Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais, Maendeleo ya Vijana, kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

Hon. Fadhili Ally Liwaka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nachingwea

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais, Maendeleo ya Vijana, kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

MHE. FADHILI A. LIWAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami ninamshukuru Mwenyezi Mungu kwa rehema kubwa ya kuendelea kuwepo hapa tukiendelea kulijenga Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niruhusu pia kwa heshima kubwa na unyenyekevu, nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri, Ofisi ya Rais, Maendeleo ya Vijana, kaka yangu Mheshimiwa Joel Nanauka. Mosi, kwa kazi nzuri aliyoanza nayo ya kuitumia Wizara hii ambayo ni mpya; na la pili, kwa uwasilishaji mzuri ambao umebeba mapana na maono makubwa kwa ajili ya vijana wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara hii ni mpya, na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan aliamua kuianzisha makusudi ili kuweza kulipa nguvu Taifa la vijana walio wengi nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kufanya hivi ninataka nimhakikishie Mheshimiwa Waziri, anaweza asituone kwenye gari lake analopanda, anaweza asituone kwenye meza yake pale ofisini, anaweza asituone kwenye majukwaa mbalimbali ndani na nje ya nchi, lakini tunafikiri pamoja na yeye, tunawaza pamoja na yeye, tunaamua pamoja na yeye na tuongoza pamoja na yeye. Kwa lugha nyepesi, vijana wote wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tuko pamoja naye. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, fursa ya vijana kuweza kulitumikia Taifa hili iliasisiwa tangu kuanzishwa kwa Taifa hili, lakini tumekuwa na vipindi kadhaa ambavyo tumekuwa tukiitazama fursa rasmi ya vijana kuweza kushiriki moja kwa moja kwenye kuleta matokeo chanya. Hii ni kutokana na mabadiliko ya sayansi na teknolojia na dunia inavyokwenda sasa, na pia vijana wameongezeka, uhitaji umeongezeka, na tumekuwa na mahitaji makuwa ya kuingia kwenye maeneo mahususi ili kulijenga Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti na Waheshimiwa Wabunge, ni ukweli usiopingika kwamba hata kama tukiwa na nguvu ya kiasi gani, hatuwezi ku-satisfy mahitaji ya vijana kwenye soko la ajira tukawamaliza wote. Hiyo haiwezekani, lakini sisi kama nchi tunaweza kuwa na mipango mikakati na mwelekeo utakaowezesha vijana wetu kupata unafuu wa kuwa katika majukumu ya kila siku. Jambo hili ndilo dira ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuanzisha Wizara ya Maendeleo ya Vijana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yetu ina makundi mbalimbali ya vijana, na mimi nimekuwa muumini ninayeamini kwamba ni lazima tukatae dhana ya kuamini kwamba liko kundi la vijana linahesabika kama bomu. Makundi yote ya vijana nchi hii ni fursa, makundi yote ya vijana nchi hii ni ya uzalishaji, makundi yote ya nchi hii ni tegemeo la Taifa kwenye usalama wa nchi, uzalishaji na mwelekeo wa free country. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, makundi haya yote Serikali imedhamiria kuyaweka kwenye mwelekeo wa kuleta matokeo. Kundi la bodaboda tunalifikia, makundi ya machinga tunayafikia, makundi ya wachimbaji tunayafikia, makundi ya wakulima na wajasiriamali wote wenye ngazi ya ujana na kuelekea utu uzima kazi hii inafanywa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie Mheshimiwa Waziri kwamba sisi tuko tayari kabisa kumsaidia na kumshauri. Tunamwombea kwa Wizara zote zilizoko nchini zimfungulie milango aingie kwenye kila Wizara anayotaka. Wizara hii ni kama mtoto wa mwisho ambaye anaita kaka kushoto; anageuka, dada kulia, anageuka; mama mbele, anageuka. Atakwenda Wizara ya Madini kuna fursa za vijana afunguliwe milango ili vijana wapate manufaa. Tunayo Wizara ya Kilimo, kuna irrigation schemes nyingi nchi