Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Ngara
Contributions
nil
Answers
nil
Commettees
1
Ministries
nil
MHE. DOTTO J. BAHEMU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika Hotuba ya Mheshimiwa Waziri kuhusiana na maendeleo ya vijana. Nami nikiwa kama kijana, basi ninashukuru angalau nimepata nafasi hii ya kuzungumza na Serikali, na vilevile kuzungumza na vijana wenzangu nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa muda mrefu sisi kama vijana tumekuwa tuna changamoto nyingi ambazo kwa bahati mbaya zilikuwa hazipati ufumbuzi wa haraka kwa sababu zilikuwa zinashughulikiwa na idara. Tulikuwa ni idara ya vijana ambayo ilikuwa katika ofisi ambayo inashughulikia matatizo mengine mengi. Kwa hiyo, sisi vijana tulikuwa ni kama idara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunashukuru kwa mara ya kwanza katika uongozi wa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, sisi vijana tumetolewa kuwa kama idara, sasa tumekwenda kupewa Wizara rasmi ya kwenda kushughulikia matatizo yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais na tunampongeza sana kwa sababu tunaamini kwamba pamoja na matatizo mengi tuliyonayo sisi kama vijana, lakini hili la kutupa Wizara ambayo ita-deal na vijana pekee yake, angalau inatoa mwanga kwamba yapo mazuri mengi ambayo yanakuja kwa ajili ya vijana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Aweso kaka yangu huwa anasema kwamba “Asiyeshukuru kwa kidogo, hata kwa kikubwa hawezi kushukuru.” Kwa hiyo, vijana tunashukuru angalau kwa hili tu la kutupa visa. Sisi vijana, hili tu peke yake, tunashukuru, tunajua mambo mengine mengi yanakuja, Mheshimiwa Rais atakwenda kuyamaliza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile ninaomba kumpongeza kaka yangu Mheshimiwa Waziri, ameeleza katika hotuba yake mambo ambayo ameyafanya tangu amekabidhiwa hii Wizara. Ni Wizara mpya, lakini ameeleza mlolongo wa mambo mengi sana ambayo yamefanyika ndani ya kipindi kifupi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunampongeza yeye pamoja na watendaji wake. Tumekuwa tukiona vilevile ambavyo anaenda katika maeneo mbalimbali, anakunywa chai na bodaboda, anakula maandazi na mamalishe. Hii inaonyesha jinsi gani ambavyo Mheshimiwa Rais hakukosea kumpa Mheshimiwa Joel kuwa msimamizi wa sekta yetu sisi vijana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto zote ambazo zinahusu vijana, mwisho wa siku zinaongea katika eneo moja. Vijana inawezekana tunaambiwa tunahitaji vitu vingi, lakini tunahitaji kitu kimoja tu, fedha. Tunahitaji fedha, siyo kitu kingine chochote kile. Sasa fedha inapatikana kupitia njia mbalimbali; kuna ajira, kuna ujasiriamali, na vitu kama hivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hata mipango mingine yote ambayo tutakuwa nayo, kama kijana hatakuwa na fedha ina maana hatuna uhakika kama vijana tutakwenda kuridhika, kwa sababu changamoto nyingine kubwa sana ambayo inatajwa ni ajira.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kama vijana tukitendewa haki katika eneo hili kwenye hii Wizara yetu ya Vijana, vijana tukapata yale ambayo tunahitaji, ina maana hata tatizo la ajira kwa nchi yetu litakwenda kupungua kwa kiasi kikubwa sana, kwa sababu vijana wengi ndiyo ambao wanahitaji ajira. Ni kwa bahati mbaya kwamba ukiangalia jinsi ambavyo mambo yanaenda, hatuoni kama kuna mwanga wa tatizo la ajira kumalizika kwa siku za karibuni. Kwa hiyo, ambacho kinaweza kikafanywa na Serikali ni kutuwezesha sisi vijana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumemsikia Mheshimiwa Waziri amekuja na jambo zuri kuhusiana na Benki ya Vijana, tunapongeza sana kwa hili, lakini kabla Benki ya Vijana haijaanza, sisi vijana hapa katikati tunaishije?
