Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Sex
Female
Party
CHAUMMA
Constituent
Special Seats
Contributions
nil
Answers
nil
Commettees
1
Ministries
nil
MHE. SIGRADA W. MLIGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa nafasi hii ili niweze kuchangia kwa ufupi sana Mpango wa Maendeleo 2025/2050. Mimi nina mambo machache sana ambayo yamekuwa yakisumbua kwa muda mrefu sana. Kuna issue ya vijana na akinamama na hiyo mikopo ya 10%. Kuna changamoto kubwa sana kwenye hii mikopo na changamoto siyo kwamba fedha hazipo, lakini pia changamoto siyo kwamba wananchi wanashindwa kukidhi vigezo
Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto kubwa ambayo nimeiona ni complications za namna ya kuipata hiyo mikopo. Hiyo mikopo imekuwa na complications nyingi sana. Complication ya kwanza walengwa kabisa watu wa chini hawaipati hiyo mikopo, lakini ukweli ni kwamba hiyo mikopo vinaundwa vikundi hewa vya watu wenye access ya kuifikia hiyo mikopo kwa kutanguliza watu ambao siyo walipaji na ndiyo maana ikija kusumbua, halmashauri zinapoanza kufuatilia zile fedha haziwaoni wahusika, ndiyo maana wanakutana na kitu kinaitwa vikundi hewa. Huo ndiyo ukweli, kwa sababu taarifa za hizi fedha haziwafikii watu ambao ni walengwa kule chini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ushauri wangu kwenye huu Mpango ambao unaendelea ambao unahusisha na haya mambo pia; kuna mtu alishauri hapa, hizi fedha ziwe na mlango maalum. Nimeona sasa hivi Serikali imepitisha hela upande wa wanawake na watoto kupitia Waziri wa Mambo ya Wanawake na Watoto; pia na Vijana; kuna fedha zimepitia kwa Waziri wa Michezo na Utamaduni (Mheshimiwa Makonda); kuna fedha zimeenda huko CRDB na NMB; na kuna fedha zinapitia halmashauri. Hivi vitu vinatuchanganya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia masharti ya hizi fedha, Wizara ya Michezo ina masharti yake; halmashauri wana masharti yao na ukija hizi fedha za NMB zina masharti yake. Kuna watu wamesema ni fedha ambazo hazina riba. Ukiangalia ule mwongozo unasema zile fedha zina riba ya asilimia saba. Ushauri wangu, kwa nini Serikali isitoke na format ya pamoja ili kusiwe na lugha tatu utafikiri kuna Serikali saba kwenye nchi moja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hizo fedha ambazo zinapatikana NMB, kwanza kuna mwongozo ulitolewa na Serikali kwamba watu wanaotakiwa kukopa hizo fedha ni watu ambao mtaji wao ni chini ya shilingi milioni nne. Ukiangalia hao watu maana yake ni watu ambao ni wajasiriamali na ninakumbuka kipindi cha Hayati Magufuli alitoa formula nyepesi sana kwamba watu ambao mitaji yao ni shilingi laki mbili, tatu, nne na tano (chini ya shilingi milioni nne) wawe na vitambulisho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ni hii hii miaka 65, lakini ule mpango ule baada ya Mheshimiwa Magufuli kufariki ule mpango nao haupo. Wale wajasiriamali wadogo wadogo wamerudishwa tena kwenye shilingi elfu sita kila mwezi, kitu ambacho tunawachanganya watu. Unavyowaambia tena hawa watu wawe na leseni wakati ukiangalia sheria ya kodi inamtambua mfanyabiashara ambaye ana mtaji wa kuanzia shilingi milioni nne kwenda juu. Hawa watu wamesema wawe na mtaji wa chini ya shilingi milioni nne. Huyu tax clearance anaitoa wapi? TIN Number anaitoa wapi? Leseni ya biashara anaitoa wapi? Wakati huyu wamemchukulia kama ni mjasiriamali mdogo ambaye analipa ushuru wa halmashauri husika. Kwa hiyo, kuna contradiction ambazo zinafanywa na Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mapendekezo yangu, tuwe na formality iliyo wazi ambapo watendaji wa vijiji na mitaa watawaambia direct watu wao. Hizo hizo fedha, kwa mfano za halmashari, wale wakopaji wa vikundi wawe wamechapisha mpangokazi wao. Baadaye watu wamechapisha wameenda kukopa fedha wakawaambia hapana hatutaki mpango uliochapishwa tunataka mpango ambao umeandikwa kwa mkono. Halafu hizo hizo fedha wanakopesha hawa watu wenye ulemavu. Masharti waliyoyaweka kwa watu wa kawaida wameweka na kwa watu wenye ulemavu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mtu hawezi hata kutembea, yeye amekaa tu pale kutembea hawezi unamwambia atoke kule Makete, nilikutana na walemavu Mheshimiwa Festo wanatoka kilometa karibu kumi na kitu kwenda halmashauri kupeleka hizo documents. Masharti ni yaleyale tofauti yake ni kwamba mlemavu anaweza kukopa peke yake, lakini masharti ya mwanasheria, sijui