Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Mbulu Vijijini
Contributions
nil
Answers
nil
Commettees
1
Ministries
nil
MHE. DKT. EMANUEL Q. NUWAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kupata nafasi hii ya kuweza kuchangia kwenye bajeti hii ya Wizara ya Maendeleo ya Vijana. Pia ninapenda kuanza kwa andiko moja kutoka Waraka wa Kwanza wa Yohana 02:14 ambao unasema, “Nimewaandikia ninyi vijana kwa sababu mna nguvu.”
Mheshimiwa Mwenyekiti, Taifa letu lina vijana wa kutosha 34% ya population ambao wana nguvu na tunamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuwa na kizazi ambacho kina nguvu ndani ya Taifa letu la Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa vijana ambao Biblia inasema tunawaandikia, na kwa kuwa wana nguvu; Biblia inasema kwamba, pia wamejaa Neno la Mungu. Nami ninasema, wamejaa pia maarifa, ujuzi na uwezo wa kuchangia maendeleo ya nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunasema kwamba hawa vijana wetu ni rasilimali na ni fursa kwa ajili ya nchi yetu na wao wenyewe. Kwa hiyo, ninapenda kuanza na andiko hilo na kusema kwamba tutambue rasilimali hii kubwa ambayo nchi yetu imejaliwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaona kwamba pia hawa vijana wetu wanachangia asilimia kubwa sana ya nguvu kazi, zaidi ya 55%. Kwa hiyo, kama nchi kwa kweli ninampongeza Mheshimiwa Rais kwa kutambua kundi hili la vijana ambao ni zaidi ya 34%, kwa kuliundia Wizara kabisa ndani ya nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa vijana wetu wametawanyika, wapo vijijini na mijini. Vilevile, wana elimu tofauti, wengine wamemaliza darasa la saba, wengine hawajamaliza, wengine wapo Form Four, wengine vyuo, ngazi mbalimbali za elimu. Lazima tuwatambue na kuwapa fursa sawa za kuweza kuwaendeleza na kuweza kuchangia maendeleo ya nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kutambua mchango huu, Rais amefanya kazi kubwa, ndiyo maana ametoa ajira 12,000, ajira 5,000 sekta ya afya na 7,000 sekta ya elimu. Bado tumesikia juzi katika mwaka unaokuja zaidi ya 45,000 watakwenda kuajiriwa katika mwaka unaokuja. Kwa kweli ni mchango mkubwa sana ambao Serikali inaendelea kutambua nguvu kazi hii ambayo inakwenda kutumikia nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba sana kuunga mkono Wizara hii na kazi ambayo inaifanya. Ninapendekeza mambo machache. Jambo la kwanza, katika kupitia tumeona kuna vitengo vingi sana, lakini ningependa kupendekeza kwamba mahitaji ya vijana yanabadilika muda hadi muda, hivyo kuwepo na kitengo cha utafiti na ubunifu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mahitaji ya vijana yanabadilika sana, na vilevile vijana wetu ni wabunifu na wana talanta mbalimbali. Kuwe na kitengo ambacho kitatengewa fedha ili tuweze kutambua mahitaji ya vijana kadiri muda unavyokwenda, na pia umri wao unavyobadilika na mahitaji yao kutoka eneo hadi eneo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kitengo hiki pia kitatambua namna ya rasilimali fedha inayotengwa itakavyogawanywa. Mahitaji ya kijana wa Ilala ni tofauti na mahitaji ya kijana wa Nkasi na mahitaji ya kijana wa Nkasi ni tofauti na mahitaji ya kijana wa Mbulu. Kwa hiyo, tuweze kuona tusije tukaweka kwenye kapu moja, tuone namna ambavyo tutatambua mahitaji yao na kitakachotusaidia ni utafiti.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajua umri unawatofautisha, lakini pia jiografia inaweka tofauti ya mahitaji, elimu walizonazo pia inaweka tofauti ya mahitaji yao, na pia hata na jinsia. Kwa hiyo, ningependekeza kuwe na kitengo hicho na kitengewe fedha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba vijana kwa kuwa wana nguvu, wana uwezo na wana maarifa, lakini wana upungufu, tunahitaji kuwajengea uwezo; lakini je, tunahitaji kuwasikiliza?
