Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Sex
Female
Party
CCM
Constituent
Special Seats
Contributions
nil
Answers
nil
Commettees
1
Ministries
nil
MHE. JOSEPHINE J. KAPOMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kupata nafasi ya kusimama siku ya leo kuchangia katika hotuba hii ya Wizara ya Madini.
Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee kabisa ninapenda kumpa pongezi kaka yangu Mavunde na timu yake yote, Naibu Waziri, Katibu kwa kazi kubwa ambayo wameifanya. Tunapoongelea madini maana yake tunaongelea uchumi wa Tanzania na tunaongelea ukuaji wa uchumi wa Tanzania. Kwa hiyo, kaka yangu Mavunde, kiatu alichokivaa kimemtosha sawasawa, akaze mwendo na ashikilie hapo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee ninafarijika sana. Nikiangalia jinsi tulikotoka na tunapoelekea. Ukiangalia takwimu zinaonesha mwaka wa fedha 2023/2024 tilipata maduhuli zaidi ya bilioni 750 na kadhaa, lakini mwaka unaofuata tulipata zaidi ya trilioni moja na mwaka 2026 hatujamaliza mwaka wa fedha, ndani ya miezi tisa tumeshazidi zaidi ya 114% katika ukusanyaji wa maduhuli.
Mheshimiwa Naibu Spika, hii inamaanisha nini? Hii ina maana kwamba mikakati ambayo Waziri amejiwekea kama Wizara ya Madini, inaenda sawasawa siyo mikakati ya kwenye makaratasi. Kwa hiyo, ninaomba nimpongeze kwa sababu sisi ni Tomaso, tunataka kitu ambacho Waziri anakizungumza tukione. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, leo nitajikita moja kwa moja katika madini ambayo mchangiaji dada yangu Mheshimiwa Esther ametoka kuyasemea. Nimetoka Mkoa wa Morogoro, Mkoa wa Morogoro kila mtu anafahamu jinsi tulivyobahatika kuwa na madini ya kila aina, lakini sasa shida inayokuja ni kwamba haya madini hayajapewa thamani ambayo yanatakiwa kupewa.
Mheshimiwa Naibu Spika, Morogoro tu pale tuna madini kama limestone, tuna marble, tuna golden shine, amethyst, sand stone, kitenge, feldspar, just name it! Ninaweza nikataja mpaka asubuhi, lakini ukiangalia kwa takwimu mwaka 2023 mpaka mwaka 2025 tumefanikiwa kukusanya maduhuli ambayo ni kama bilioni 16 siyo kweli! Hii ni kwa sababu ninaona kama nguvu kubwa tumeiweka kwenye baadhi ya madini ambayo ni gold na Tanzanite.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ni wakati wa kuyapa haya madini thamani na nini sasa kifanyike? Mimi binafsi ni mchimbaji mdogo na kumekuwa kuna shida ambayo wachimbaji wengi wa madini haya ambayo either siyo ya vito wanapitia, mojawapo ni kukosa masoko. Mfano, ninachukulia sasa hivi mtu anachimba sandstone, leo hii ukichimba sandstone ukimpelekea Mchina anakwambia shilingi laki tatu kwa kilo, kesho ukipeleka anakwambia shilingi laki tatu kwa kilo, baada ya wiki ukimpelekea anakwambia hii jiwe leo leta mbaya sana, mimi nitanunua kwa shilingi elfu nane, kwa sababu hakuna soko, I mean hakuna bei elekezi ambayo ipo manageable, unakuwa huna cha kufanya inabidi uuze.
Mheshimiwa Naibu Spika, imagine nimetoka na mzigo kutoka kwa baba yangu kule Profesa Kabudi, Kilosa mpaka Dar es Salaam, mzigo ambao ninaenda kuuza kwa kilo shilingi laki na hamsini, nikifika Dar es Salaam ananiambia shilingi elfu nane. Siwezi kurudi nao ule mzigo Kilosa! Kwa sababu nilipokwenda mara ya kwanza alinunua kwa kilo shilingi laki na hamsini nilivyorudi nimeenda kukopa na kufanya kila kitu ili niongeze kilo nyingi kwa sababu ninajua nikipeleka Dar es Salaam nitauza kwa shilingi laki na hamsini.
