT. EMANUEL Q. NUWAS: Mheshimiwa Naibu Spika, ninashukuru sana. Ninapenda kukushukuru wewe na ninashukuru kwa hotuba nzuri ya Mheshimiwa Rais, ninaunga mkono hoja. (Makofi)