Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

Hon. Aisha Msantu Mduyah

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

MHE. AISHA M. MDUYAH: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Ikiwa mara yangu ya kwanza kuchangia katika Bunge hili Tukufu, ningependa nimshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema aliyeniwezesha kufika siku hii ya leo, nami jina langu limeandikwa katika Orodha ya Wabunge wa Bunge la Kumi na Tatu la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, ninapenda kumshukuru sana Mwenyekiti wangu wa Chama Cha Mapinduzi, ambaye ni Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan pamoja na vikao vyake vyote vilivyopita vya kuniteua mimi kugombea, lakini pia kuniteua kuwa Mbunge wa Viti Maalum ninayewakilisha watu wenye mahitaji maalum. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bila kuwasahau nipende kuwashukuru wanawake wote ambao ni Wajumbe wa Mkutano Mkuu Maalum wa UWT – Taifa chini ya Mwenyekiti wetu, mama yetu kipenzi, Mary Pius Chatanda kwa kunikopesha imani yao ndani ya hii miaka mitano 2025 - 2030 na ninachoweza kuahidi kwao ni ushirikiano uliotukuka katika utekelezaji wa Ilani yetu ya Chama Cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia niishukuru familia yangu pamoja na marafiki zangu ambao wamehakikisha kwamba ndoto zangu haziwezi kukwama mahali popote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikiwa ninaelekea katika kuchangia hotuba hii, ninapenda kuipongeza Wizara ya Nishati: Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Naibu Waziri, Menejimenti ya Wizara, pamoja na taasisi zote zilizoko hapo chini ya Wizara ya Nishati kwa juhudi kubwa wanazoziweka katika kuhakikisha kwamba Taifa letu linasonga mbele kwenye sekta ya nishati. Tunaona REA wanavyoweka juhudi zao kubwa katika kuhakikisha kwamba vitongojini pia tunapata umeme na wameweza kuanza na vitongoji 9,009. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaona pia Serikali yetu namna ambavyo hailali usiku na mchana kuhakikisha kwamba mafuta siyo kikwazo katika nchi yetu na kuhakikisha pia masuala ya kiuchumi na kijamii hayakwami kwa kigezo cha mafuta. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ninapenda pia kuipongeza Wizara yetu kwa kuendelea kuibua vyanzo mbalimbali vya nishati. Tunaona nishati ya jua, nishati ya umeme wa maji, lakini pia gesi asilia na joto ardhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikiwa ninaelekea katika kuchangia hotuba hii nikianza na suala la nishati safi, sisi kama Taifa kwanza tunajivunia kuwa na kinara wetu wa masuala ya nishati safi ambaye ni Rais wetu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan. Hata jana tu tumeona akitoa mitungi ya gesi kwa mama lishe na baba lishe Jijini Dar es Salaam. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hili ninaipongeza pia Wizara kwa kuendelea kutoa elimu kwa wananchi, lakini pia kutoa majiko banifu yenye bei ya ruzuku na kuhakikisha kwamba nishati safi inamfikia kila mwananchi. Ninaomba tu waendelee kutoa elimu hii na kuhakikisha kwamba kila mwananchi aliyeko mjini na pembezoni mwa mji anajua umuhimu wa kutumia nishati safi, kwani tukiongelea kuhusu masuala ya athari za mabadiliko ya tabianchi, basi wanawake, watoto, na watu wenye ulemavu huathirika zaidi. Hata takwimu zinatuambia kwamba watu wenye ulemavu wanaathirika mara mbili zaidi kukitokea athari zozote ikiwemo mafuriko, ukame na vitu vingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninapenda pia kupendekeza kwamba tuwe na National Clean Cooking Energy Coordination Framework. Leo hii unaweza ukafika ndani ya nyumba moja ya mwananchi ukakuta ana mitungi hata mitano hadi sita ambayo amepewa na watu kadhaa. Amepewa mitungi hii na Mbunge wake wa jimbo, akaja Mbunge wa Viti Maalum akampatia, wakaja STAMICO kupitia mkaa wao mbadala wakampatia na wadau wengine wa nishati safi pia wakampatia, hali ya kuwa jirani yake hana hata mtungi mmoja wa gesi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kukiwa kuna huu mfumo wa uratibu tunahakikisha kwamba wananchi wote wanapata nishati safi, lakini pia upatikanaji wake unakuwa nafuu na pia inawezesha hata wale waliopo pembezoni wanaweza kuji-coordinate kuweza kupata.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hii pia niweze kupendekeza kwamba fursa hizi kama tunavyoona Wizara ya Nishati inavyotoa mikopo, vituo vya mafuta vinajengwa pembezoni mwa miji, basi itoe pia mikopo hii kwa vikundi vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu, hasa waliopo pembezoni mwa miji waweze kupata mikopo hii na kuweza kuuza nishati hii kwa bei nafuu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, ninapenda kuongelea kwenye suala la Local Content. Sisi kama Taifa tunajivunia kuwa na sera hii, lakini pia ni Watanzania wachache sana ambao wanafahamu hivyo. Kwa hiyo, ninapendekeza Wizara iweze kuelezea zabuni ambazo ziko chini yake, ambazo ni specific kwa ajili ya Watanzania. Pia, ihakikishe kwamba wakandarasi hawa wa sekta ya nishati wanahakikisha kwamba zabuni hizo zinaenda kwa Watanzania pekee. Hali hii itafanya uchumi wetu uzidi kukua kwa Mtanzania mmoja mmoja, lakini pia Taifa kiujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mwisho, ninapenda pia kuipongeza Wizara ya Nishati kwa kuhakikisha kwamba vijana wanaendelea kupata ujuzi. Tunaona vijana wengi wanaji-engage na miradi ya mikakati ikiwepo wa ECO ambapo wanaenda kupata skills kutoka kwa wakandarasi ambao wako nje. Ninatoa tu wito kwa vijana wenzangu kuendelea kupata ujuzi kwenye sekta ya nishati safi, vijana wote ikiwemo watu wenye ulemavu, kwani tunatambua kwamba mnyororo wa thamani ni mkubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie fursa hii kuwatia moyo, kwa ni mimi pia hali ya kuwa nina ulemavu, lakini nimesomea Uhandisi wa Mafuta na Gesi. Kwa maana hiyo, vyote vinawezekana kwa vijana wenzangu hasa wenye ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mchango huu mchache nilioutoa na kwa moyo wa dhati, ninaomba niunge mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)