Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Ilemela
Contributions
nil
Answers
nil
Commettees
1
Ministries
nil
MHE. KAFITI W. KAFITI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nami nimshukuru sana Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema kwa kuendelea kutujaalia afya njema na kuwa pamoja hai katika Bunge hili Tukufu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee sana kuwashukuru wananchi wangu wa Jimbo la Ilemela kwa kuendelea kuniamini, nami kama kijana ninawaahidi kuendelea kuchapa kazi ndani ya Bunge na nje ya Bunge, kwa maana hiyo niwahakikishie kwamba wana jembe, mimi ni mtu wa vitendo na siyo mtu wa maneno. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba tena nichukue nafasi hii kumpongeza sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuwaamini vijana katika kusukuma gurudumu la maendeleo ya Taifa. Ndugu zangu ninaomba tu niwajulishe kwamba dhamira ya Rais katika kuhakikisha inawainua vijana kiuchumi imeendelea kudhihirika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunafahamu kwamba vijana ndiyo nguvu kazi ya Taifa, Taifa lolote ili liweze kuendelea linahitaji nguvu ya vijana, kwa hiyo vijana pamoja na kuwa nguvu kazi, tunaamini vijana ni mtaji na si liability katika Taifa letu. Dira yetu ya 2050 inahitaji kuwaongezea ujuzi na uimara vijana wote katika nchi yetu ya Tanzania. Kwa hiyo, kama Serikali na kama nchi kwa ujumla tunashukuru sana kwa kuendelea kuwaamini vijana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda kumpongeza sana Rais hata ukiangalia Bunge hili, wengi asilimia kubwa ni vijana. Kwa maana hiyo Taifa hili sasa linaongozwa na vijana na vijana tuliomo katika Bunge hili hatuna budi kuhakikisha tunawasimamia vijana wenzetu ili waweze kujikwamua kiuchumi. Vijana tumekuwa tukilalamika kuomba nafasi na kupewa nafasi za uwakilishi. Sasa nafasi tumepewa, ni jukumu letu ni kuhakikisha tunaonyesha njia kwa vijana wenzetu kwa kuleta maendeleo thabiti katika Taifa letu la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nimpongeze sana Waziri, kaka yangu Joel Nanauka. Rais hakukosea ametuleta Rais kijana, mzalendo, mchapakazi, muadilifu, mwenye hofu ya Mungu, tunamwamini na vijana tuko nyuma yake. Nasi tutampa ushirikiano wa kudumu na kuhakikisha yale matamanio ya Rais, matamanio ya Serikali, matamanio ya vijana wa nchi hii yanakwenda kukamilika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nami niongelee sasa mambo matatu leo nitaenda kusisitiza. Awali ya yote kwa sababu Rais amekuwa na nia thabiti ya kuwainua vijana. Wakati anafanya kampeni aliahidi kutoa zaidi ya bilioni 200 kwa vjijana wetu na bilioni 200 hizo zimeshaanza kutoka. Kwa hiyo, ndugu zangu ninaomba niwahakikishie kwamba vijana wote pesa hizi zilizotoka ni kwa ajili ya vijana wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pesa hizi zilizotoka haziangalii itikadi ya chama, dini wala kabila, vijana wote wenye sifa watakwenda kukopeshwa pesa hizi. Nami nimhakikishie Waziri, vijana tuko nyuma yake kuhakikisha hizi bilioni 200, ambazo Serikali imetenga, ambazo Rais amezielekeza kwa vijana, basi zinakwenda kufanya kazi ya kuwainua vijana mbalimbali kwenye Taifa letu la Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kuipongeza Serikali kwa kuendelea kutimiza ahadi yake, leo Wizara ya Vijana kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Vijana, tumeahidiwa kupata zaidi ya bilioni nane na mpaka saa hizi zaidi ya bilioni 2.5 zimeshatolewa kwa Wizara hii, pongezi kubwa kwa Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na yote hayo bado tunaamini hizi bilioni 200 bado zinahitaji kusimamiwa na Wizara hii ya Vijana. Tunafahamu pesa nyingi zimeweza kupelekwa katika Wizara Mtambuka, Wizara za Kisekta ili kuweza kukamilisha mahitaji kwa vijana. Tumeona kwamba kwa wale ambao vijana wana-deal na kilimo, pesa zao ziko Wizara ya Kilimo, wanao-deal na madini ziko Wizara ya Madini na sekta nyingine, lakini ninaomba tuwahakikishie kwamba vijana tutaendelea kutumia hii fursa na tuendelee kuitumia hii fursa kwa umakini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo kumekuwa na malalamiko pesa hizi hazitoki kwa wakati, kumekuwa na malalamiko vijana hawapati pesa hizi lakini pesa hizi zimekuwa zikitoka japo ninaweza nikasema kwamba bado Serikali inatakiwa iongeze pesa hizi ili kila kijana aweze kunufaika na mikopo hii na pesa ambazo zimetolewa na Rais. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kuchangia Wizara hii, vijana tunajukumu kubwa la kuhakikisha ajenda ya maendeleo na dira yetu ya 2050 tunakwenda kuitekeleza. Ukiangalia hata sensa za 2022 vijana ndiyo asilimia kubwa zaidi ya 60%, Maana yake nini? Dira hii ya 2050 bila kuwaimarisha vijana haitoweza kutekelezeka. Nasi vijana ndiyo lazima tuchukue msingi huu, ni lazima tusimame pamoja kuhakikisha dira hii tunakwenda kuitimiza kwa wivu mkubwa, kuhakikisha kila kijana ananufaika na pesa hizi ambazo Rais amezitoa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo niendelee kuipongeza Serikali kwa kuendelea kutenga pesa kwa ajili ya maendeleo ya vijana, kupitia Wizara hii zaidi ya bilioni tano zimetengwa kwa ajili ya maendeleo ya vijana. Kupanga ni jambo moja na utekelezaji ni jambo lingine. Katika miaka minne iliyopita kabla ya Wizara hii haijaanzishwa, Wizara hii ilikuwa inatengewa bilioni moja wakati ule ni Wizara ya Ajira, Kazi na Vijana, sasa hii Wizara inajitegemea, tunaomba hii bilioni tano kwa ajili ya maendeleo ya vijana iweze kutengwa na iweze kutolewa kwa wakati ili iweze kunufaisha vijana wetu. Kwa hiyo, katika eneo hilo ninaomba tuendelee kuiomba sana Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie wasaa huu vilevile kuomba sana vile Vyuo vya Maendeleo ya Vijana kwa maana Chuo chetu cha Morogoro cha Ilonga pamoja na Chuo chetu cha Songwe, Sasanda, Serikali iendelee kutoa pesa zaidi ya bilioni mbili zimeidhinishwa, sasa ninaiomba sana Serikali kuanzishwa kwa mafunzo haya ya muda mfupi yatakwenda kunufaisha vijana wengi katika maeneo ya kilimo, katika maeneo ya ujasiriamali, katika maeneo ya uzalendo kuhakikisha kila kijana ananufaika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine niombe tu kitu kimoja kwamba Serikali sasa ije na mpango wa kuwaandaa vijana wake, na hili nimekuwa nikichangia na nimekuwa nikiongea na Waziri wa Mipango, kwamba sasa ifikie wakati Serikali lazima ije na mpango wa kuhakikisha inawatoa vijana wake kutoka sehemu moja kwenda sehemu nyingine. Mfano, vijana leo wa Form Four wakimaliza wale ambao hawajafanikiwa kufaulu wanakwenda wapi? Vijana wa Form Six ambao hawakufaulu wanakwenda wapi? Vijana wanaomaliza Chuo Kikuu nini mpango wa Serikali kuhakikisha unawainua kiuchumi vijana hawa?
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo, Serikali ije na mpango huu, dira yetu ya 2050 itakwenda kutekelezeka kwa sababu tutajua mahitaji ya vijana hawa. Leo tumetoa bilioni 200 hatujafanya research je, ni vijana wangapi watakwenda kunufaika na kiwango hiki?
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo lingine labda kwa kumalizia kwa sababu tuko kwenye Wizara hot ya vijana na wanatusikiliza nitaomba muda wako kidogo na mimi kwa sababu ni Mjumbe wa Kamati hii vijana ndiyo kimbilio letu, kwa hiyo uniwie radhi kidogo tuna madini mazuri ya kuwaona kwamba vijana wengi wanakwenda kunufaika na Serikali hii ya Chama Cha Mapinduzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo la kilimo kupitia BBT tuendelee kuweka msisitizo, vijana wengi watakwenda kuajiriwa hapa. Tunafahamu tuna vijana wanatoka SUA, ni ajabu kumwona graduate wa SUA anakwenda kutafuta kazi wakati kuna nguvu kazi Serikali inaweza ikatoa mitaji na vijana hawa wakaenda kujiajiri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna vijana wanaomaliza mikataba JKT wakimaliza wanarudi mtaani, kwa nini tusiwaanzishie mashamba ya wao kujiajiri na kuweza kuchangia pato la Taifa? Kwa hiyo, tunafahamu tuna uhaba wa sukari, vijana waende tuwaanzishie mashamba na mitaji waende wakalime. Tunayo mahitaji ya alizeti, kwa maana ya kilimo kama nchi tuna mahitaji ya kutosha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kwa kumalizia tunapotoa bajeti hii ni lazima Serikali sasa ije na mpango kuhakikisha pesa zinazotoka zimekwenda kufanya nini? Zimesaidia vijana wangapi? Tuimarishe vitengo vya monitoring and evaluation ili kuona tija ya pesa hizi zinapotoka kweli zionekane zinawanufaisha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, niombe Wizara hii imeanzishwa ni Wizara mpya, tunao vijana ambao walikuwa chini ya maendeleo ya jamii kule kwenye Halmashauri. Sasa tuombe watoke kule warudi kwenye Wizara yao ya Vijana kwa sababu sasa Wizara ya Vijana iko kamili na inaendelea na shughuli zake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, ninaomba kuunga mkono hoja, vijana tukae mkao wa kula, sasa ni wakati wetu wa kuleta maendeleo kwa nchi yetu. Asanteni sana kwa kunisikiliza. (Makofi)