hii, afunguliwe milango ili vijana wapate fursa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajua ziko Wizara nyingi. Wizara ya Michezo ina wasanii, ina wacheza mpira, na ina wanamitindo. Hawa wote wako chini ya uratibu na usimamizi wa Wizara hii ya Maendeleo ya Vijana. Kwa hiyo, tuko hapa kuunga mkono Wizara hii, na pia kuondoa hofu kwa vijana, kwamba sasa wamepata mwarobanini wa masuala yao kuweza kujadiliwa kwa kina na kupatiwa utatuzi unaoeleweka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninataka nishauri maeneo machache. Eneo la kwanza ni eneo la viwanda. Utakubaliana na mimi kwamba nchi zote duniani ziliweza kufanya mapinduzi ya viwanda vidogo na vikubwa, walisaidia sana kupunguza ombwe la vijana waliokosa ajira. Kwa wale ambao wanasafiri kwa barabara ya kusini kuelekea Mkoa wa Lindi, wataona unapopita Mkuranga pale kuna viwanda. Ukipita usiku, ukipita mchana utaona idadi ya watu wanaokwenda kiwandani kupishana ili kufanya shughuli za kila siku. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lile linawezekana, na Wizara hii ina nguvu ya kufanya hivyo. Sisi tunaamini, kwamba kwa uwezo wa Waziri aliyeteuliwa, maarifa yake, uweledi wake, exposure aliyonayo, hawezi kuchoka kutafuta namna ya vijana kuingia kwenye soko la ajira kupitia viwanda mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nirudie tena eneo la pili katika ushauri, bado ninasisitiza eneo la kutazama juu ya kodi na mlolongo wa tozo nyingi katika shughuli za vijana. Vijana wanaoanza kutengeneza ujenzi wa Taifa hili wanaanza na mitaji midogo sana. Wanachohitaji wao ni fursa ya kufanya shughuli zao ili kufikia miradi mitaji mikubwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niliwahi kusema kwenye Bunge hili, tupunguze baadhi ya tozo na baadhi ya kodi kwenye fursa za vijana kwenye ajira zao ikiwemo waendesha bodaboda. Tulishaomba na ninamshukuru sana Mheshimiwa Waziri, alifanya kongamano kubwa ambalo lilikuwa na mgeni rasmi Mheshimiwa Waziri Mkuu. Vijana walileta hoja zao. Moja ya hoja kubwa waliyoleta ni pamoja na tozo hizi nyingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado tunao Wamachinga, bado ninaamini kwamba tunaweza kukusanya kidogo tukapata kingi na kila kijana akawa motivated kufanya kazi ya kiuchumi. Ninamwomba Mheshimiwa Waziri, tufanye mapitio vizuri kabisa ili kwenda kuona kundi lile la machinga tunapotaka kukusanya kutoka kwao, tunakusanya kwa namna gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hoja ya vitambulisho ilikuwa ni hoja nzuri na ilisaidia kupata kwa usahihi na kwa wingi, tuifikirie, lakini kama iko njia nyingine kupitia makundi na kupitia platform walizoziweka, basi ninamwomba Mheshimiwa Waziri, tushirikiane kwenye hili ili kuona fursa zao kule. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaelekea kumaliza mchango wangu. Sasa nchi hii imejengwa vizuri sana, na moja ya jambo kubwa ambalo watu wanalipigania ni siasa na maendeleo. Hata hivyo, na mtanisaidia, imekuwa tofauti kidogo. Wako wenzetu wengine wameichagua siasa kuyatia masikio ya vijana kauli zenye maumivu badala ya kauli zenye matumaini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nipo hapa kuwaomba vijana wa nchi hii, kwanza wawe na imani na Serikali ya Mheshimiwa Dkt. Samia. Pili, wajue kile tunachokifanya ni kwa ajili yao. Kwa bahati nzuri, niruhusu niseme kwa heshima kubwa sana, kwamba kaka yangu Mheshimiwa Ado Shaibu, yuko hapa ndani mtu ninayemheshimu sana, kwa sababu yupo kwenye chama kikubwa cha kisiasa chenye kusika ndani na nje, basi mimi na yeye na Wabunge wengine tusaidiane, tunapotoka nje kwenye platform zetu tuwaambie vijana juu ya kauli zinazoleta matumaini na siyo kuwalazimishia maumivu ambayo nchi haijachagua kuyafanya. Moja kati ya hayo, ni kutokuwatenga na mipango, sera na mwelekeo wa nchi hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, ninaunga mkono hoja. Ahsante sana kwa nafasi. (Makofi)