Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mpango Elekezi wa Maendeleo wa Muda Mrefu 2026/2027–2050/2051, Mapendekezo ya Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2026/2027–2030/2031 na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Mwaka 2026/2027; na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali Katika Muda wa Kati ya 2026/2027 hadi 2028/2029.

Hon. Prof. Pius Zebhe Yanda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Buhigwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mpango Elekezi wa Maendeleo wa Muda Mrefu 2026/2027–2050/2051, Mapendekezo ya Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2026/2027–2030/2031 na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Mwaka 2026/2027; na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali Katika Muda wa Kati ya 2026/2027 hadi 2028/2029.

MHE. PIUS Z. YANDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia na ninashukuru kwa sababu niliomba nitoe mchango kwenye hotuba ya Mheshimiwa Rais lakini sikupata nafasi. Awali ya yote ninaomba nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuchaguliwa kuwa Rais kwa kipindi kingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hiyo iko wazi kwamba ni kwa sababu aliweza kupata kura za kumwaga na ninaomba niweze kutoa taarifa kwamba katika Jimbo letu la Buhigwe, alipata kura 98%. Kwa hali hiyo naomba basi pia niweze kumshukuru yeye kama Mwenyekiti wa Chama Taifa, kwa kuweza kuteua jina langu ili niweze kupeperusha bendera ya Chama Cha Mapinduzi na wananchi wakaweza kunipigia kura za kutosha. Kwa hiyo, ninawashukuru pia Wanabuhigwe kwa kuniamini na kunipa kura za kutosha na ninawahakikishia ya kwamba nitawatendea haki katika kuwasilisha yale yanayowahusu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, niseme tu kwamba hizo kura nyingi zilizopatikana zilitokana na kazi kubwa ya Serikali ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kuwezesha miradi mbalimbali katika Jimbo la Buhigwe; tukizingatia kwamba Wilaya ya Buhigwe ni changa ikiwa na umri wa miaka 12, lakini tunavyoongea sasa hivi tumepata hospitali ya wilaya yenye vifaa vyote vya kiwango cha juu, tumeweza kupata barabara inayounganisha Mnanira na Kasulu ambayo ni link moja muhimu sana. Pia tumewezeshwa vituo vya afya, zahanati, shule za sekondari na shule za misingi ikiwemo shule ya watoto wa kike, ambayo ni boarding na iko dedicated kwa ajili ya wasichana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli, hayo yaliwafurahisha Wanabuhigwe wakaona kwa kweli wana kila sababu ya kutoa shukrani. Sasa baada ya kusema hayo naomba sasa niweze kuchangia kwenye hoja iliyoko mbele yetu, nikianza kwanza kuwapongeza Mawaziri waliowasilisha hiyo hoja, tukianza na Profesa Kitila Mkumbo ambaye ni Waziri wa Uwekezaji, lakini pia na Mheshimiwa Balozi Hamis Mussa Omar ambaye pia ni Waziri wa Fedha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kusema tu kwamba, ninaweza nika-confirm tu kwamba, hiyo mipango mitatu ya mwaka wa muda mrefu, mwaka wa muda wa kati na mwaka wa muda mfupi, imeweza ku-reflect yale yaliyoko kwenye dira lakini pia kwenye hotuba ya Mheshimiwa Rais. Nianze na sekta ya kilimo, ningependa kunukuu kwenye hotuba ya Mheshimiwa Rais ukurasa wa 20 ambayo inasema kwamba: “Katika miaka mitano ijayo tunaenda kufanya uwekezaji mkubwa kwenye sekta za uzalishaji tukianza na kilimo, tutaongozwa na dhana ya kilimo ni biashara, mkulima ni mwekezaji.” Kwa kweli huo ni mwelekeo unaolenga kufanya mapinduzi makubwa sana katika sekta ya kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mara kadhaa tumekuwa tunawaangalia wakulima kama ni wakulima ambao wanalima kilimo cha kujikimu. Sasa ukishaanza na neno hilo maana yake ni kwamba ni wakulima ambao wanalima ili waweze kupata tu kile kiasi kidogo cha kuwezesha familia yake kuweza kuishi, lakini tukija na mtazamo huu maana yake ni kwamba sasa wanapewa fursa wakulima waweze kuonekana kama wawekezaji wengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mambo mengi tunahitaji kufanya hivyo, moja ni kubadilisha mindset mtu ajue kabisa ana fursa ya kuweza kufanya shughuli zake za kilimo kama mwekezaji na sio mkulima