Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mpango Elekezi wa Maendeleo wa Muda Mrefu 2026/2027–2050/2051, Mapendekezo ya Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2026/2027–2030/2031 na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Mwaka 2026/2027; na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali Katika Muda wa Kati ya 2026/2027 hadi 2028/2029.

Hon. Thomas Maganga Kampala

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Katavi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mpango Elekezi wa Maendeleo wa Muda Mrefu 2026/2027–2050/2051, Mapendekezo ya Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2026/2027–2030/2031 na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Mwaka 2026/2027; na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali Katika Muda wa Kati ya 2026/2027 hadi 2028/2029.

MHE. THOMAS K. MAGANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru kwa kunipa nafasi ili niweke mchango wangu kwenye hoja mahususi ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa letu. Kwanza, nichukue fursa hii kumpongeza sana Waziri, kaka yangu Profesa Alexander Kitila Mkumbo, kwa wasilisho zuri, lakini pia nichukue fursa hii kumpongeza Waziri wa Fedha naye kwa andiko zuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli usiopingika hakuna Taifa duniani liliwahi kuendelea bila kuwa na mpango. Mzee wangu Profesa Muhongo amechangia vizuri sana mchana hapa; ametupitisha tulikuwa wapi, tumetoka wapi, tumefika wapi na wapi tulianguka na akatoa suluhisho la tutanyanyukaje. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Mpango huu ninataka nijielekeze moja kwa moja kwenye kilimo. Ni ukweli usiopingika kilimo ndicho kinaajiri Watanzania wengi nchi hii. 70% ya Watanzania wameajiriwa kwenye kilimo. Ni lazima Serikali ichukue hatua za makusudi kuwekeza kwenye kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo ndiyo njia pekee ya kutusaidia kuweka mazingira mazuri ya kusababisha vijana wengi wanaotoka vijijini wasitoke vijijini kukimbilia mjini. Tukiwekeza vizuri kwenye kilimo na vijana wengi vijijini wakavutika na kilimo, mjini kutapunguza wimbi kubwa la vijana ambao hawana ajira. Niwaombe sana, kaka yangu Profesa Kitila Mkumbo ninamshukuru na ninampongeza sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ameanza kwa mfano kuwekeza kwenye kilimo. Ni lazima Serikali iamue kwa makusudi kufanya proper investment kwenye irrigation schemes. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kule Jimbo la Katavi tuna maeneo 13 ambayo yanafaa kwa kilimo cha umwagiliaji na imefanyika study, wamekuja watu wa kilimo wamefanya study na wakathibitisha kuwa kweli yanafaa. Ninamwomba Waziri atakapokuja wakati anafanya majumuisho atueleze ana mpango gani kwenye eneo la kilimo. Ameeleza vizuri kabisa, Mpango huu unaokwenda unakwenda kubadilisha kilimo kutoka kwenye kilimo cha kujikimu kuja kwenye kilimo cha biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakubaliana naye, sisi Katavi tuna zao la tumbaku ambalo linafanya vizuri. Leo hii ninavyoongea mwaka jana wakulima wa tumbaku wa Jimbo Katavi wamelima kwa kiwango kikubwa na wamepata fedha nyingi sana wakahamasika kulima. Hivi ninavyoongea wakulima wa tumbaku wa Jimbo la Katavi wamejipanga kulima badala yake imekuja notice kwenye vyama vya ushirika wapunguze kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati huo huo tunajipanga kwenda kwenye kilimo cha biashara, wakati huo huo wakulima wetu wanakatishwa tamaa, tunakwenda wapi? Niiombe Serikali sisi Katavi wale wakulima wanalima na ile tumbaku tutalima tutavuna. Wasipotengeneza mpango mzuri wajipange watwambie ile tumbaku wataikoroga juice. