Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Moshi Mjini
Contributions
nil
Answers
nil
Commettees
1
Ministries
nil
MHE. MORRIS J. MAKOI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Ninaomba nikushukuru wewe binafsi, lakini kwa vile ninaongea hapa kwa mara ya kwanza kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Moshi Vijijini, ninaomba nichukue nafasi hii kumshukuru sana Rais wetu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan. Nimshukuru pia Makamu wa Rais, lakini na Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba kwa kazi kubwa wanayofanya kuhakikisha nchi yetu inasonga mbele. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba pia nichukue nafasi hii kumshukuru Waziri wa Kilimo, Naibu Waziri, Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo na timu yao yote, bila kumsahau Mkurugenzi Mkuu wa COPRA na Mkurugenzi wa Wizara ya Kilimo wa Mazao Mchanganyiko. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Jimbo langu ninalotoka la Moshi Vijijini na Vunjo, kilimo kikubwa ambacho kimesaidia wananchi miaka mingi ni kilimo cha kahawa, lakini katika miaka ya hivi karibuni kilimo kile ni kama kimepewa kisogo na ninaona hata Wizara ya Kilimo na wenyewe kama wamekaa pembeni kabisa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijaendelea ninaomba kabisa kwa ruhusa yako nimwombe Waziri wa Kilimo na timu yake ya Wizara watusaidie Wilaya ya Moshi, Jimbo la Moshi Vijijini na Vunjo, waweze kurejea tena kwenye kilimo cha kahawa kwa sababu ndiyo njia pekee ya kujipatia riziki na kipato kwa wananchi wa Majimbo hayo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba sasa pamoja na kwamba Wizara imetusaidia hivi karibuni kupata miche ya kahawa, ninawaomba waendelee kuongeza nguvu kwa sababu wananchi wale sasa wamekubali kurudi shambani ili wazalishe upya kahawa baada ya kugundua kwamba bei imekuwa kubwa na wamegundua kwamba Mheshimiwa Rais Samia ana nia ya dhati kabisa kuwezesha wakulima wote ambao wana nia ya kuzalisha mazao ya biashara hususan zao la kahawa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kama unavyojua kule kwetu Kilimanjaro, Chama Kikuu cha KNCU ndicho ambacho kilichochea vyama vingi vya msingi na wakulima kujiondoa kwenye kulima kahawa kutokana na madeni mengi ambayo chama kile kimeshindwa kuwalipa vyama vya msingi.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kwamba nimepata hakikisho la fedha zinazodaiwa kulipwa, lakini ninataka niweke kumbukumbu sawa kwenye Bunge hili kwamba, Chama Kikuu cha Ushirika KNCU wanadaiwa na vyama 40 kutoka Jimbo la Moshi Vijijini na Jimbo la Vunjo jumla ya shilingi milioni 800 na kidogo. Uhakiki uliofanyika karibuni unaonesha kwamba hizo fedha ni za msimu wa 2010/2011- 2012/2013 mpaka karibu 2016 zilikuwa hazijalipwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, unaweza kuona jinsi gani hali hiyo imechochea umaskini, kukata tamaa kwa wakulima na hali nyingine ambayo kwa kweli kumshawishi mtu arudi shambani alime kahawa imekuwa ni ngumu, lakini wananchi wale sasa wapo tayari baada ya kupata hakikisho kwamba fedha zile zitalipwa kupitia Mkurugenzi wa TCB. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba niongelee ushirika: ushirika nayo imekuwa ni changamoto kubwa sana katika Wilaya ya Moshi; majimbo mawili Vunjo na Moshi vijijini.
Mheshimiwa Naibu Spika, ushirika wameshindwa kabisa kurekebisha sheria ambayo itawezesha wale ambao wachache wanaotumia fedha za wananchi vibaya waweze kukumbwa na mkono wa sheria. Kwa hiyo, kule Moshi SACCOS nyingi ambazo zilikuwa zimeanzishwa na wakulima ama zimefilisika, ama zimefilisiwa na wale viongozi na hakuna hatua zozote ambazo zimechukuliwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ninaomba Mheshimiwa Waziri, atakapokuja kufanya majumuisho, aniambie na awaambie wananchi wa Moshi Vijijini kupitia Bunge hili ni hatua gani watachukuliwa wale ambao wamekula fedha zao kutoka kwenye baadhi ya Vyama vya Msingi na SACCOS ambazo zilikuwepo na ambazo zilikuwa zimeenda vizuri na zilikuwa zinatoa tija kubwa sana kwa wale wananchi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, niombe nizungumzie habari ya upatikanaji wa mbolea. Ninaomba nichukue nafasi hii kumshukuru sana Mkurugenzi wa… eeh...
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Makoi.
MHE. MORRIS J. MAKOI: Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru. (Makofi)