Mheshimiwa Naibu Spika, nikifika Dar es Salaam akisema kwa shilingi elfu nane na tena ukienda muda mbaya anakwambia fanya haraka mimi nataka funga ofisi. Kwa hiyo, ukiangalia sasa mimi ninafanyeje, inabidi uuze kwa bei hiyo hiyo. Sasa hii hatukuzi Uchumi. Haya madini ni kweli yanauhitaji ndiyo maana hawa ndugu zetu zamani walikuwa wanakaa Dar es Salaam lakini sasa hivi ukienda Gairo, ukienda Dutumi, ukienda Kisaki wamejenga mpaka na nyumba. Wanachosema wenyewe wanatupa technical assistance lakini technical assistance kwetu kule Morogoro hawa majamaa wanatupa digger na jenereta ndiyo technical assistance.
Mheshimiwa Naibu Spika, anatupa digger na jenereta, lakini yeye anachukua 85%, anakupa 15%, anaondoka nayo. Kilichobakia kwamba vijana wetu wengi wamekuwa na stress na hawaoni thamani, mbaya zaidi haya madini wakiyauza wanaona kabisa hawa wanunuzi wanafaidika. Imefika sehemu sasa hivi unamwona Mchina anakuja kununua madini kijijini kule Kilosa amejenga na nyumba, lakini pesa anayonipa mimi siwezi hata kuezeka bati. Kwa hiyo, sasa hii kipekee kwa uchumi ambao tunataka kwenda nao kwa kweli, ni ngumu.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninaishauri Serikali hii technical support ambayo hawa wawekezaji wanakuja nayo kama kofia ya kuwekeza si kweli, hii technical support wanayoisema si kweli! Sisi ambao tupo chini tunajua, wanachokifanya wanachimba na likibaki shimo ambalo wanajua halina mwamba, halina mwendelezo anaondoka anaenda sehemu nyingine. Mbaya zaidi aina hizi za madini mchakato wake haufanyiki Tanzania, haya yanaondoka makinikia kama yalivyo, yanaenda kufanyika huko China.
Mheshimiwa Naibu Spika, at least hata tungekuwa tunachimba Tanzania, tunasema usafishaji wake labda kama dhahabu unafanyika Tanzania, watu wapate ajira, processing zingine zinafanyika Tanzania tungesema kweli at least hata kama unanunua kwa bei ndogo lakini some processes zinafanyika Tanzania na vijana wetu na ndugu zetu wanapata ajira.
Mheshimiwa Naibu Spika, akinunua sand stone na vumbi lake vilevile analibeba kupeleka China, akienda China anatengeneza ananiletea mimi tiles hapa, ananiletea vyoo, ananiletea taa. Kwa hiyo, ukiangalia kabisa ni kwamba thamani haipo, sisi wanatuachia mashimo, hawatuachii kitu na hizo CSR wanazosema hazipo. Kwa sababu, mtu anaahidi hizo CSR kama walivyotangulia wachangiaji wengine, ninaona sasa ni wakati ambao inabidi zifanyike kwa percentage. Kwa sababu mtu hawezi kuchimba madini, akapata thamani ya milioni 500 akajenga tundu moja la choo, hakuna kitu kama hicho.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kumalizia...
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa.
MHE. JOSEPHINE J. KAPOMA: Mheshimiwa Naibu Spika, hizi sehemu za uwekezaji wa madini, kaka yangu Mavunde anapoteza pesa nyingi.
NAIBU SPIKA: Ahsante sana, unga mkono hoja.
MHE. JOSEPHINE J. KAPOMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba kuunga mkono hoja, mengine kaka yangu nitakuja tuyaongee. Ahsante sana. (Makofi)