Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

Hon. Salehe Mbwana Mhando

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilindi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

MHE. SALEHE M. MHANDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nami nichukue fursa hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kupata nafasi ya kuchangia hotuba ya Wizara ya Kilimo kwa siku ya leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami pia nianze kumpongeza Rais wetu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa mapinduzi makubwa ambayo anaendelea nayo katika sekta hii ya kilimo hapa nchini. Hili halina ubishi, uwekezaji mkubwa unaofanywa na Serikali ya Awamu ya Sita katika kutekeleza ilani ya Chama cha Mapinduzi inaonekana na mambo yanaendelea kwa kiwango ambacho kinaleta tija. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, niwapongeze sana Mheshimiwa Waziri wa Kilimo Mheshimiwa Geodfrey Chokolo akisaidiwa kwa umahiri mkubwa na Naibu Waziri ndugu yangu Mheshimiwa Silinde, Katibu Mkuu pamoja na timu nzima ya Wizara ya Kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nianze kwa kuunga mkono hoja ya hotuba ya Wizara ya Kilimo na ninaunga mkono kwa maana kwamba katika Taifa letu na katika nchi yetu tumekubaliana kwamba kilimo ni uti, na Mheshimiwa Waziri ameboresha siyo uti wa mgongo, utii wa mgongo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo ni kwamba, hapa leo tunazungumzia hatima ya maisha ya Watanzania, na hatima ya uchumi wa Taifa letu. Kwa maana kwenye kilimo kule ndiko kunakofanya tunaweza kuishi, kupata chakula, utoshelevu wa chakula, usalama wa chakula, halikadhalika, kilimo sasa hivi ni biashara. Kwa hiyo, hapa tunazungumzia uchumi wa wananchi wetu kwa mtu mmoja mmoja, Taifa na tunazungumzia suala la uchumi katika pato letu la Taifa kwa maana ya kuweza kuuza nje ya nchi na kupata fedha za kigeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na muktadha huu, ninaomba nichangie hotuba hii katika eneo muhimu sana ambalo limeelezwa na Waziri katika hotuba yake ya bajeti, lakini kwa msisitizo mkubwa nimeisikiliza sana hotuba ya Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge. Eneo ambalo tunatakiwa kuliwekea uzito sana katika suala la kilimo, mapinduzi ya kilimo, ni suala la umwagiliaji. Kilimo tunahitaji tutoke kwenye kilimo cha msimu twende kwenye kilimo cha mwaka mzima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa hakuna njia nyingine zaidi ya uwekezaji kwenye miundombinu ya umwagiliaji. Katika miundombinu ya umwagiliaji, kwanza tukubaliane kwamba kupanga ni kuchagua, lazima fedha itoke iende kwenye eneo hilo. Miradi mingi tumeelezwa hapa, kwanza tuwe na miradi ya kimkakati tusipunguze miradi mingi, tukubaliane twende na miradi kadhaa ambayo tunaitekeleza mpaka ilete matokeo twende hatua nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe mfano, kuna miradi kadhaa ambayo leo imeelezwa hapa, ukienda huwezi ukakuta kuna mradi ambao sasa hivi unazalisha mara mbili kwa msimu, haupo. Kwa hiyo, bado safari ni ndefu. Hapa, nilikuwa niombe na kuishauri Serikali kupitia Wizara ya Kilimo, mamlaka, na Wizara ya Fedha; kati ya jambo ambalo tunatakiwa kwenda kumwachia alama Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwenye nchi hii ni kwenda kuitoa Tanzania kutoka kwenye kilimo cha msimu wa mvua kwenda kwenye kilimo cha msimu wa muda wowote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna fursa ya kuilisha Afrika, tuna fursa ya kuilisha dunia, na hata yanayoendelea duniani haya kwa upande mwingine kwa Tanzania sisi hii ni fursa. Leo hata hii miradi inayotekelezwa, tunatekeleza miradi ya kukinga maji ya mvua, baada ya mvua, ikiondoka, miradi ile na yenyewe haifanyi kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nashauri tuchague miradi. Kuna mabonde ambayo unajua kabisa ukisema Usangu, ukisema kule Mwamburu - Katavi, ukisema kule Morogoro, una hakika kwamba tukitengeneza miradi, Kilindi