iandikwe. Mtu haoni unataka aandike ataandikaje na asaini mwenyewe kwa mkono wake? Kwa hiyo, issue siyo fedha, fedha ninaamini zipo, issue ni complications za namna ya kuzipata hizo fedha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, sisi Njombe Mungu ametubariki sana. Ninapata shida kuona Taifa kama la Tanzania ambalo tumebarikiwa kila kitu eti tunakosa fedha. Tunakosaje fedha nchi ambayo Njombe pale wilaya zaidi ya nne zina madini. Sisi kule Makete kuna madini, Ludewa kuna madini, Njombe Mjini pale kuna madini, lakini ukiangalia kwenye taarifa zenu nchi nzima wamefanya survey 16% tu ya sehemu ambazo tunamiliki madini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi leo hii Njombe hatukutakiwa kuwa na miradi yenye miaka sita haijakamilika. Haikutakiwa Njombe tukose hela za kukamilisha eti Barabara ya Ludewa – Njombe. Mimi huwa ninatafakari kwamba, hivi kweli huwa tunakaa mezani na kutafakari kwamba hii nchi tumebarikiwa? Ile Njombe ile, tuna miradi ya maji 2008 imekwama. Njombe ambayo ukiitazama kila kona, kila baada ya kilometa moja unakutana na mto, kila baada ya kilometa unakutana na mto. Huku mto, huku mto na huko mto.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati wa kampeni nilitafakari kitu kimoja. Wananchi wamefanikiwa kutoa maji bondeni kwenda kwenye vipalila. Sisi kule tuna kilimo maarufu kinaitwa vipalila, viazi vya kumwagilia. Mwananchi ndani ya siku 10 ameshatega maji mtoni ameyapandisha juu kwenye mashamba yake eka 20.
(Hapa kengele ya kwanza ililia)
MHE. SIGRADA W. MLIGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, dakika zangu zimeisha?
MBUNGE FULANI: Endelea.
MHE. SIGRADA W. MLIGO: Okay sawa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikawa ninajiuliza inawezekanaje mkulima wa viazi tena darasa la pili anapandisha maji kutoka mtoni ndani ya siku kumi amesambaza kwenye shamba lake la viazi halafu Serikali ina mradi wa 2008 na haujakwisha mpaka leo! Hivi inawezekanaje? Nikagundua, unajua Mheshimiwa Musukuma kuna vitu anaongea lakini ukimsikiliza vizuri unakuta kuna logic ingawaje huwa tunamcheka kidogo. Iko hivi, unakuta mkulima wa kawaida ambaye hana shule ana maarifa kuliko sisi ambao tuna PhD na degree. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikasema basi inawezekana tuwe tunajifunza basi hata kwa hao watu ambao wao hawakwenda shule ila ni wakulima. Kwa hiyo, ninavyozungumza hivi na ninaipa ushauri Serikali kwamba, tunavyokwenda kutekeleza hii mipango basi tuangalie hata ile miradi ambayo ilikuwepo toka enzi hizo za Kikwete na Magufuli. Kuna miradi hiyo Njombe labda kama hamna taarifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna Mradi wa Maji unaitwa Igongwi wa 2008. Haya ukija kwenye issue nyingine, kwa mfano uwanja wa ndege, mimi nimekuwa Diwani 2015 niliukuta uwanja wa ndege upo kwenye mipango kwamba tunataka Uwanja wa Ndege Njombe. Sasa hivi Njombe tuna wawekezaji wakubwa sana wanahitaji hiyo ndege ili waweze kusafirisha mazao yao na kuwahi issues zao. Mtu wa Njombe unaweza ukamkuta amevaa ndala lakini ana billions. Kwa hiyo, kupoteza shilingi milioni moja kwenda Dar es Salaam akawahi deal la shilingi milioni 800 haoni shida. Njombe wanahitaji ndege.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mkatuambia Baraza la Madiwani litafute eneo, mwaka 2015 hiyo. Tukatafuta eneo, na lipo mpaka leo, lakini mkatuambia tusimamishe wale wanaopatikana katika maeneo ya karibu, na hilo eneo ambalo tumehama, sasa wasiendeleze maeneo yao. Maskini, tukawasimamisha watu wanaoishi karibu na uwanja wa ndege kwa hoja kwamba, tunataka kuupanua. Miaka zaidi ya mitano wanasubiri tupanue uwanja, hatujawahi kupanua. Baada ya hiyo miaka mitano kwisha tumerudi tena, tunasema aah, aah, hapa hatupanui, tumehama, tunaenda Uwanja wa Ndege Kibena huko. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninavyozungumza hivi, hii issue ya Uwanja wa Ndege wa Njombe aliyoizungumzia Mheshimiwa Deodatus siyo ya jana, labda kwa sababu hawa Mawaziri ni wapya. Mimi nimeingia kwenye Baraza la Madiwani mwaka 2015, nimeikuta. Kuhamisha Uwanja wa Ndege tumepitisha sisi, na eneo tumetafuta sisi. Kwa hiyo, ninashauri, tunaomba uwanja wa ndege haraka, siyo stori mpya. Ni miaka 18 sasa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ninaishauri Serikali…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu muda umeisha, ahsanteni sana. (Makofi)