Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Kakonko
Contributions
nil
Answers
nil
Commettees
1
Ministries
nil
MHE. ALAN T. MVANO: Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii. Awali ya yote, nimshukuru sana Mwenyezi Mungu ambaye anaendelea kutujalia afya sisi sote. Nitumie vilevile nafasi hii kumpongeza sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoifanya na niwapongeze sana Waziri wetu wa Nishati, Naibu Waziri wa Nishati na timu yote ambayo inamsaidia majukumu. Kwa kweli, kazi kubwa inafanyika na mwenye macho haambiwi tazama. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na mambo mengine yote ninayoweza kuyasema ni kwamba lazima nianze na pongezi kwa sababu mimi ninatokea Kakonko katika Mkoa wa Kigoma, Mkoa wa Kigoma hapa tunavyozungumza tayari umekwishaunganishwa kwenye gridi ya Taifa. Ndiyo maana tunaona katika Mkoa wa Kigoma viwanda sasa vinajengwa. Ukienda Kigoma Mjini utaona Kiwanda cha Cement, utaona Kiwanda cha Nondo, utaona Kiwanda cha Kuchakata Asali, kuna Viwanda pale vya Kusindika na Kuchakata Samaki.
Mheshimiwa Naibu Spika, ukija kwenye Wilaya ya Kasulu utaona Kiwanda cha Sukari. Tunaamini mpango mzuri wa Serikali hii kwamba Kiwanda cha Kuchakata Zao la Muhogo katika maeneo ya Kakonko na Kibondo tunaamini hili nalo litafanikiwa kwa sababu tayari tunao umeme wa uhakika. Hizi ni pongezi kubwa sana na lazima tuziseme. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo Wilaya ya Kakonko ina vijiji 44 na vitongoji…
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Alan, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Festo Sanga.
TAARIFA
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa yangu ni fupi tu.
Mheshimiwa Naibu Spika, wakati Mbunge anachangia hapa pia Watanzania wakumbuke kwamba Mkoa huu ulikuwa unatumia diesel ya takribani shilingi bilioni 21 kwa mwaka, lakini kwa juhudi ya Dkt. Samia Suluhu Hassan kuunganisha gridi ya Taifa, tumeokoa shilingi bilioni 21 kwa mwaka kwa matumizi ya diesel. (Makofi)
MHE. ALAN T. MVANO: Mheshimiwa Naibu Spika, ninashukuru sana na ninaipokea taarifa.
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mbunge subiri, taarifa ya Mheshimiwa Sanga, unaipokea? (Kicheko)
MHE. ALAN T. MVANO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana na ninaipokea taarifa. Kimsingi Watanzania watambue kwamba Mkoa wa Kigoma unatambua sana jitihada kubwa zinazofanyika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, yapo mengi ningeweza kuyasema, lakini kwa sababu ya muda niseme hivi, Wilaya ya Kakonko pekee vijiji vyote 44 hivi tunavyozungumza vina umeme, kati ya vitongoji 355, vimebakia vitongoji takribani 50 tu, vingine vyote vina umeme. Kwa hiyo, lazima nitoe shukrani nyingi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tumeona jitihada za Serikali, tarehe 17 ya mwezi Januari ulisainiwa mkataba wa shilingi trilioni 1.2 ambapo vitongoji 9,009 vilikuwa vinakwenda sasa kunufaika na umeme vijijini. Kwenye mpango ule Serikali hii njema imesema Mkoa wa Kigoma, Mkoa wa Kilimanjaro na Mkoa wa Katavi vitongoji vyote vinakwenda kupata umeme kupitia kwenye mkataba huo. Ninaomba kwa niaba ya wananchi wa mikoa hii nifikishe shukurani hizi nyingi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na shukrani hizo, yapo mapendekezo. Jambo la kwanza ambalo ninapendekeza ni kwamba, tunatamani sana kuona kazi kubwa inaendelea na tayari mipango mizuri tumeiona, jambo la umuhimu ni kwamba umeme umeshakwishafika kwenye vitongoji vingi, hamu ya wananchi sasa ni kuona umeme unasambaa ndani ya vitongoji. Kwa hiyo, hili ni jambo muhimu na wananchi wanatamani sana kuliona. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ni vitendea kazi. Wakati Wizara inapeleka vitendea kazi katika maeneo yetu, ni muhimu sana kuangalia jiografia za maeneo yetu, maeneo ambayo yana milima mikubwa na mabonde, yapelekewe vitendea kazi kwa uharaka na yaangaliwe kwa jicho la pekee. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mathalani, tunashukuru sana katika Wilaya ya Kakonko tumepata gari dogo jipya upande wa TANESCO, lakini tunaomba pia kupitia nafasi hii tuweze kupata lori kwa sababu ya jiografia tuliyonayo ili wananchi wetu waweze kupata huduma nzuri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine muhimu sana, ni kwamba tutakubaliana kwamba umeme sasa tunao, lakini matumizi ya umeme tuliyonao walio wengi wanatumia umeme kuwasha taa majumbani na kuchaji simu. Sasa kama Taifa tunahitaji kufanya mageuzi ya matumizi ya umeme wetu, tunahitaji kuufanya umeme utumike kiuchumi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ninapenda kupendekeza kwamba Wizara itengeneze timu izunguke katika nchi hii kupitia viongozi na waliopo katika mikoa waangalie watu wanahitaji umeme ambao wanahitaji kuutumia kwa ajili ya kuzalisha ili watu hawa wapewe kipaumbele. Ninatoa mfano, Wilayani Kakonko kuna mwekezaji anafuga ng’ombe kisasa, anafanya uwekezaji mkubwa kabisa pale, lakini ili afikishiwe umeme kwenye eneo lake anatakiwa alipie shilingi 65,000,000. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunahitaji Wizara iliangalie eneo hili kwa jicho la pekee kwa sababu hawa watu wenye viwanda, taasisi za Serikali, shule, viwanda tunahitaji wafikishiwe umeme, hawa ndiyo watumiaji wakubwa. Huyu mtu akifikishiwa umeme kwenye kiwanda chake hiki kwenye biashara yake kama hii ataweza kuajiri watu. Unaona kwenye biashara kama hii ndugu yetu huyu analazimika kukamua ng’ombe kupata maziwa mara moja kwa siku, badala ya kupata lita 12,000 za maziwa analazimika kupata lita 6,000 pekee kumbe angekuwa na umeme angeweza kukamua mara mbili kwa siku. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mchango wangu wa leo unajikita katika eneo hili, Wizara iangalie na itenge fedha, tuzunguke katika nchi hii ili kuona zile taasisi zote ambazo zinahitaji umeme, zifikishiwe umeme. Viwanda vyote vinavyohitaji umeme wafikishiwe umeme ili hawa watumiaji wakubwa waweze kuwa na manufaa makubwa na vilevile manufaa hayo yaweze kushuka katika jamii yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kutoa mchango huo, ninakushukuru sana na ninaunga mkono hoja. (Makofi)