Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Madini kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

Hon. Dotto Jasson Bahemu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngara

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Madini kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

MHE. DOTTO J. BAHEMU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Nishati na Madini, ninaomba niungane na Mwenyekiti wetu, kuendelea kumpongeza Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi kama kijana nimejua kwamba, vijana wote wanafarijika pale ambapo vijana wenzetu wanapata nafasi, wanazitumia vizuri na wanazitendea haki. Mheshimiwa Waziri Anthony Mavunde anaitendea haki sana nafasi yake, ambayo Mheshimiwa Rais amemwamini. Tunampongeza, sisi vijana wenzake na anazidi kutu-inspire katika maeneo mengine na tunamtakia kila la heri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo tunajua kwamba, hakuna kijiji kisicho na wazee, kaka yetu pia, Naibu Waziri, tunampongeza sana kwa msaada mkubwa anaoutoa kwa Mheshimiwa Waziri pamoja na Menejimenti nzima ya Wizara. Baada ya pongezi hizo, sisi katika Jimbo letu la Ngara tuna Mradi wa Kabanga Nickel; kama ambavyo maeneo mengine yana dhahabu, mengine yana almasi, sisi katika Jimbo la Ngara na Wilaya ya Ngara Mwenyezi Mungu ametujalia tumepata nickel, lakini imekuwa ni story ya muda mrefu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa takwimu ama kumbukumbu inaonesha kwamba, utafiti wa kwanza ulianza kufanyika mwaka 1976 pale Kabanga Nickel. Hii ni kwa mujibu wa Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano wakati wakisaini mkataba na kampuni ambayo inatakiwa kuendesha huu mradi, alisema yeye mwenyewe kwamba, utafiti wa kwanza ulianza mwaka 1976.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kipindi chote hicho ambacho sisi watu wa Ngara tumekuwa tunasubiri kwa muda mrefu kuweza kunufaika na ile rasilimali ambayo Mwenyezi Mungu ametujaalia, mpaka leo hakuna namna ambavyo tunaweza tukasema kwamba, tupo tumenufaika au tunaona dalili za kunufaika. Kwa bahati mbaya ni kwamba, hata jitihada zote ambazo zinafanywa na Mheshimiwa Waziri na Mheshimiwa Rais kwa sasa hivi, mimi Bahati nzuri nimekuwa ninazungumza na Mheshimiwa Waziri mara kwa mara, ameniambia jinsi ukweli ulivyo na ninauona mwanga.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa siku ya leo ninamwomba Mheshimiwa Waziri, kwa mdomo wake, aongee na watu wa Ngara atuambie Mradi wa Kabanga Nickel ni lini unaanza? Kauli moja tu! Atuambie Mradi wa Kabanga Nickel ni lini unaanza? Hilo tu litakuwa limetosha; sisi hatuna kitu kingine ambacho tunataka kusikia kwa siku ya leo kutoka kwa Waziri zaidi ya kwamba, Mradi wa Kabanga Nickel unaanza lini? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu, siyo kwamba hatuamini, tunaamini kwamba ni kitu kinakuja kutokea, lakini kwa bahati mbaya sisi watu wa Ngara tulishang’atwa na nyoka huko nyuma, sasa hivi tukiona majani tunakuwa na wasiwasi. Kuanzia mwaka 1976 mpaka leo ambavyo tunaendelea, tumekuwa tunaona zinakuja kampuni; inakuja kampuni hii inatoka, inakuja kampuni nyingine inatoka, inakuja kampuni inatoka.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa sisi uelewa wetu, wananchi wa kawaida, ni tunajua kwamba, tayari pale shughuli zinaendelea. Hayo mambo ya kitaalam wanayajua wao kwamba, sijui ni utafiti! Sijui ni nini, lakini sisi wananchi wa kawaida ambao tumezunguka eneo lile, ambao tunategemea tuwe tunanufaika na eneo lile, tunajua kwamba shughuli zinaendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mwaka 2021 tunakumbuka ndipo mkataba ulisainiwa, kwa ajili ya kuanza huu mradi rasmi, miaka mitano iliyopita. Ninakumbuka kwenye ile hafla ya kusaini ule mkataba iliyofanyika Bukoba, mgeni rasmi alikuwa Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano na miongoni mwa watu ambao walitufanya sisi watu wa Ngara tukapata faraja kwamba sasa tunaenda kunufaika ni Mheshimiwa Profesa Kabudi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Profesa Kabudi wakati anaelezea manufaa ya ule mradi, item Namba 7 aliyoitaja, ninaomba niinukuu alisema: “Miongoni mwa faida za huo mradi ni kuendeleza biashara, uchumi na maisha bora kwa Wilaya ya Ngara na Wilaya ya Kahama na wananchi wake kwa ujumla”. Akamalizia kusema, “Ngara Oyee!”, akamalizia kusema “Kahama Oyee!”. Sasa, leo ni miaka mitano imepita tangu kauli zile za kututia matumaini za Mheshimiwa Profesa Kabudi, ambazo alizitoa jinsi ambavyo tunaenda kunufaika na Tembo Nickel, lakini mpaka sasa hivi watu wa Ngara wanaamini kwamba, ni story zinaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kwa sababu, tumepita katika vipindi mbalimbali vya kuambiwa hiki kitaenda hivi, hiki kitaenda vile, mpaka leo, hata angekuja nani leo akatuambia, mimi ninajua kwa sababu, pengine angalau nimepata nafasi ya kuwa kwenye Kamati ya Nishati na Madini, ninajua kwamba, kuna kitu kinakuja, lakini watu wa Ngara wanaamini ni story kwa sababu, story za hivyo wameambiwa kwa miaka mingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa, leo inawezekana ikawa ni siku ambayo wananchi wa Ngara watafurahi sana watakapomsikia Waziri. Kwa kipindi chote ambacho kimepita Mheshimiwa Waziri, tunaomba basi leo awafurahishe watu wa Ngara, awape matumaini, awaambie Mradi wa Kabanga Nickel utaanza lini? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna vijana wengi wa kule Ngara wameomba kazi katika huu mradi ambao wanaamini kwamba, unakwenda kuanza, sasa hata akipata kazi sehemu nyingine anaogopa kwenda kwa sababu, anategemea hapa kwa hiyo, kuna vitu vingi sana vime-stuck. Kuna watu wengine wameanza kutengeneza biashara zao, wameanza kubuni mawazo ya biashara, lakini kila siku kitakuja hiki, kesho kitakuja kitu kingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu ilitokea huko nyuma tukawa tunaamini kwamba hiki kitu kinaenda kutokea na kwa sababu hakijawahi kutokea, Mheshimiwa tunaomba atushangaze watu wa Ngara, basi tunaomba itokee. Sisi Ngara mambo ambayo huwa tunayaomba kwa Serikali, ni mengi. Wakati huu ambao tumekuja tumesema vitu vingine, wakitupa vitaenda kupunguza shida nyingine hata hawatapigiwa kelele.

