Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

Hon. Josephine Joseph Kapoma

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

MHE. JOSEPHINE J. KAPOMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa nafasi hii niliyoipata ili na mimi niweze kuchangia hotuba hii ya Wizara ya Kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee ninapenda kumpongeza kaka yangu Waziri wa Kilimo, Mheshimiwa Daniel Chongolo pamoja na timu yake Naibu Waziri, Katibu Mkuu kwa hotuba kubwa na nzuri ambayo imelenga na kuwapa matumaini makubwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa ajili ya maslahi ya muda, ninaomba nijielekeze moja kwa moja. Mosi, nitaelekea kwenye zao la tumbaku. Kwa nini zao la tumbaku, zao la tumbaku mimi nikiwa kama mwakilishi wa watu wa Morogoro hili zao ni katika mazao ya kimkakati ambayo watu wa Morogoro linatuingizia kipato kikubwa kwa sababu viwanda vya kuchakata tumbaku viko Mkoani Morogoro. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, zao la tumbaku kwa takwimu tu, mwaka wa fedha 2020/2021 tulipata jumla ya mapato ya USD milioni 392, lakini kufika mwaka wa fedha 2024/2025 tumepata mapato ya zaidi ya USD bilioni 1.2, ni zaidi ya 187% ya ongezeko la pato.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sisi watu wa Morogoro, Kiwanda cha Mkwawa Tobacco mwezi Aprili, 2024 kufika Disemba, 2025 tumefanikiwa kupata zaidi ya ushuru wa Halmashauri levy bilioni 2.7, lakini viwanda hivi tu kwa Morogoro toka Rais alivyokuja na mapinduzi ya tumbaku, Morogoro viwanda hivi vimeweza kuajiri ajira za muda mrefu zaidi ya wafanyakazi 1,000 na ajira za msimu zaidi ya 5,000.

Mheshimiwa Naibu Spika, pongezi hizi huwezi kuziongelea bila kumtaja Mkurugenzi wa Bodi ya Tumbaku Ndugu Stanley. Kazi kubwa aliyoifanya katika mapinduzi ya tumbaku watu wote tunaelewa. Pia, sisi kama watu wa tumbaku pongezi kubwa tunazipeleka na wachangiaji wengi wamelalamika kwamba mbolea zinachelewa, lakini wakulima wa tumbaku na wadau wa tumbaku kwa kweli kwenye suala la mbolea hilo hatuna malalamilko kwa sababu mbolea tumepata kwa wakati. Kwa hiyo pongezi nyingi sana ziende kwa kaka yangu Mshote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninajielekeza sasa kuishauri Serikali. Wachangiaji wengi waliopita wamelalamika kuhusu suala zima la bei. Kweli mwaka jana wastani tuliuza kwa dola 2.3, lakini mwaka huu tunaenda kuuza kwa dola 1.9. Sasa ninaishauri Serikali, soko la tumbaku linakuwa-controlled, ni soko la kidunia hatuna control na bei ya tumbaku. Sasa tufanye nini, nilikuwa ninaishauri Serikali kwa sababu soko la tumbaku liko-controlled, ni wakati sasa sisi kama Tanzania tukaangalia masoko mengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano Tanzania hatufanyi biashara na China, lakini tunao Mabalozi kama Balozi ambayo iko China. Huu ni wakati sahihi wa kuona ni vipi tunaweza tukatanua wigo wa soko na kwa kifupi China kufanya biashara na sisi, kitu ambacho tunatakiwa kukifanya ni mikataba ya nchi kwa nchi ambayo ni bilateral agreement.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukitanua wigo wa soko na kuongeza watu wengine Wallah nakuapia, hili suala la bei ya tumbaku halitakuwa kero kwa sababu tutakuwa na wigo mpana sana wa soko. Kwa sababu sasa hivi tuna wanunuzi wachache ambao wanaweza wakapanga bei wanayoitaka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninapenda kuishauri Wizara kwamba shida ya bei ya tumbaku kidunia pia inasababishwa na cost of production. Hata hivyo, Tanzania tuna uwezo wa kutengeneza viwanda vyetu, ambapo tutatengeneza vifungashio kama magunia na kamba, tunayo katani na hizi malighafi ambazo hivi vitu tunaweza tukavitengeneza katika nchi yetu. Kwa sababu bei ya tumbaku inaathirika kikubwa sana na cost of production.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tukipata nafasi ya kuweka mikakati katika kujenga viwanda vya mbolea, viwanda vya magunia na nyuzi zikapatikana hapa, tunaenda kupunguza cost of production, hivyo hata soko la dunia likiyumba kwenye bei ya tumbaku, sisi bado tutakuwa tumeuza tumbaku yetu kwa faida na soko likipanda maana yake tutauza kwa supper abnormal profit. Kwa hiyo ninatoa ushauri huu katika hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, soko la tumbaku sasa hivi tumekuwa na shida kubwa hasa katika mikutano ya kidunia, tumekuwa tunapigwa vita sana katika uzalishaji wa tumbaku.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mbunge, ahsante sana.

MHE. JOSEPHINE J. KAPOMA: Mheshimiwa Naibu Spika, dakika moja ninamalizia.

NAIBU SPIKA: Unga mkono hoja, muda wako umekwisha.

MHE. JOSEPHINE J. KAPOMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba kuunga mkono hoja. (Makofi)