Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Kalambo
Contributions
nil
Answers
nil
Commettees
1
Ministries
nil
MHE. EDIFONSI J. KANONI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru sana kwa kunipa nafasi ili na mimi nichangie hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Maendeleo ya Vijana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, ninamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa nafasi siku ya leo. Pia ninamshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan. Pia, ninakishukuru sana Chama changu cha Mapinduzi Wilaya ya Kalambo na viongozi wote wa Chama cha CCM Mkoa, bila kuwasahau wananchi wangu wa Wilaya ya Kalambo ambao walinipa kura za kutosha ili niweze kuwawakilisha katika Bunge lako Tukufu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa maono yake makubwa kwa kuunda Wizara ya Vijana kwa ajili ya kuwakilisha vijana, na hasa kwa kumpata Mheshimiwa Waziri kijana ambaye ana maono makubwa kwa ajili ya kuwakilisha vijana katika Bunge lako Tukufu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninajielekeza kwenye mikopo. Mheshimiwa Rais amekuwa na maono makubwa kuhakikisha anawakwamua vijana kiuchumi, na hususan ukizingatia kuwa vijana ni wengi, ambao wako 76%, katika Taifa letu. Takwimu zinaonesha kuwa vijana wanaohitimu elimu ya vyuo vikuu ni kati ya vijana 500,000 mpaka 600,000 kwa mwaka. Tathmini katika miaka mitano mpaka miaka kumi tutakuwa na vijana karibu 7,000 mpaka 8,000 ambao watakuwa wamehitimu elimu mbalimbali katika vyuo vyetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais kwa kulizingatia hilo, na kwa kuwa na maono makubwa, akaweka mpango wa kuunda Wizara ya vijana na kuweka fedha kwa ajili ya kuwasaidia vijana. Hili ni jambo kubwa sana ambalo linatakiwa kuungwa mkono kwa nguvu zote kwa maono ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi fedha, shilingi bilioni 200 zimegawanyika katika Wizara za kisekta. Wazo langu, ninaishauri Serikali, fedha hizi zirudi katika sekta ya vijana ili vijana wawe wanajua kwamba fedha zetu ziko Ofisi ya Rais (Maendeleo ya Vijana). Zimeenda kilimo, zimeenda uvuvi, na zimeenda maendeleo ya jamii, zirudi kwa vijana ili Mheshimiwa Waziri awe anazisimamia mwenyewe. Sasa kama vijana wanaenda huku wanaambiwa rudi huku, hii haitaweza kuwasaidia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaiomba Serikali, nina imani sana Mheshimiwa Nanauka. Hawa vijana wana shida ya kuwa matajiri na Mheshimiwa Rais ndoto yake ni kutengeneza vijana wengi kuwa matajiri...
MHE. KANGI A. LUGOLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.
MWENYEKITI: Mheshimiwa Kanon kuna taarifa.
TAARIFA
MHE. KANGI A. LUGOLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa ninaomba nimpe taarifa Mheshimiwa Kanoni, kwamba hata hizi Wizara mbili zilipotoa matangazo ya mikopo kwa vijana, Wizara ya vijana walisema kijana aje na andiko lisilozidi kurasa tano, halafu Wizara ya Mifugo na Uvuvi ikasema kijana aje na andiko lisilozidi kurasa mbili. Utaona hata Wizara hizi zinapokuwa nyingi zinawachanganya vijana. Kwa hiyo, anachosema ni sahihi. (Makofi)
MWENYEKITI: Mheshimiwa Kanoni, unaipokea hiyo taarifa?
MHE. EDIFONSI J. KANONI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaipokea taarifa kwa mikono miwili. Ninasema hivyo kwa sababu gani? Mheshimiwa Rais ana malengo makubwa juu ya vijana wetu, na sisi kama Wabunge tunahitaji kuona vijana wanafanikiwa, na vijana wawe tayari kupokea mkopo kwa sababu hakuna mtu anayependa umaskini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama vijana wanamaliza vyuo vikuu halafu wanabaki, mimi mwenyewe ni mzazi ninaangalia, kama Mheshimiwa Rais anajitoa kutoa fedha kwa ajili ya kuwainua vijana kiuchumi, Serikali isisite kutoa fedha kwa ajili ya kwenda kwa vijana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vijana wanafuata hizi fedha kwenda kukopa, lakini masharti yanakuwa ni mengi. Tangazo la Serikali linasema Mheshimiwa Rais ametoa fedha kuwawezesha vijana kiuchumi. Wakienda benki wanakuta kuna masharti. Unamwambia kijana aliyetoka Chuo Kikuu aonyeshe biashara, ataonyesha biashara gani ambayo ameanzisha? Sasa hii inasababisha hizi fedha kukwama na hazitoki kama tunavyokusudia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kama zinabaki benki, ni kwa manufaa ya nani? Sheria zibadilishwe, usimamizi ubadilishwe, na masharti yapungue. Kama ni dhamana, Wabunge tupo, Madiwani wapo, Wenyeviti wa Serikali wapo, na wa vitongoji wapo. Masharti yawe nafuu, wakopeshwe vijana ili waweze kunufaika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninatokea Kalambo. Vijana zaidi ya 1,500 hawana kazi, lakini wana imani kubwa sana na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwamba hizi fedha zitawafikia na wao watanufaika kiuchumi. Hata hivyo, wanalalamika wakienda sekta ya benki wanakuta kuna masharti, wanaomba fedha mpaka miezi mitatu wanakata tamaa. Masharti yabadilishwe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunahitaji kutengeneza vijana wa dira ya miaka 25. Tunawatengeneza vipi kama hatuwezi kuwapa fursa za fedha? Wape imani hawa vijana. Uwezo wa kufanya kazi wanao. Serikali iwape imani, kusiwe na mashaka, na kusiwe na kigugumizi katika kuwapa fedha, watafanya mageuzi makubwa sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tuna lengo la miaka mitano miaka 20, au 25, hatuwezi kwenda bila hawa vijana. Uchumi wa nchi na uchumi wa dunia unaendeshwa na sekta binafsi. Sasa kama ni sekta binafsi, halafu mikopo inatoka kwa kusuasua, unategemea kitu gani kitatokea?
Mheshimiwa Mwenyekiti, sina mashaka na Mheshimiwa Waziri wa Wizara hii, Mheshimiwa Nanauka. Asimamie, na sisi kama Wabunge tupaze sauti hizi, fedha zirudi katika Wizara yenye dhamana na vijana ili waweze kuzisimamia wao wenyewe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninatoka ukanda wa kule Ziwa Tanganyika. Wale vijana wavuvi unamwambia aweke dhamana, anaweka dhamana gani? Wale vijana wengine ambao hawana shughuli, wako mtaani wataweka dhamana gani? Kwa hiyo, Serikali iamue namna ya kupunguza masharti ili vijana waweze kunufaika. Wako hapo wanasikiliza tunavyowasilisha hoja zao. Wananajaza fomu za maombi ya mikopo labda vijana 100 au 50, wanapata watu wachache kwa sababu ya masharti. Masharti yapungue.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, vikundi ambavyo vinasemwa, masharti ya kuunda vikundi siyo lazima. Ikiwezekana, kama kuna utaratibu, sheria zibadilishwe ili aweze kukopa mtu mmoja mmoja, kwa sababu kuna watu wanaingia kwenye vikundi na hawataki, na hawana sifa. Sasa analazimika kuingia kwenye kikundi, anakopa fedha, na mwisho marejesho yanakuwa yanakuwa ni ya shida...
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MWENYEKITI: Ahsante sana.
MHE. EDIFONSI J. KANONI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaunga mkono hoja.