Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

Hon. Fadhili Ally Liwaka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nachingwea

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

MHE. FADHILI A. LIWAKA: Mheshimiwa Spika, na mimi ninaungana na Wabunge wenzangu kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa rehema kubwa hii ya uzima, lakini ninatumia fursa hii adhimu sana kukushukuru wewe kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Spika, leo tuko hapa kama Taifa tukiwa na matumaini makubwa wakati ambapo Bunge letu linakwenda kupitisha bajeti hii ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa.

Mheshimiwa Spika, niruhusu kwa unyenyekevu mkubwa sana na heshima kubwa, kumpongeza sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye ndiyo amekuwa askari wa mstari wa mbele mwenye kupambania, kuyaishi, kuyainua na kuyahuisha maisha yetu Watanzania kwenye eneo hili la ulinzi na usalama, hususan katika eneo la majeshi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wewe utakuwa shuhuda na Wabunge wenzangu watakubaliana nami kwamba Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan amekuwa na kipaumbele kisichotia shaka juu ya usimamizi wa ulinzi katika maeneo ya mipaka na jamii zetu zinazozunguka. Amekuwa akitumia sera na maono yake katika kuhakikisha kwamba tunakuwa na Jeshi imara lililojikita katika masuala yenye ubobezi kwenye eneo la ulinzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaomba uniruhusu pia nimpongeze sana kaka yangu na ndugu yangu Waziri wa Ulinzi, Mheshimiwa Dkt. Rhimo Nyansaho kwa kazi kubwa ambayo anaifanya na hapa ametoka kuzungumza Mheshimiwa Kingu kwamba sambamba na kubeba jukumu zito la kuihudumia Wizara hii, lakini bado amebeba sura na taswira inayoakisi namna ambavyo kiongozi anayesimamia vyombo vya ulinzi anavyopaswa kuwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na amefika mbali akachukua maandiko yaliyobeba unyenyekevu ndani yake na kubeba nia ya mtu sahihi anayepaswa kuwapigania na kuwapambania wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Dkt. Nyansaho si mgeni kwetu, kwa sisi vijana wa rika yetu tumemsoma sana alipokuwa PSSSF, tumemsoma alipokuwa Azania, tumemsoma alipokuwa TIC, lakini tumemsoma alipokuwa TANESCO alipofanya kazi kubwa ya kurudisha matumaini kwenye eneo la umeme, na leo hii sishangai, sipati bumbuwazi nikimwona akiwa anatekeleza wajibu wake vizuri kwenye eneo hili nyeti na uti wa mgongo wa Taifa letu katika nyanja zote za kiuchumi, jamii na suala zima la kiusalama lenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, toka Jeshi letu limeundwa tangu kuvunjwavunjwa kwa jeshi la wakoloni na nchi yetu kupata uhuru na kuamua kujisimamia wenyewe na kuunda Jeshi la Wananchi wa Tanzania, jeshi hili halijawahi kutuangusha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama yako mataifa duniani yanaweza kufikia mwisho wa dunia, yakawekwa mbele ya hukumu, yakaulizwa tuambieni katika nchi na ardhi niliyowapa, mbele za Mungu, nini mliwahi kujivunia? Ukiacha ardhi, ukiacha maji, ukiacha uoto wa asili na mimea tuliyopewa pamoja na wanyama, jambo pekee tunalojivunia Watanzania ni kuwa na Jeshi imara, lenye nguvu, uzalendo na uwezo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika namna ya kibinadamu unaweza ukajiuliza, je, kama mimi nisingezaliwa Tanzania, neno amani na utulivu unaojengwa na jeshi imara ningeweza kuuona wapi?

