Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Kakonko
Contributions
nil
Answers
nil
Commettees
1
Ministries
nil
MHE. ALAN T. MVANO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii. Nianze kwa kumshukuru sana Mwenyezi Mungu ambaye anaendelea kutujalia afya njema, vilevile niendelee kuwashukuru sana wananchi wa Kakonko kwa kuniamini na kunituma kuwawakilisha katika hili Bunge Tukufu. Ahadi yangu kwao ni kwamba, nitaendelea kufanya kazi hii kwa uaminifu na nitafanya kazi hii kwa maslahi mapana ya Wilaya ya Kakonko na Nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe vilevile pongezi kwa Mheshimiwa Rais na Mheshimiwa Waziri kwa kazi kubwa ambayo wanaifanya. Katika Wilaya ya Kakonko yapo mambo ambayo tumeyaona yamefanyika kwa kipindi kifupi, ikiwa ni pamoja na kutuletea mbegu za alizeti za ruzuku. Kwa kweli wananchi wa Kakonko wanashukuru sana, tumepokea na kazi inaendelea ndani ya Wilaya ya Kakonko. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili tunashukuru pia tumepata Kituo cha Utafiti wa Mazao katika Wilaya ya Kakonko na tumekwishatenga ekari 267 na kazi inaendelea. Jambo la tatu, tunashukuru pia wakulima wetu wa tumbaku wamekaa muda mrefu bila kulipwa na siku mbili zilizopita wamepokea malipo ya zaidi ya milioni 300. Tunaishukuru sana Serikali hii inaongozwa na Dkt. Samia Suluhu Hassan, tunaamini na fedha nyingine ambayo haijalipwa, italipwa ili wananchi wetu waendelee kufanya shughuli zao vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Kakonko ingependa kuona mambo kadhaa yanafanyika katika mwaka huu wa fedha. Jambo la kwanza ni kukarabati miundombinu ya umwagiliaji na kujenga ile ambayo haijajengwa. Kwanza kabisa tuna maeneo ya Itumbiko, Liwiti, Katengela, Mwiluzi na Bwaru. Maeneo hayo yote yanafaa kwa kilimo cha umwagiliaji, kwa hiyo tunaamini ili tuweze kuboresha uzalishaji katika sekta ya kilimo, basi Wizara ituangalie kwa jicho la pekee maeneo hayo ili miundombinu iweze kutengenezwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, tunaomba sana kiwanda cha kuchakata na kuongeza thamani zao la muhogo kama ilivyoahidiwa, basi jambo hili nalo lifanyike ili wananchi waweze kuona faida katika zao hilo. Jambo la tatu, tumetenga ekari zaidi 1,000 kwa ajili ya block farming ya zao ya parachichi, tunaiomba Serikali ilione pia eneo hilo ili tuweze kufanikiwa na wananchi wetu waweze kupata manufaa ya kilimo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la nne, tunaomba pia zana za kisasa za kilimo ziweze kufika katika Wilaya ya Kakonko, kwa sababu bado wapo wananchi wengi ambao wanaendelea kulima kwa kutumia jembe la mkono. Jambo la mwisho katika mambo ambayo tungependa kuona yanafanyika, ni kuendelea kuhakikisha pembejeo zinapatikana kwa wakati ili wakulima wetu waweze kufanya vizuri na kuongeza uzalishaji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mambo yote hayo nimetoa pongezi kwa Serikali na nimeona mpango mzuri wa Waziri na mpango mzuri wa Rais. Mambo haya yote yakifanyika maana yake ni kwamba, tunakwenda kuona mageuzi katika uzalishaji wa mazao yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa pendekezo langu mimi ninajikita katika eneo la masoko. Pamoja na mambo mengine yote yatakayofanyika tusipoliangalia vizuri eneo la masoko maana yake ni kwamba tunakwenda kuzalisha kitu kikubwa na mwisho wa siku tutakosa pakupeleka. Jambo la kwanza la kuangalia Wizara hii kwa kushirikiana na Wizara nyingine lazima ije na mpango mkakati wa namna ya kuendea masoko. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, soko la kwanza la muhimu la kuangalia ni sisi wenyewe Watanzania tupo zaidi ya milioni 70 maana yake ni kwamba tukiwa na mkakati mzuri sisi wenyewe tutakuwa soko la kwanza kwa mazao tunayozalisha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili soko la nchi za jirani yapo mambo yanapaswa kufanyika ili tuweze kuyaendea masoko hayo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza, tujenge maghala maeneo ya mipakani ili watu wanaotaka kupeleka mazao nje ya nchi yetu waweze kuwa na sehemu ya kuhifadhia mazao yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, Serikali ijikite katika kuhakikisha kilimo kinachofanyika kinakuwa ni kilimo cha mkataba, watu wasilime bila kujua watapeleka wapi mazao yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu, lazima Wizara ije na mpango wa kuhakikisha wananchi wetu wanapata elimu ya kilimo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza wajue wanapolima wanatumia mbolea gani kwa ardhi gani? Vilevile masoko ya mazao yanapatikana wapi? Kwa hiyo ninashauri Wizara ije mpango wa kuandaa channel maalum kwa ajili ya television zetu kama walivyofanya wenzetu wa utalii Safari Channel inafanya vizuri, watu wakiangalia wanaona fursa zilizopo, tuangalie kwenye channel zetu na redio zetu, zitoe habari za elimu kwa ajili ya wakulima wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimejikita katika eneo hili kwa sababu jukumu la kumi la Wizara ya Kilimo ni kutafuta masoko na kuratibu masoko, lakini eneo la tatu ni masoko ya kimataifa. Hapa ninapendekeza kwamba Wizara ije na mpango mkakati wa kuyaendea masoko ya kimataifa kwa kuwatumia Mabalozi wetu walioko katika nchi za mbali. Moja kati ya eneo la kupima performance ya Mabalozi wetu iwe ni pamoja na kuangalia exports wanazozifanya kutoka Tanzania kupeleka kwenye nchi zao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mambo haya yote muda hauwezi kutosha kuelezea haya, ninaomba sana Serikali iangalie eneo hili la masoko.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa, pendekezo langu kwa sababu lazima mambo haya yaende pamoja, unaona Wizara ya Uchukuzi inaingia lazima liweke vizuri miundombinu, unaona Wizara ya Viwanda na Biashara inaingia kwa sababu lazima tutafute masoko. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapendekeza ikimpendeza Mheshimiwa Rais aunde Wizara maalum ya masoko ili sasa iende kufanya kazi moja kwa moja kwa kushirikiana na Wizara nyingine ili tuweze kuyatafuta masoko ndani, tutafute masoko ndani ya nchi jirani na tutafute masoko katika nchi za mbali
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kutoa mchango huo ninakushukuru sana na ninaunga mkono hoja. (Makofi)