Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mpango Elekezi wa Maendeleo wa Muda Mrefu 2026/2027–2050/2051, Mapendekezo ya Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2026/2027–2030/2031 na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Mwaka 2026/2027; na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali Katika Muda wa Kati ya 2026/2027 hadi 2028/2029.

Hon. Rashid Mohamed Mtima

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Newala Mjni

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mpango Elekezi wa Maendeleo wa Muda Mrefu 2026/2027–2050/2051, Mapendekezo ya Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2026/2027–2030/2031 na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Mwaka 2026/2027; na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali Katika Muda wa Kati ya 2026/2027 hadi 2028/2029.

MHE. RASHID M. MTIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nichukue nafasi hii kukushukuru wewe binafsi kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa letu. Kwa sababu ni mara ya kwanza ninachangia, ninaomba kwanza nichukue nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu, kwa kuniwezesha kuwa sehemu ya Bunge hili la Kumi na Tatu. Nishukuru tena chama changu kwa kuniamini na kunipa nafasi ya kupeperusha bendera katika Jimbo la Newala Mjini kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninajua ni maamuzi ya viongozi wa kitaifa wakiongozwa na Mwenyekiti wa Chama chetu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, ninawashukuru sana. Vilevile, ninawashukuru pia viongozi wa mkoa wakiongozwa na Mwenyekiti wa Mkoa Mheshimiwa Saidi Nyengedi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninawashukuru sana pia wananchi wa Jimbo la Newala Mjini wakiongozwa na Kamisa wa Chama chetu aliyeko pale Alhaji Mwangi Rajab Kundya na Mwenyekiti wangu wa CCM Mheshimiwa Jabir Mtanda. Vilevile ninawashukuru sana wananchi hawa kwa kutoa kura nyingi sana 98% kwa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa nafasi ya Urais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikwambie tu wakati Mheshimiwa Rais akiwa mgombea, alivyokuja Mtwara nilimwambia kwamba Wana-Newala Mjini watakupa kura nyingi ambazo kwa Kimakonde ni kura za kumbambandija. Kwa hiyo, kwa 98% alizopewa ni kura za kubambandija kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan pamoja na Mheshimiwa Dkt. Emmanuel Nchimbi kwa kuaminiwa na Watanzania wote na kupewa kura za kutosha. Pia, nimpongeze Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba kwa kuteuliwa na kupewa nafasi hiyo kubwa kabisa inayosimamia utendaji wa nchi yetu. Katika hotuba yake ya kwanza ameonesha dira kabisa kwamba nini anakitaka Watanzania na watendaji wote waweze kutumikia Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze Mawaziri na Naibu Mawaziri wote kwa kuaminiwa na Mheshimiwa Rais kuweza kupeperusha utendaji katika Wizara zao. Pia, niwapongeze tena Mheshimiwa Mussa Azzan Zungu na wewe binafsi kwa kuchanguliwa katika nafasi zenu hizo. Vilevile, niwapongeze Wenyeviti wa Bunge, Wenyeviti na Makamu Wenyeviti wa Kamati ambazo zinasimamia utendaji wa Bunge hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hizo pongezi niombe sasa kuanza kuchangia mipango yote mitatu na Mwongozo wa Bajeti ya mwaka 2026/2027. Ninaomba nijikite eneo moja tu, eneo la kwanza, kigezo cha maendeleo ambayo sisi wenyewe tumejiwekea katika mpango kwamba kwa miaka 25 tunataka Mtanzania awe na kipato cha dola 7,000. Eneo hili ukiangalia kwa miaka mitano ya kwanza tumesema afike dola 1,638. Ukiangalia kwa kipato alichokuwa nacho sasa Mtanzania ni tofauti ya dola 361, sasa ukichukua hiyo dola 361 kwa awamu tano za miaka mitano hatufiki hiyo dola 7,000 kwa Mtanzania tutakapofika mwaka 2050. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamaanisha nini hapa? Ninamaanisha kigezo tulichojiwekea ni kikubwa ambacho tunatakiwa sisi kama Watanzania tuweze kuhakikisha kwamba tunaamua kwa dhati kuleta maendeleo kwa wananchi. Maendeleo katika mpango yanabebwa na nini? Yanabebwa na sekta ya uzalishaji, lakini ukisoma mipango hii hata ile ya nyuma inasema changamoto kubwa ambayo imewahi kutokea katika mipango ya nyuma ni uhafifu wa kuchangia sekta ya uzalishaji, ndiyo imefanya mipango mingi isiende kama tulivyotarajia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia kwa nchi yetu sekta ya uzalishaji kubwa ni ipi? Ambayo inabeba Watanzania wengi zaidi ya 54% inabeba hiyo, ni sekta ya kilimo. Kwa hiyo, ni lazima tuone kwa namna sekta ya kilimo tunaweza kuleta maendeleo makubwa ambayo yanawagusa Watanzania wengi ili wakifika mwaka 2050, basi waweze kuwa na kipato cha dola 7,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo kwa nchi yetu kina maeneo tofauti tofauti na mazao ambayo yanategemea maeneo tofauti tofauti. Nikizingatia eneo ambalo mimi ninatoka eneo la Newala, zao kubwa kule ni korosho. Tunaweza tukasema kwa namna gani tunajipanga kuhakikisha uzalishaji wa zao la korosho ambao umekuwa ukiongezeka basi uongezeke maradufu ili wananchi wa Newala Mjini inapofika mwaka 2050 waweze kupata kipata hicho cha dola 7,000. