Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

Hon. Patali Shida Patali

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

MHE. PATALI S. PATALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nishukuru kwa nafasi hii uliyonipa. Mchango wangu kimsingi ninaomba ujikite kwenye maeneo, hasa eneo kubwa la mbolea. Ninaomba nifikishe salamu za Wanambeya Vijijini kwa kuwasemea maeneo mawili kwa haraka. Kwanza ni kuhusu pareto. Mbeya Vijijini ni moja ya wilaya ambayo inaongoza kwa kilimo cha pareto nchini, kwa mujibu wa taarifa za Bodi ya Pareto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatambua kuna jitihada mbalimbali zinazofanywa na Serikali kwa ajili ya kuboresha biashara ya zao hili. Hivi karibuni na kwa kupitia Taarifa iliyowasilishwa, kuna mpango wa ujenzi wa haya makaushio 150 na sisi Mbeya vijijini tunayo 40. Tuiombe Serikali ituharakishie ujenzi huu wa haya makaushio kwa ajili ya kuboresha hili zao la pareto Mbeya Vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie bei; moja ya changamoto kubwa kwenye zao hili la pareto ni kuwa na vishoka wengi ambao wanadidimiza jitihada za makusudi za wakulima. Serikali kupitia Wizara ya Kilimo, Mheshimiwa Waziri, kaka yangu Chongolo wawaangazie macho hawa vishoka ambao wanaingilia kati kwenye hizi bei za hili zao la pareto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nizungumzie mazao. Jimbo la Mbeya Vijijini tunazalisha zaidi ya tani laki sita za mazao ya chakula lakini mahitaji yetu ni takribani tani laki moja na tisini hadi laki mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na yale ambayo Waheshimiwa Wabunge wengi wamechangia katika Bunge hili, tusipoliangalia vyema hili suala la masoko nchini, tunaenda kuzalisha mazao mengi na tukakosa masoko kwa kwenda kuyauza. Cha kwanza, ninaomba nisisitize kuboresha masoko ya ndani, ikiwa ni pamoja na kujenga masoko kwenye kila wilaya ambazo zinaongoza kwa uzalishaji wa mazao ya chakula. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, unaweza ukawaza hizi tani 400,000 sisi Mbeya Vijijini ambazo tunazalisha ziada ya chakula dhidi ya mahitaji yetu tutazipeleka wapi endapo hatutaboresha au kuchukua hatua za makusudi kujenga masoko?

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili ambalo ninatamani kujikita ni suala la mbolea; na hapa ninaomba nichangie haraka haraka kwa sababu ya muda mfupi. Nchi yetu hii inakadiriwa ifikapo mwaka 2030 tutakuwa na takribani ya wastani ya watu wasiopungua milioni 77.55. Watu hawa wote wanahitaji ardhi kwa ajili ya kilimo ili kuelekea ule uchumi wa dola trilioni moja ifikapo mwaka 2050 kama Dira yetu ya Taifa inavyoeleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kilimo chetu kiwe na tija ni lazima tuangalie uwezekano na kuchukua jitihada za makusudi katika kuimarisha upatikanaji wa mbolea nchini. Hali ilivyo sasa, tunapata mbolea ya ruzuku na hapa ninamshukuru sana Mheshimiwa Rais; lakini bado kuna changamoto ya kuchelewesha mbolea na pia kuingiliwa na walanguzi wanaoficha mbolea. Wakati mwingine zinaadimika sokoni na kuwalazimisha wakulima wazitafute kwa njia nyingine. Ni kwa sababu mkulima anakosa option, kwa hiyo inabidi awatafute walanguzi. Niiombe Wizara ya Kilimo kupitia TFRA, ninatambua wanafanya kazi nzuri sana, lakini waboreshe eneo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, ili kutatua hii adha ni kuhakikisha viwanda vyetu vya ndani tunavipa nguvu katika maana ya uwekezaji. Waheshimiwa Wabunge wengi wamesema tuna takribani viwanda 48 vya uzalishaji wa mbolea, lakini viwanda viwili tu; INTRACOM na Minjingu ndivyo at least vinazalisha, vinabeba viwanda vingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe kwa kumalizia, tutafute uwezekano wa kuwekeza kwenye viwanda hivi ili kuongeza tija ya upatikanaji wa mbolea na kuwarahisishia wakulima ili kupata mbolea na kilimo ambacho wanalima kiwe na tija na cha uhakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, ninaomba kuunga mkono hoja. (Makofi)