Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

Hon. Hemed Sumry Haidary

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

MHE. HAIDARY H. SUMRY: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote ninapenda kumshukuru Mwenyezi Mungu na kukushukuru wewe kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, niendelee kumshukuru na kumpongeza Dkt. Samia Suluhu Hassan, jemedari ambaye anaongoza mapambano kuhakikisha kwamba nchi hii inaenda kwenye mabadiliko makubwa kwenye Wizara hii ya Kilimo. Ninawapongeza na kuwashukuru Mheshimiwa Waziri wa Kilimo, Naibu wake na watendaji wote wa Wizara hii kwa kazi kubwa na nzuri ambayo wanaifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Jimbo langu la Mpanda Mjini tuna maeneo ambayo yanapaswa kulimwa kwa kilimo cha umwagiliaji, maeneo mawili. Eneo la kwanza ni eneo la Mwamkulu. Ninaishukuru sana Serikali kuna mradi pale wa umwagiliaji unaendelea na tayari umeshafikia 70%. Tunaishukuru sana Serikali, lakini rai yangu katika eneo hili, tunaiomba Serikali ikamilishe huu mradi na kubwa zaidi iweze kujenga mabwawa, kwa sababu tunatamani kupata matokeo. Mradi huu ukikamilika kufika 100% ya ujenzi wa ile miundombinu ya umwagiliaji, kama hatuna bwawa tafsiri yake wakulima watabaki kwenye hatua ile ile ya kulima mara moja kwa mwaka ambayo siyo malengo ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunaiomba sana Wizara ije na mpango wa kujenga mabwawa na wakulima na wananchi wa eneo lile wako tayari na wameupokea vizuri mradi. Tunaamini watazalisha karibu mara mbili au mara tatu ya kile wanachozalisha sasa. Ninamwomba sana Mheshimiwa Waziri, tupia jicho kwenye eneo hilo ili tuweze kupata matokeo ambayo Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, anatarajia kuyapata. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo hili la hii Skimu ya Umwagiliaji ya Kakese kumekuwa na ahadi za Serikali na juzi Mheshimiwa Waziri Mkuu amefanya ziara kwenye jimbo langu. Maombi yangu na ya wananchi wa Jimbo la Mpanda Mjini ilikuwa ni kuomba hii skimu sasa ianze kujengwa. Majibu ya Naibu Waziri wa Kilimo ambaye tulikuwa naye kwenye ziara hiyo alisema kwamba Serikali wakati wowote itatangaza zabuni ya huu mradi ili sasa kazi ya ujenzi wa hii skimu ianze. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimepitia kwenye hotuba yote ya Wizara ya Kilimo nimeona kwamba tuko kwenye upembuzi yakinifu kwa 25%, mambo hayo yalishafanyika tayari na kwa 100% mambo yote yameshakamilika, sasa kwa nini wanaturudisha kwenye upembuzi yakinifu?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninaomba kupitia Wizara, wautangaze mradi huu wa Kakese ili nao uweze kuanza kujengwa. Ukianza kujengwa utaleta ukombozi na utaongeza mapato kwa Serikali, lakini pia utaongeza mapato kwa Halmashauri ya Manispaa ya Mpanda ambayo bajeti yake kwa 50% wanategemea haya mabonde mawili ili kuweza kupata mapato ya ndani ya Halmashauri. Ninamwomba sana Mheshimiwa Waziri azingatie huu mradi atusaidie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huu mradi wa Kakese ambao bwawa lake litajengwa kwenye eneo la Dilif utahudumia mabonde mawili, utahudumia Jimbo langu la Mpanda Mjini na Jimbo la pili la Mheshimiwa Lupembe kwenye eneo la Nsimbo. Kwa hiyo, unaona ni muhimu kiasi gani bwawa na mradi huu uanze kujengwa ili kuwasaidia wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuongelea eneo la umwagiliaji, niende kwenye soko. Ahadi ya Ilani ya CCM ya mwaka 2025 - 2030 ni kujenga Soko kubwa la Kimataifa la Mazao kwenye Jimbo langu la Mpanda Mjini. Ninaiomba Serikali, hiyo pia ni ahadi ya Mheshimiwa Rais alipokuja kwenye kampeni, mambo mahsusi aliyoongelea ni pamoja na hili soko la mazao kwenye Jimbo langu la Mpanda Mjini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamwomba sana Mheshimiwa Waziri, tunafahamu ndiyo umeingia kwenye Wizara, inawezekana mambo hayajakaa sawasawa. Ninakuomba katika bajeti ijayo, sijaliona kwenye bajeti hii, ninakuomba katika bajeti ijayo, basi watutengee ili na sisi tuweze kupata soko. Tuna soko dogo pale…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. HAIDARY H. SUMRY: Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna soko dogo pale ambalo linafanya vizuri, lakini watu wanapigwa na jua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana kwa kupata nafasi hii. Ninaunga mkono hoja na Mungu awabariki sana Wizara ya Kilimo. (Makofi)