Mheshimiwa Spika, ninataka nikiri mbele ya Bunge lako Tukufu kuwa, sisi Watanzania, sisi Wabunge, kama vile jeshi linavyotulinda kwa silaha, kwa akili na maarifa, ndivyo sisi wananchi na Wabunge tunavyowalinda wao kwa maombi, imani na maarifa yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jeshi letu limefanya kazi kubwa sana, limepambana katika maeneo ya ndani na nje ya nchi. Limejenga hehsima katika diplomasia ya Ulinzi, limejenga heshima katika uzalishaji mali, limejenga heshima katika masuala ya usalama. Kwa unyenyekevu mkubwa sana na heshima, ninaomba niwapongeze sana wasimamizi wa vyombo hivi. Ninampongeza sana Afande CDF Jacob Mkunda kwa kazi kubwa ya usimamizi anayoifanya na utulivu alioutengeneza kwenye jeshi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia ninampongeza Jenerali wa JKT kwa kazi kubwa anayoifanya ya ku-recruit vijana wetu, kuwatengeneza, hatimaye leo tunapoliona Jeshi la Tanzania tunaiona JKT iliyoandaliwa vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa, mimi nina maeneo machache sana ya kuweza kuchangia na kutengeneza ushauri wangu. Eneo la kwanza, ukiachana na shughuli za ulinzi wa mipaka, uzalishaji mali, lakini sisi sote tutakuwa mashahidi, tumeliona jeshi letu likishiriki katika masuala ya kijamii, masuala ya kuokoa, masuala ya kutengeneza comfort kwa watu na masuala yote yanayohusu majanga.

Mheshimiwa Spika, jeshi hili limefanya kazi kubwa pale Hanang, ndugu zangu wa Hanang watakuwa mashahidi namna jeshi lilivyofanya kazi yake vizuri. Jeshi hili limefanya kazi kubwa tulipopata majanga Kariakoo, watu wote wanajua na tunafahamu. Jeshi hili limesimamia ujenzi pale Msomera kwa nguvu kubwa, uwezo mkubwa na weledi mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ndiyo kusema kwamba mashaka yetu juu ya matumizi ya maarifa ya kijeshi hayaishii kwenye medani ya vita. Bado tunayapeleka kwenye medani ya maisha ya kijamii. Sasa tuna maeneo mawili ambayo niliomba kuchangia.

Mheshimiwa Spika, jambo la kwanza ni juu ya vijana wa Tanzania ambao wanamaliza kidato cha sita. Kwa sasa utaratibu tulionao ni wa kuwachukua vijana waliomaliza kidato cha sita kwenda kujitolea kwa mujibu wa sheria, lakini tunawaacha vijana wengi sana huko mtaani. Kwa kadri tunavyoona uwezo wa jeshi na namna wanajeshi wanavyokuwa, basi ni ombi langu na ninaamini Serikali yangu sikivu itaweka bajeti ya kutosha kupitia Wizara ya Fedha, ili vijana wote wanaomaliza kidato cha sita wasiende kwa mafungu, waende wote wanapokuwa wamemaliza, ili tukajenge Taifa la wasomi wenye uzalendo, ili tukajenge wataalamu wenye kuijua nchi hii, ili tukajenge wataalamu wasomi watakaokuja kulipigania Taifa hili kwa jasho, damu na nyama yao yote. Hilo ni eneo langu la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la pili, amezungumza vizuri Mheshimiwa Dkt. Jafo na nilimpenda aliposema jeshi letu limebeba heshima na matumaini. Kama kuna jambo la mwisho na ni tumaini kwa Watanzania, pale wanapomwona mwanajeshi kwenye jambo gumu, hapo wanakuwa wamemaliza matatizo yao yote.

Mheshimiwa Spika, wako wazee wetu wamepigana Vita vya Kagera, wako katika maeneo mbalimbali nchini. Wako kila wilaya na kila jimbo la Mbunge hapa. Ninaiomba sasa Wizara, ninashauri namna ya kufanyia kazi hili jambo.

Mheshimiwa Spika, kwenye kila wilaya kuna Kamati za Usalama, ninaomba tuwatumie Wakuu wa Wilaya waliopo na Wakuu wa Vikosi vya Mgambo walioko kule, kuwabaini wazee waliobakia ambao wamepigana kulipigania Taifa hili katika kuliokoa dhidi ya mashambulizi ya Idi Amin. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pale Kagera walifanya kazi kubwa sana. Sasa hawa wazee wanadai madai yao, na mimi sina mashaka Mheshimiwa Waziri katika jambo hili, tukilichukua vizuri tukaliweka kwenye utaratibu, wazee wetu hawa tutapata manufaa, tutajua namba yao na tutasaidia kuwaokoa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo ninaunga mkono hoja na ninashukuru sana kwa nafasi. (Makofi)