kule Tamota, miradi ambayo ukaweka miundombinu ya mabwawa, maji yakatengenezewa miundombinu ya umwagiliaji, tukazalisha kipindi cha mvua na kipindi cha kiangazi, haya ndiyo maana halisi ya miradi ya umwagiliaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninaomba hapa niweke msisitizo kwamba kilimo ni maji. Hakuna msamiati mwingine kwamba tutazalisha bila kuwa na maji. Kilimo ni maji na hili ninaomba niliwekee msisitizo kabisa kwamba hata nikiishia leo kuchangia hapa, nitakuwa nimesaidia Taifa letu kwamba kilimo ni maji na bahati mbaya sana tunapoteza maji. Mvua zinanyesha, tunalalamika hapa. Kuna jambo halijakaa sawa sawa kwenye mipango na kwenye utekelezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, twende tukatumie hii baraka ya Mwenyezi Mungu kutupa mvua kwa ajili ya faida ya uzalishaji wa mara mbili mara tatu kwa msimu tuwe sisi ndiyo ghala la chakula kama inavyoelezwa kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo nilitaka kulichangia leo ni suala zima la zana za kilimo. Eneo la zana la kilimo nalo hili ni eneo muhimu sana katika kuleta mapinduzi ya kilimo hapa nchini, na nipongeze sana jitihada za Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan na Wizara husika ya Kilimo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hili ninaomba sana Jimbo la Kilindi, Wilaya ya Kilindi, lile ndiyo eneo la uzalishaji kwenye ukanda wa kaskazini likiungana na wenzake wa Kiteto. Ninaomba sana katika ule mpango wa kusambaza matrekta, power tiller maeneo haya yapewe kipaumbele kwa sababu ndiyo yanayolisha ukanda mzima wa kaskazini na nchi jirani ya Kenya na maeneo mengine. Ninaomba tulitumie hili eneo kuwekeza katika miundombinu au vitendea kazi kama matrekta, power tiller kwa wakulima wetu ili tuhakikishe kwamba tunakwenda kuongeza tija, kuongeza uzalishaji na mwisho wa siku kuinua pato la wananchi wetu na pato la Taifa kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nitoe rai na nitoe ushauri kwamba pia katika eneo hili twende kwa maeneo tuangalie vipaumbele vya maeneo. Ninaomba tukubaliane, tukiamua kwenda kwa utaratibu wa kwamba hivi vitu tunatapanya, peleka huku kimoja peleka huku viwili, havitoi matokeo, hatupati tija.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba tukubaliane, tunaposema tunapeleka hapa, tupeleke kitu kilete matokeo, na yale matokeo yatoe tija, tuhamie sehemu nyingine. Tutafika kwenye maeneo yote, lakini kwa kwenda kwa utaratibu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni suala la masoko, na hapa nilikuwa ninaomba kuzungumzia NFRA. Moja ya chombo ambacho kinaweza kikaleta na kikachachusha masoko ya ndani ni kupitia NFRA. Changamoto ya NFRA; mfumo wa upatikanaji wa fedha kwenye NFRA unabishana na masuala ya masoko kwa wakulima kule kwenye maeneo yetu. Ukipeleka fedha mwezi wa Tisa, hiyo fedha haimnufaishi mkulima. Kuna watu wamekusanya, wameweka kwenye store ndio wanaonufaika na fedha zile za NFRA, lakini mkulima ambaye amehangaika amejishughulisha na kilimo kwa miezi yote ile, anajikuta ameangukia kwenye walanguzi, amepata hela ndogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho wa siku unapokuja kupeleka NFRA fedha, zinakwenda kunufaisha watu ambao hatujakusudia. Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan anakusudia kwenda kupeleka tabasamu kwa Watanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mfumo wa upatikanaji wa fedha za NFRA utazamwe, ikibidi apewe fedha mwezi wa Pili, au wa Tatu tayari kwa maandalizi. Mavuno yanaanza mwezi wa Tano na wa Sita, wawe wameshajiipanga, wahakikishe kwamba ule utaratibu tuliouweka wa kupeleka mifumo ya ukaushaji mazao tukawasaidie wakulima ili tuiwezeshe NFRA inunue mazao ambayo yamekaushwa vizuri, yanahifadhika, na pia kuweza kuwapa wananchi soko la uhakika na kuleta ushindani kwa wanunuzi binafsi kwa kipindi husika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuchangia hayo, ninakushukuru sana kwa kunipa nafasi, ninaunga mkono hoja. (Makofi)