Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

Hon. Onesmo Merdson Mnkondya

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbozi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

MHE. ONESMO M. MNKONDYA: Mheshimiwa Naibu Spika, Ninakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia bajeti ambayo imewasilishwa na Wizara ya Nishati na Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ninampongeza Mheshimiwa Waziri kwa kazi nzuri anayoifanya na ninakiri kupokea umeme kwangu kule vitongoji 39, japo nina vitongoji 80 vimebaki, lakini kwa mpango wa Serikali nina uhakika kuelekea mwaka 2030 kama ambavyo Ilani ya chama chetu inasema vitakuwa vimekamilika. Kwa hiyo, sina shaka na Mheshimiwa Waziri, nimeona mipango yake kwenye Wizara kwamba vitongoji vyote vinakwenda kufikiwa na umeme.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesimama leo hii kwanza kwa sababu kuu ambayo inatupata sisi watu wa Songwe. Watu wa Songwe hatuna umeme wa uhakika. Hivi nilivyosimama hivi leo umeme Mkoa wa Songwe ni mara nyingi sana unakatika katika na umekuwa ni maarufu kwa Mkoa wetu wa Songwe. Yaani unaweza ukasema tuko gizani sasa. Hili jambo sisi kama Wabunge kwa kweli limeleta shida sana kwa mkoa wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumewaambia wananchi wetu kwamba muwe na subira. Sisi ni wawakilishi wenu tutakwenda Bungeni kuwasemea na ikiwezekana hivi nimesimama Mheshimiwa Waziri, unapokwenda kuwasilisha hotuba yako (kumaliza) ninakuomba tu; kwa namna ambavyo tuna tatizo Mkoa wa Songwe la katikakatika ya umeme. Hii inatokana na kwamba sisi watu wa Songwe tunachukua umeme kutoka pale Mbeya. Kuna kituo kimoja kinaitwa Mwakibete cha kupozea umeme.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukimuuliza hata mtoto mdogo leo ukimuuliza Mwakibete ni nini, atakuambia ndiye anayetukatia umeme. Yaani hiki kituo cha kupozea umeme kimekuwa ni maarufu mno. Kwetu imekuwa ni kero. Matangazo yote yanayokuja na watu wa TANESCO, tatizo Mwakibete. Ni kweli, sasa kama mtu mwingine anatu-control sisi Watu wa Songwe, tutashindwaje kukosa umeme? Control zote zipo kwao, wakiwa na jambo lao lolote lile watakata tu umeme Mkoa wa Songwe tunakosa umeme. Laini yote tunakosa umeme, tena siyo Mbozi tu peke yangu, wilaya zote za Mkoa wa Songwe majimbo yote ya Mkoa wa Songwe, Wabunge wako hapa wanajua hilo, kwamba kelele ni umeme Mkoa wa Songwe. Tunakosa wawekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi wakulima kuna uzalishaji wa hali ya juu kule. Wafanyabiashara, viwanda vidogovidogo haviendelei wajasirimali wadogo hawawezi kufanya kazi kwa sababu umeme haupo, siyo wa uhakika. Ninaamini atakuja na mpango wa dharura wa kutusaidia watu wa Songwe wakati tunasubiri huu Mradi wa TAZA unaokwenda kukamilika. Kwa kweli umeme Mkoa wa Songwe hauridhishi. Hatuko salama kwenye umeme. Ninaomba Mheshimiwa Waziri alichukue hili na atusaidie tupe majibu. Hivi wananchi wa Mkoa wa Songwe wanasubiri Serikali inakwenda kusemaje. Sina shaka na Waziri anakwenda kuwajibu na kutuma wataalam huko wakatuangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, inawezekana ndiyo, toka tuchukue hii laini mpaka sasa, wakati tunaanza na hii laini ya kutoka Mbeya kuja Songwe ilikuwa na watumiaji 68,000. Sasa watumiaji wameongezeka kwenda 144,000. Ni pongezi kwa Serikali kuongeza watumiaji, ndiyo hivyo vitongoji vimeshapata umeme na ongezeko ni watu 80,000. Sasa, bado tunatumia laini ile ile na miundominu ile ile. Hapana, Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo ambalo ninataka nishauri sasa, kupitia mradi ambao unaelekea kutukomboa sisi watu wa Songwe wa TAZA. Mradi huu ni mzuri, ni mpango mzuri wa Serikali, lakini mradi huu ulikuwa umepangwa ukamilike tarehe 21 Mei, 2026, bado mwezi mmoja. Hivi ni kweli unakwenda kukamilika? Tatizo linakuja kwa wakandarasi wanaotekeleza huu mradi. Inawezekana hawawasimamii vizuri. Sasa, Mheshimiwa Waziri hawa wakandarasi wasimamiwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpe Waziri mfano wa wakandarasi hawa; mkandarasi kutoka Iringa kuja Kisada amekamilika hana tatizo. Mkandarasi kuja hapa Kisada sijui panaitwa Sasada, kuja Mbeya…

MBUNGE FULANI: Kisada.