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa nilitaka nione, tuwe na dhamira ya dhati ya kuona je, kama wakulima wa korosho na mashamba yao waliyokuwa nayo kwa namna gani tunaboresha yale mashamba ili upatikanaji au mvunaji wa korosho atoke kwenye tani anazopata leo, basi aweze kupata tani zaidi, ili aweze kupata kipato cha zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninasema tulenge katika mazao yote si tu wakulima wa kubwa hata hawa wakulima wadogo, kwa nini? Kwa sababu tukileta nguvu kwa wakulima wadogo tukiwasaidia wakaweza kuongeza kipato chao tutaweza kuweka mazingira mazuri ya utofauti wa kipato kwa Watanzania. Kwa sababu hawa watakuwa wana kipato ambacho kitakuwa na uhakika tunavyoelekea mwaka 2050, kwa sababu tofauti kubwa ya kipato inaleta risk kwenye usalama wa nchi. Kwa hiyo, lazima wakulima wadogo wadogo tuwape nafasi, tuwasaidie na wenyewe tuwainue kwenye uchumi kuelekea hiyo dola 7,000 kwa mwaka 2050. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninatamani mpango huu twende tukaushushe kwa wakulima wadogo wadogo na namna gani tunaweza tukashusha mpango huu kwa wakulima wadogo wadogo? Ni kupitia katika halmashauri zetu kwa sababu kule ndiko wako Maafisa Ugani ambao wataweza kuwashauri wataweka record za wakulima wao kwenye maeneo yao na kuona je, wanajipanga vipi kumwezesha mkulima anayepata tani moja leo ili ikifika mwaka 2050 apate tani mbili, tatu kutoka katika shamba lao, hili linawezekana. Kwa hiyo, lazima Mpango huu tukashirikishe halmashauri, tushirikishe watendaji wa halmashauri kutokea Mkurugenzi, Madiwani, Wakuu wa Idara na kule chini kwa watu ambao wanaenda kusimamia kilimo chetu cha kila siku. Ninaomba sana Mpango huu uweze kuzingatia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tunapowasaidia wakulima wadogo wadogo wakaweza kuzalisha kwa mfano kwenye korosho baada ya mavuno tuwekeze kwenye kubangua. Korosho inayobanguliwa nchini kwetu ni ndogo sana ni tofauti na nchi nyingine za Afrika. Ivory Coast wanabangua zaidi yetu sisi, sisi tunabangua asilimia isiyovuka 20. Ivory Coast wanatafuta 80% kwenye ubanguaji. Kwa sababu korosho ghafi ukiuza unapata fedha ni kama robo ya bei ambayo ungeipata ungebangua. Kwa hiyo, hili litatu-assure wakulima wetu kuweza kupata fedha nyingi, lakini hata tutakapouza nje kuweza kupata fedha nyingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ubanguaji huu ukienda Newala leo unaanza kwenye kaya, mtu mmoja mmoja ana mashine ya kubangua na watu wanakuja kununua korosho iliyobanguliwa lakini vikundi vya akinamama. Tuwekeze na viwanda vikubwa viweze kubangua tuweze kuuza korosho ambayo imekuwa processed ambayo inatoa fedha nyingi kutafuta hiyo 7,000 ya mwaka 2050.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo hili tuliwekee nguvu kweli na si tu kwenye korosho, niseme mazao mengine maeneo mbalimbali tuweke kwenye large scale lakini vilevile, tuweke kwa mkulima mmoja mmoja ili kuwainua Watanzania wote kwa umoja wao. Tusije tukawaacha watu wenye uchumi mdogo chini huko vijijini ambao baadaye wanaweza wakahatarisha afya ya nchi hii kiusalama. Hilo nilikuwa ninataka nilichangie vilevile. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ukienda kwenye korosho kusini, nani anasimamia korosho? Ni vyama vya msingi. Ukienda kwenye Mpango tumezungumzia kuongeza idadi ya wanachama. Nilikuwa ninaomba mpango uangalie vilevile nani anaongoza ushirika? Tuweke mifumo ambayo tutapata viongozi waadilifu ambao watalinda fedha za wanachama wao na kuwapatia fedha zao ili tuweze kufika hiyo dola 7,000. Tukiwa na viongozi ambao wao wakikaa pale wanafanya wakulima wasipate haki yao ya msingi ya kilimo walichokifanya kwa mwaka mzima itakuwa tunawanyonya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, lazima Mpango nao uone na uweke mifumo ambayo tutapata viongozi kwa ajili ya ushirika, kwa sababu wao ndiyo wanaosimimia hili zao kule chini. Nilikuwa ninataka nishauri hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukimzungumzia Mtanzania kwenye sekta hiyo ya kilimo aweze kupata hizo...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Malizia Mheshimiwa, muda umekwisha.

MHE. RASHID M. MTIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa ninaomba tuwekeze kwenye umwagiliaji, huko nako tufanye Mtanzania awe anafanya kazi muda wote na kuweza kupata kipato muda wote. Pia, wanaosimamia Madiwani na viongozi wa Serikali za Mitaa, tuone namna ya kusimamia haki zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaunga mkono hoja. (Makofi)