Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

Hon. Juma Ramadhani Mustafa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Igalula

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

MHE. JUMA M. KAWAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii ili nichangie bajeti ya Wizara ya Kilimo 2026/2027. Kwanza kabisa ninaanza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, ambaye amejaalia mimi na Wabunge wote jioni hii tumekutana hapa Bungeni. Pili, shukrani zangu za kipekee ninazipeleka kwa Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anazoendelea kufanya kupitia Wizara hii ya Kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba nijielekeze moja kwa moja kwenye mchango, kwenye Wizara hii ya Kilimo. Kama jinsi tunavyoona Wizara hii ya Kilimo imeajiri zaidi ya watu 65% Watanzania wa nchi hii. Hata hivyo, inachangia kwenye pato la Taifa zaidi ya 27%, inachangia kwenye Mfuko Mkuu wa pato la Taifa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na faida hizi bado kuna changamoto mbalimbali ambazo zinatakiwa zichukuliwe hatua za haraka kwenye Wizara hii ya Kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata tukiangalia kwenye Ripoti ya Wizara ya Mwaka 2026 inaonesha ongezeko la mazao yanakuwa kwa asilimia 4.5, hii inatuambia nini? Mazao yanaongezeka lakini bado ongezeko la watu haliendani na mahitaji ya chakula nchini. Hapa tunaona kwamba, bado Wizara haijawekeza kwa wakulima wadogo wadogo kwa sababu ndio uti wa mgongo wa sekta hii ya kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ninaishauri Wizara ijielekeze kwenda kuwekeza tija zaidi kwa wakulima wadogo wadogo hapa nchini, hasa hasa kuweza kuangalia kwenye masuala ya pembejeo, mbegu zenye ruzuku na kuwatafutia masoko wakulima wadogo wadogo, ndiyo watakuwa wameweka tija kubwa kwenye sekta ya kilimo nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na mafanikio haya ya Wizara, lakini ndani ya Jimbo langu la Igalula bado kuna changamoto mbalimbali ambazo zinawakabili wakulima wangu. Ucheleweshaji wa pembejeo kufika kwa wakati kwa wakulima hasa vijijini bado inaonekana ni changamoto kubwa sana, licha ya wakulima kulima kwa bidi, lakini bado pembejeo zinachelewa kufika. Zinafika katikati ya msimu wa kilimo na wakati mwingine zinafika zinakuta wakulima kabisa wamemaliza kulima kilimo hiki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninashauri nini hapa? Serikali ihakikishe tunapata pembejeo kwa wakati ili wakulima waweze kulima vizuri na tuweze kupata tija kwenye sekta hii ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tukiangalia kwenye Ilani ya Chama Cha Mapinduzi, tunaona ni jinsi gani sisi kwenye Mkoa wetu wa Tabora ilani imetuelekeza vizuri. Katika miaka hii mitano, ilani imetuelekeza kwamba inatakiwa tukaongeze uzalishaji wa mbegu kutoka tani 80,000 mpaka tani 19,000; inatakiwa tukaongeze uzalishaji wa mazao ya biashara kutoka tani 200,000 mpaka tani 300,000 lakini na mazao ya chakula kutoka tani 200,000 mpaka tani 500,000. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, haya yote hatuwezi kuyapata bila kuirejea ilani ambayo imetuahidi kwamba Mkoa wa Tabora inatakiwa tupate kiwanda cha mbolea ndani ya miaka hii mitano ili tuweze kuyashuhudia haya. Watu walioandaa ilani wameyaona malengo haya ya miaka mitano kwenye sekta ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaiomba sana Wizara iharakishe mchakato wa kupata Kiwanda cha Mbolea katika Mkoa wa Tabora. Kama watakuwa wanakutana na changamoto zozote za kuhusu maeneo, sisi Wabunge tupo, tutakaa na Viongozi wetu wa Mkoa, kuweza kutafuta maeneo ambayo tutaweza kujenga Kiwanda chetu cha Mbolea Mkoa wa Tabora. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la miundombinu ya skimu ya umwagiliziaji. Takwimu zinaonesha kwamba ni chini ya 10% tu, ardhi ambayo inafaa kuwekezwa kwenye umwagiliziaji ndiyo ambayo imetumika nchini. Ninaiomba sana Wizara iendelee kutafuta fedha kwa kushirikiana na Wizara ya Fedha, tuhakikishe skimu za umwagiliziaji tunakwenda kuzikwamua nchi nzima na hii ndiyo italeta maendeleo ya kweli kwenye sekta ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spia, kwa sababu Ilani ya Chama Cha Mapinduzi, sisi Mkoa wa Tabora inatuelekeza kwamba ndani ya miaka hii mitano inatakiwa tukazalishe kutoka ekari 37 za sasa mpaka ekari 150,000. Bila ya kwenda kuzirejea hizi skimu za umwagiliziaji sisi hatutaweza kufanya vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaiomba Wizara ya Kilimo ihakikishe kwamba Skimu ya Umwagiliziaji ya Bwawa la Goweko inakwenda kujengwa ndani ya miaka hii mitano, lakini Skimu ya Umwagiliaji ya Kata ya Miswaki inakwenda kujengwa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana.
MHE. JUMA M. KAWAMBA: …Skimu ya Umwagiliaji pia ya Kata ya Loya na yenyewe inakwenda kujengwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la mazao...

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa muda umekwisha, malizia sentensi ya mwisho.

MHE. JUMA M. KAWAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, ninashukuru sana kwa kunipa nafasi hii. Ninapenda kuishauri Wizara kama tunataka maendeleo ya kweli na mageuzi ya kweli kwenye sekta ya kilimo, sera zetu ziende zikawalenge wakulima wadogo wadogo kwa ajili ya kwenda kuleta mapinduzi makubwa na halisi ya kiuchumi nchini.

NAIBU SPIKA: Ahsante sana.

MHE. JUMA M. KAWAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, ninashukuru sana, ninaunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. (Makofi)