MHE. ONESMO M. MNKONDYA: Kisada yes, kuja Mbeya yuko slow mno, yuko taratibu sana. Mpaka hivi ninavyozungumza, kati ya nguzo 495 amesimamisha nguzo 199, bado nguzo 296, atamaliza? Huyu ndiye atakayechelewesha. Mpango mahsusi uende kwa huyu mkandarasi, kama ni kusimamiwa asimamiwe. Atatuchelewesha sisi watu wa Songwe kupata umeme.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukitoka hapo mkandarasi wa kutoka Mbeya kuja kwetu Songwe hadi Nkangamo, Kituo cha Kupozea Umeme yuko vizuri, bado nguzo sita tu. Huyo hatuna shaka naye.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine litakalochelewesha mradi huu ni kile Kituo cha Kupozea Umeme Nkangamo, mpaka sasa mkandarasi hajaanza kusafirisha zile transformer kutoka bandarini kwenda Songwe na tunajua zile transformer zilivyo na uzito, sidhani kama ana gari za kwenda kusafirisha zile transformer kwa wakati. Ninaamini hatakuwa na uwezo huo. Sasa, nini cha kufanya ili kumsaidia na transformer moja ya kusafiri ni kati ya siku 28 na kuendelea? Ili kumsaidia Serikali yetu, ninaamini ina uwezo mkubwa tu, ipeleke gari zenye uwezo wa kubeba mizani mizito ili aweze kusaidiwa huyu mkandarasi, aweze kuleta transformer akamilishe mradi wake pale Nkangamo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye uwasilishaji wa Mheshimiwa Waziri, kwa kweli ninampongeza sana. Wakati ninaendelea kutafakari namna gani tutakavyopokea huu umeme sisi Watu wa Songwe, kama sasa tuna changamoto na Kituo cha Kupooza Umeme cha Mwakibete Mbeya na sasa wameturuka vilevile kituo cha kupooza umeme kutoka Mbeya kimeenda mpaka wapi? Nkangamo!

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ninawaza hivi umeme huu utatoka Nkangamo uanze kurudi tena Songwe. Makao Makuu ya Songwe jamani yako Mbozi. Tunapaswa kuwa na substation mahali hapa tu-control wenyewe ule umeme. Sasa uende kule urudi huku, hivi inawezekana? Itakuwa ni hali ile ile. Kitakachotokea kule Nkangamo ndicho kitakachotuathiri huku. Mpaka tuje tu-solve hilo tatizo muda ushakwenda. Ninamwomba Mheshimiwa Waziri, kutoka Mbeya tatizo lilikuwa lile lile. Waje watuwekee substation Mbozi Makao Makuu pale, watu wa-control pale ili tusipate shida ambayo tunaipata sasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninajua kule Nkangamo ni mahsusi kwa ajili ya Zambia, ni mahsusi kwa ajili ya wenzetu wa Rukwa na kuendelea, lakini kwetu hatutapata manufaa. Wakati kengele ya kwanza inagonga, ninaomba nimalizie kwa kusema kwanza ninampongeza sana Meneja wa TANESCO Mkoa, ni kijana mzuri, kijana mdogo kama mimi tu. Kazi anayoifanya, pamoja na kukatikakatika umeme ni nzuri, anaitwa Engineer Chonya. Anafanya kazi nzuri usiku wote, kwanza anatoa ushirikiano mzuri, ila anazidiwa na wenzetu wa kule kwenye kituo ambacho kinatuletea shida hapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa huyu Meneja, Mkoa wetu wa Songwe hatuna Ofisi ya TANESCO. Hivi ninavyozungumza anatoka kwenye nyumba ya kupanga ndio ofisi, jengo la kupanga ndio ofisi. Kweli kwa mkoa wenye hadhi kabisa, kesho kutwa tu tunaenda kupata Manispaa, tuendelee kutumia ofisi ya kupanga, kweli? Hawa watu wana kiwanja. Mheshimiwa Waziri wajengee ofisi, ili kuwanusuru na wenyewe angalau wawe na uwezo wa kufanya kazi, wawe na ofisi yao badala ya kupanga.

Mheshimiwa Naibu Spika, meneja huyu ndiye anayefanya kazi pia, kama meneja wa wilaya yetu, lakini kazi yake ni nzuri, wamjengee ofisi. Ninaomba sana Serikali ichukue jambo hili la umeme kukatikakatika kwa Mkoa wetu wa Songwe, kama jambo la dharura kwa Wanasongwe tuondokane na giza ambalo tuponalo sasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru sana kwa nafasi ambayo umenipa na mchango ambao nimeutoa kwa rafiki yangu Mheshimiwa Waziri. Ninaamini Wanasongwe wanakwenda kunufaika kuanzia kesho na kuendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana na ninaunga mkono hoja. (Makofi)