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maendeleo na mpango wowote ni lazima ujielekeze kwenye miundombinu. Nimeongea mara nyingi na nimeongea na Waziri wa Ujenzi kuhusu Barabara inayotoka Inyonga – Majimoto – Kibaoni – Sumbawanga – Tunduma – Zambia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii ni ya kimkakati. Barabara hii ni fupi, ambayo itarahisisha Wakazi wa Mkoa wa Mara, Mwanza, Shinyanga, Simiyu na Tabora wanaotaka kwenda Zambia kuliko kupita njia ndefu, ambayo itawalazimisha watoke Mwanza, waje Shinyanga, waje Tabora, waende Singida, waje Dodoma, waende Iringa, waitafute Mbeya kwenda Tunduma mpaka Zambia; badala yake barabara hii ikitengenezwa vizuri mkazi wa Mkoa wa Mwanza atatoka Mwanza – Shinyanga – Tabora, Tabora atakata Sikonge, Sikonge anaingia Inyonga, anaingia Majimoto – Sumbawanga – Tunduma – Zambia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nini faida yake? Faida yake ni itawapunguzia wananchi safari ndefu na mlolongo wa safari, ili kwenda Zambia, kwa ajili ya kujiletea maendeleo. Tutapunguza urefu wa safari na wananchi wetu watatumia muda mfupi, kwa ajili ya shughuli za maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninataka nichangie tena upande wa VETA. Kama ambavyo wenzangu wamechangia, VETA ni suluhisho pekee litakalowasaidia vijana ambao hawakusoma na waliosoma ili kujipatia ajira. Wakati ambapo sikuwa Mbunge niliwahi kumsikiliza Mbunge mmoja amechangia hapa, alisema mitaala ya VETA ibadilishwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi tuna mafundi simu, mafundi wa gereji, mafundi wa pikipiki na kila kada ina maeneo yake. Wale watu wengi kule hawakusoma, lakini wakipata mafunzo mazuri ya VETA, wakakusanywa vizuri, wale wote watakuwa na certificate ambazo zitawawezesha kwenda mahali na ku-apply kazi wakapata. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakuomba, tunalo tatizo hapa, kama ambavyo nimesema mwanzo, hakuna nchi ambayo inakwenda bila mpango. Amechangia jana kaka yangu, Mheshimiwa King, akasema tunapopitisha mpango huu ni vizuri tukaweka na Sheria. Usipoweka Sheria maana yake ni nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulipata tatizo, alifariki Rais wetu mpendwa, Dkt. John Pombe Magufuli akaingia Mama Samia Suluhu Hassan, isingekuwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ana utashi akakuta hii miradi mikubwa, mama huyu angekuwa ni mvivu, akaacha miradi hii leo tusingekuwa tunaongelea SGR imeanza, leo tusingekuwa tunaongelea Bwawa la Mwalimu Nyerere limeanza, leo tusingekuwa tunaongelea Kigongo Busisi. Haiwezekani miaka yote tunayokwenda tukapata Rais kama Mama Samia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, atakuja kutokea Rais hapa, wametengeneza mpango hauna sheria na kuna miradi mikubwa kama hii iliyokuwepo, anaamua kuacha anaanzisha ya kwake. Watambana na nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninawaomba sana na ninaiomba Serikali yangu, mawazo haya yanayotolewa na Wabunge ni vizuri yakazingatiwa. Kama ambavyo ukirudi kwenye Hansard kule kuna michango mizuri iliwahi kutolewa na Wabunge wakati tunatengeneza BRT Phase 1. Wapo Wabunge waliwahi kuchangia wakasema na wakashauri kuwa, hapa tunapotengeneza, tunapopitisha Jangwani hapa hapafai kuweka terminal panatakiwa kuwekwa daraja, lakini watu hawakusikia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wasipokuwa na mpango watakuwa wanakwenda na kurudi. Badala yake sasa leo Jangwani tunajenga Daraja, kwa nini? Hatukusikiliza ushauri na hatukuwa na mpango. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na ninaunga mkono hoja. (Makofi)