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamshukuru na ninampongeza Mheshimiwa Waziri, ameanzisha vijana platforms. Ninaomba zile vijana platforms ziende mpaka ngazi ya kata. Zikifanyika katika ngazi ya halmashauri, changamoto ni kwamba wapo vijana ambao hawawezi kufika, ama kwa sababu ya miundombinu, ama kwa sababu ya uchumi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, twende mpaka ngazi ya kata, tuwasikilize vijana hawa, wana mawazo, wana maoni, wana ujuzi, wana vitu vyao, tuwasikilize ili tuweze kuwagawanyia fursa kulingana na mahitaji yao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe Serikali, pamoja na hayo, tunajua kwamba ili kutengeneza fursa za ajira, tunahitaji kutazama mambo kadha wa kadha. Moja ni mafunzo ya ujuzi kwa vijana wetu. Hawa vijana wapo makundi mengi sana. Wapo wenye elimu ya darasa la saba, wasio nayo, wenye Form Four, wenye Diploma, wenye Degree na wana mahitaji ya ajira pamoja na fursa za uchumi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tutazame kwa kuhakikisha kwamba tunatengeneza mwongozo wa mafunzo ambao utawakamata vijana wote hawa ambao utakwenda kuwasaidia kuwapa ujuzi na kuwapa maarifa kulingana na sekta zao na eneo ambalo wanafanyia kazi au eneo ambalo wanahitaji kujiendeleza. Kwa hiyo, tunaweza tukaandaa short courses au short contents ambazo zitawasaidia vijana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba suala la ujasiriamali na kuwajumuisha vijana katika maeneo yale ya upatikanaji wa fedha. Tunajua kuna elimu tofauti, tunajua kwamba wanahitaji mitaji, lakini ninaomba tuwe na mwongozo wa kuwasaidia vijana hawa katika eneo hili la ujasiriamali, na kuwajumuisha katika upatikanaji wa mitaji kwa ajili ya kujiendeleza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe mfano mmoja, tunahitaji mazingira wezeshi kwa ajili ya kuwawezesha vijana wetu. Kwa mfano, bodaboda tumewapa vijana, na tumewakopesha katika zile 10% na wapo watakaokuja kukopa, lakini vilevile wengine watakwenda kwenye kilimo. Wanapopita barabarani, kuna changamoto za kuadhibiwa kwa sera fulani fulani hasa za kukamatwa na kupigwa faini, na wanapopigwa faini tunawarudisha nyuma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, fikiria kwa mfano kijana ambaye anabeba gunia moja, anachajiwa labda shilingi 20,000 au 30,000 ya faini njiani. Tayari umeshamfilisi; iwe ni bodaboda, iwe anafanya shughuli za ujasiriamali katika kilimo. Kwa hiyo, tuone sera zetu na mazingira yetu yawe wezeshi kwa ajili ya kuwasaidia vijana wetu kujiajiri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tuna taasisi ambazo zinaajiri, tuone namna ambavyo tunaweka incentives; iwe ni tax incentives kwa zile taasisi ambazo zitaajiri vijana, iwe pia ni kwa kupata access to the capital incentives, tuweze kuona namna ya kufanya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie mambo mawili ya mwisho. Tunamshukuru Mheshimiwa Rais, tumepata shilingi bilioni 200 na tunashukuru kwamba vijana wengine wamependekeza kuwa na benki, Wizara itazame, lakini ninapendekeza namna ambavyo fedha hizi zitawafikia vijana, tuone routs ziwe tofauti tofauti.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuliona ile cheque wakati inakabidhiwa inakwenda CRDB Bank, lakini tuone benki ambazo zipo katika halmashauri zetu ziweze kutoa fursa ili vijana wetu waweze kupata hizi fedha katika maeneo wanapoishi bila kuingia gharama kubwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kuishauri Serikali katika eneo moja. Eneo lingine ni suala la kuweza kutengeneza mazingira ya vijana kutimiza masharti.
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MHE. DKT. EMANUEL Q. NUWAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamalizia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vijana hawa hawana NIDA, wala hawana leseni ya biashara. Katika ngazi za halmashauri na ngazi ya kata tuone namna ya kuwa na ofisi moja ambayo itawahudumia vijana hawa kwa wakati, na pia kwa urahisi ili kuweza kutimiza masharti ya mikopo na kuweza ku-access hizi fursa ambazo tunazitengeneza kupitia Serikali yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana, ninaunga mkono hoja. (Makofi)