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona tulipewa shilingi bilioni 200, lakini naungana na Waheshimiwa Wabunge wenzangu wengine wote ambao wamesema kwamba zile shilingi bilioni 200 zimeenda tofauti na vile ambavyo sisi vijana tulikuwa tumetarajia, zimeenda katika maeneo mengine mengi ambayo wengine hatuwezi kukajua huku kuna kiasi gani wala utatuma kiasi gani? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, kwa kipindi hiki ambacho bado tunasubiri Benki ya Vijana ianze, tumeshuhudia majanga mbalimbali ambayo yametokea kwenye nchi yetu, tumeshuhudia sehemu nyingi ambazo zimekuwa na changamoto, Serikali imepeleka ruzuku. Kwa hiyo, changamoto ya ajira kwa vijana, changamoto ya ukosefu wa kipato kwa vijana sasa hivi tunaomba Serikali basi ichukulie kama ni suala la dharura.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ikichukulia kama ni suala la dharura, ina maana hata ile shilingi bilioni 200 ambayo tumepewa, ambayo imeenda katika maeneo mengine tofauti, Serikali tunaomba ituongezee sisi vijana. Tunaomba Serikali itukopeshe twende tukapambane kutafuta fedha, tutarudisha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika maeneo ambayo Serikali inapeleka ruzuku ili mambo fulani yafanyike vizuri, lakini sisi hatutaki ruzuku, ninaomba mtukopeshe hizo fedha, na tutengenezewe mazingira mazuri ya kuzirejesha. Vilevile ninaomba tutengenezewe mazingira mazuri ya sisi kukubalika tuweze kukopesheka, kwa sababu changamoto kubwa ambayo inatukabili vijana ni kwamba ukienda utaambiwa njoo na dhamana, au vitu mbalimbali ambavyo lazima upeleke kwa ajili ya kupata mkopo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Serikali ikitudhamini yenyewe, Serikali ina watu mpaka ngazi ya kijiji, mpaka ngazi ya kitongoji ina watu ambao ni wasimamizi. Kwa hiyo, nikiomba mkopo, itajulikana Dotto anakaa sehemu fulani, Mwenyekiti wake wa Mtaa ni fulani, Mtendaji wa Kijiji ni fulani. Kwa hiyo, siwezi kutoroka na hizo fedha hata kama sina dhamana, lakini niaminiwe kwa kitambulisho cha NIDA, kwa vyeti vyangu vya shule, kwa uongozi wa Serikali ambao uko pale. Mniamini mnikopeshe ile fedha halafu mwone baada ya muda mrefu kama sitakuja kurejesha. Tukirejesha na wenzetu watapata; na mkitupatia, changamoto ya ajira itabaki ni historia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama leo mwanafunzi ambaye amemaliza chuo kikuu anaweza akaenda Kariakoo pale, akaongea na mtu mwenye duka akamwambia naomba tisheti 10 niende nikauze nikishauza nitakurejeshea fedha yako nami nipate cha kwangu, mtu mwenye duka anamwamini yule mwanafunzi, kwa nini Serikali isituamini sisi? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, imani tuliyonayo kwa Serikali yetu ni kubwa sana na haya mambo ambayo tunayaomba, tunayaomba tukiamini kwamba yanawezekana. Tumesikia fedha ambazo zimeenda sijui content creators, sijui nini, kila sehemu ambazo fedha zimeenda unaanza kuona watu wanakuwa wengi katika lile eneo. Siyo kwamba watu wanafanya vile vitu, lakini ndiko wameona ambako kuna fedha. Kwa hiyo hata zile fedha shilingi bilioni 200 zingebakizwa kwa vijana, sisi vijana ndiyo tunajua tunataka tufanye nini? Msitulazimishe kwenda sijui kufanya hiki, kufanya hiki, au kufanya hiki. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wangepeleka kwa vijana pale, sisi tutajua zile shilingi bilioni 200, Mheshimiwa Joel atajua yeye na vijana wenzake tuzigawane vipi twende tukafanye kazi tuweze kurudisha marejesho. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, changamoto kubwa ambayo inatukabili sisi vijana, ni kuwa walalamishi. Tunakuwa walalamishi kwa sababu kuna kikundi kidogo cha watu ambao wamejipa usemaji wa vijana kwamba wao ndio wasemaji wa vijana, lakini kile kikundi siyo kikundi sahihi, ni kikundi ambacho hakina suluhisho la vijana lolote. Ni kikundi ambacho kinatufundisha sisi vijana kulalamika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba kuongea na vijana wenzangu Waheshimiwa Wabunge. Vijana wenzangu Tanzania, tusikubali kuingizwa kwenye huo mkenge wa kuwa walalamishi kwa sababu ya watu wachache. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaye Rais, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye tayari ameshaonesha mwanga kwamba matatizo ya vijana yanawezekana. Tusikilize sauti zinazotoka kwa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan na kijana mwenzetu ambaye ameaminiwa, huyo ndiye awe msemaji wetu vijana. Tusikubali wahuni wengine wakabeba ajenda ya kutusemea sisi vijana wakati sisi vijana tupo, na tunajua kwamba matatizo yetu yanatafutiwa ufumbuzi kwa jinsi ambavyo Dira imeoneshwa na Rais wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninaomba kuwaasa vijana wenzangu Wabunge pamoja na vijana wenzangu kote kule walipo, tukatae wahuni, tumsikilize Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan na Mheshimiwa Waziri wetu. Hao ndio wamebeba maono ya Sekta ya Vijana na siyo mtu mwingine yeyote yule. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. (Makofi)