wa kutafuta chakula cha kuweza kutumia ndani ya familia. La pili ni kwamba, tuangalie sasa mazingira wezeshi ya hawa wakulima ambao tunataka sasa wabadilike wawe ndio wawekezaji kama wawekezaji wengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ni kwamba, inabidi tuweze kufanya maandalizi ya wao kuweza kupata mikopo au mtaji katika mazingira rafiki. La pili, masuala ya miundombinu, kuna baadhi ya maeneo huko tunakotoka nikirejea Jimbo langu la Buhigwe; wakati wa masika kuna maeneo huwezi kufika na ninaomba nitoe ushuhuda tu kwamba mara kadhaa nimeenda nyumbani, nimeshindwa kufika kijijini kwangu. Sasa kama tunaweza tukaboresha miundombinu ambayo inaunganisha vijiji na maeneo mengine hasa kwenye maeneo ya masoko, basi maana yake ni kwamba watakuwa na uhakika wa kuweza kupata maeneo ya kuweza kuuza bidhaa zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kadhalika nikirejea Jimbo langu la Buhigwe ni jimbo ambalo ni wakulima wazuri wa matunda, nanasi, ndizi kwa wingi sana. Sasa kama tungeweza tukatengeneza mazingira ambayo wawekezaji wakaanza kuwekeza kwenye agro-processing industries maana yake ni kwamba thamani ya yale mazao yanayozalishwa basi yataweza kupata pesa kubwa zaidi na wananchi watahamasika kuendelea kulima kwa kiasi kikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nirejee mfano mwingine, Kata ya Munzezi na vijiji jirani wanalima tangawizi kwa kiasi kikubwa sana, lakini sasa wanauza kwa bei ya chini kwa sababu hawajaweza kuwezeshwa kuweza kupata uwekezaji wa kuweza kuchakata ile tangawizi ili kwamba waweze kupata faida katika kilimo chao. Tunamshukuru Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan wakati wa ziara ya kampeni, aliahidi kiwanda cha kuchakata tangawizi katika Kata ya Munzeze na ninaomba sasa Wizara husika iweze kulichukulia hilo jambo seriously ili kwamba wananchi waweze kufaidika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo tunapozungumzia barabara maana yake ni kwamba ni barabara zinazowezesha wafanyabiashara kuchukua mazao sehemu moja kupeleka sehemu nyingine hasa kwenye masoko. Kuna barabara moja ya msingi ambayo inatoka hayo maeneo ninayoyazungumzia ambayo wanalima tangawizi ambayo inakuja mpaka Buhigwe Mjini, inaenda mpaka Mwiyama na kuelekea huku kuungana na SGR.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni barabara ambayo ni kilio cha wananchi wa Buhigwe walio wengi, vijiji vingi. Bahati nzuri pia wakati wa ziara Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, aliahidi barabara hiyo iweze kujengwa kwa kiwango cha lami. Hii ilikuwa ni kuona kwamba anajaribu kutekeleza ile ndoto yake ya kuhakikisha kwamba sasa wakulima wa sasa hivi, waweze kuwa transformed kuwa wafanyabiashara wawekezaji kama wawekezaji wengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa mtazamo huu nataka nirejeshe suala la vijana kuwashirikisha kwenye kilimo. Ninafikiri hii ni fursa pekee ambayo tunaweza tukawashirikisha kwenye kilimo na hiyo itapunguza pia kasi ya vijana kutoka vijijini kwenda mjini. Changamoto moja ambayo ninaiona na ninafikiri hilo ni jambo ambalo ninaliweka hapa kwenye kikao hiki tukufu kwamba, tuanze kufikiria kwa kina, tuanze kutenda kitu kinaitwa Land Bank kama ambavyo kwenye ngazi ya kitaifa kuna Land bank kwa ajili ya wawekezaji wa nje basi tuwe na Land bank kwa ajili ya vijana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajua kila mwaka kuna idadi kubwa ya vijana wana-graduate kutoka sekondari, kutoka vyuo vikuu wanarudi vijijini je, hicho kilimo tunachozungumzia wataenda kulima wapi? Sasa hilo ni suala ambalo tunaweza tukaliangalia linaweza either likafanyika kwenye ngazi ya wilaya au mkoa, au Taifa lakini ni jambo la msingi sana. Kwa sababu otherwise itafika mahali na tukiangalia idadi ya watu inavyozidi kuongezeka maana yake ni kwamba wanaweza wakajikuta hawana maeneo hata kama tutawahamasisha kwamba waweze kuwa na kiu ya kuingia kwenye shughuli za kilimo, lakini maeneo yanaweza yasipatikane…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa kwa mchango wako, muda wako umeisha.

MHE. PIUS Z. YANDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na ninaomba kuwasilisha. (Makofi)