Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Mbozi
Contributions
nil
Answers
nil
Commettees
1
Ministries
nil
MHE. ONESMO M. MNKONDYA: Mheshimiwa Naibu Spika, ninashukuru sana kwa nafasi ambayo umenipa ili niweze kuzungumza na Wizara yetu ya Kilimo, ambayo ina Waziri bora kabisa na Naibu Waziri. Ninawapongeza kwa kazi kubwa ambayo wanaifanya kwenye Wizara yetu ya Kilimo, ninaweza nikasema ndiyo Wizara pekee ambayo imeajiri watu wengi kwenye Taifa letu.
Mheshimiwa Naibu Spika, nikizungumza kwa niaba ya Wanambozi ambao wamenituma na leo nifikishe ujumbe huu kwenye Wizara yangu muhimu kabisa hii, kwa Jimbo langu la Mbozi peke yake, waliojiajiri kwenye kilimo ni 80%. Maana yake nini, ni kwamba kilimo ndiyo ajira kwa Jimbo langu la Mbozi, tunategemea kilimo kwa asilimia hizo zote ambazo nimezisema.
Mheshimiwa Naibu Spika, wao walichoniagiza kwenu Mawaziri wangu, mwaka jana walipata shida ya changamoto ya mbolea, wamepata changamoto ya mbegu, wamepata changamoto ya madawa, lakini asilimia kubwa wamepata changamoto ya mbolea aina ya DAP. Sasa Mheshimiwa Waziri, tunapomaliza msimu huu wa kilimo, tunaanza msimu mpya mwingine. Tunaelekea kumaliza msimu lakini tunaunganisha msimu kwa jimbo langu, msimu wote tunalima sisi.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa mwaka jana changamoto ile kidogo imeleta tafaruku kwa jimbo langu. Wananchi wamelalamika kama nilivyowahi kuuliza swali hapa, wameingia hasara na hakuna mtu wa kuwafidia, ni nani wa kwenda kuwafidia na kwenda kuwaomba kwa msimu huu unaoanza?
Mheshimiwa Naibu Spika, tunahitaji mbolea iwahi kwa wakati, tunahitaji mbolea ya kupandia iwahi kwa wakati, tunahitaji tena mbolea ambayo ni bora, hakuna mbolea feki. Tunahitaji madawa bora, tunahitaji mbegu bora ili tumlinde mkulima. Ili tumlinde nani, mkulima. Bila kufanya hivyo tunahatarisha uchumi wa Wanambozi, uchumi wa Watanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, wakati huo huo mbolea zinapokuja tumeruhusu watu kuuza mbolea feki, hatumlindi mkulima, unajiuliza TFRA wako wapi, unajiuliza wako wapi walinzi hawa, wasimamizi wa bei, lakini wasimamizi wa ubora wa mbolea wako wapi? Hawapo! Wabunge tunaanza kuhangaika madukani siyo sawa, watu wa TOSCI wako wapi kwenye mbegu, watu wa TIFA wako wapi kwenye madawa hawasimamii? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ninavyozungumza mbolea Jimbo la Mbozi inauzwa shilingi 100,000 hadi shilingi 90,000, hivi ndivyo bei ya mbolea ya ruzuku ambayo Rais Samia ametupatia ndiyo bei hiyo. Kwa nini wasitoke tamko marufuku kuuza mbolea kwa bei ya juu, twende tuuze mbolea kwa bei elekezi na bei elekezi ipo wazi. Niombe tumlinde mkulima, tuwalinde wakulima wetu, tuwalinde baba zetu, tuwalinde vijana wetu ambao wanakimbilia kujiajiri wanapokuta mbolea shilingi 100,000 watajiajirije? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na muda ninaomba nishauri lifuatalo: Mwaka jana kwenye huu msimu kampuni ya TFC imekuwa mkombozi mkubwa sana, kampuni hii ndiyo kampuni pekee imetuagizia mbolea ya DAP tani 50,000 pekee yake, kampuni zote zilinyamaza. Ninaomba wakakae na kampuni hizi nyingine pia, wakazungumze kilimo, wakazungumze biashara wakazungumze maendeleo ya Watanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, wakati huohuo hii kampuni, ninaomba nishauri kwa Mheshimiwa Waziri, waendelee kuisimamia na kama kuna ruzuku waliyosambaza mbolea hawajalipwa, walipwe waagize mbolea mapema kwa ajili ya wakulima wa Mbozi na Watanzania, lakini niombe ikiwezekana wawa-support, wawape mtaji wawawezeshe, kwa sababu wana uwezo wa kufanya kazi ya kutuletea mbolea bora kabisa.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine, TFC wanapoagiza mbolea tunahitaji mbolea iwahi, wawahi kuagiza na wakulima wawahi kuipata mbolea. Kuna mlolongo mkubwa kwenye uagizaji wa mbolea, taratibu za manunuzi na mlolongo wa manunuzi kwenye Taifa letu yanaeleweka, watu hawa wanaponunua mbolea wananunua kwenye Mataifa mengine....
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa ahsante sana.
MHE. ONESMO M. MNKONDYA: Mheshimiwa Naibu Spika, wananunua kwa wafanyabiashara wakubwa, ninaomba nimalizie sekunde.
NAIBU SPIKA: Malizia sentensi yako ya mwisho.
MHE. ONESMO M. MNKONDYA: Mheshimiwa Naibu Spika, wanaagiza kwa wafanyabiashara wakubwa, wale wafanyabiashara wakubwa hawazijui taratibu zetu, ninachokiomba wawape fedha wawaondolee mlolongo mrefu wa kuagiza mbolea, habari za NeST aachane nazo kwenye suala la mbolea tu ikiwezekana wakaagize mbolea kwa faida ya Watanzania kwa faida ya Wanambozi ili tupate mbolea kwa wakati. Wakati wanasubirisubiri mbolea huwa inapanda.
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mbunge, ahsante sana.
MHE. ONESMO M. MNKONDYA: Mheshimiwa Naibu Spika, ninashukuru sana na ninaunga mkono hoja lakini dakika ni chache. (Makofi)