Mheshimiwa Naibu Spika, watakapotupa Tembo Nickel kuna mambo mengine automatically yataanza kujipeleka. Sisi watu wa Ngara hatutalalamika kwa sababu, tunaamini tutapata ajira, tutapata uchumi kama ambao alisema Mheshimiwa Profesa Kabudi, lakini kama itaendelea kuwa story, kama miaka yote, sisi watu wa Ngara tutaendelea kuwa disappointed. Tunaomba Mheshimiwa Waziri, mimi ninamjua vizuri sana, ninajua jinsi gani ambavyo yuko committed na mara kwa mara amekuwa akiniambia nenda kaa vizuri na Tembo Nickel, kitu kinaenda kuanza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba, watu wa Ngara nimewaambia vitu vingi sana, vingine vinatokea vingine vitakuja kutokea, lakini vingine havitatokea. Hili wakilisikia kutoka mdomoni mwa Waziri leo, atapokuwa anahitimisha hapa, atuambie Tembo Nickel inaanza lini na Kabanga Nickel inaanza lini?

Mheshimiwa Naibu Spika, watu wa Ngara watamshukuru na sisi tunamwombea kila la heri, tunamtakia utekelezaji mwema wa bajeti yake, ili kuwa na mengi, lakini ninaomba nisichanganye hili la Tembo Nickel na na kitu kingine. Ninaomba leo libaki hilo hilo la Tembo Nickel peke yake, ili kama ananijibu, anijibu hilo peke yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, ninaunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)