Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

Hon. Sara Msafiri Ally

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Mvomero

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

MHE. SARA M. ALLY: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia kwenye hii bajeti ya Wizara ya Kilimo. Kipekee ninamshukuru sana Waziri na timu yake kwa hotuba nzuri aliyoitoa yenye mipango endelevu ya kuongeza tija kwenye kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda nitoe shukrani zangu sana kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge, ambayo inashughulikia masuala ya kilimo kwa ushauri mzuri sana ambao Mwenyekiti ameutoa kwenye mchango wake binafsi na kwenye hotuba yake hasa kuongeza masoko na kufanya utafiti kwenye mbegu, kwenye mbolea na namna ya viwanda vyetu vitakavyoongeza uzalishaji na kufanya tathmini kwa wale ambao wameshindwa kuendeleza viwanda, tuone namna nzuri ya kuwaondoa na kuweka wawekezaji wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa ziara aliyoifanya ndani ya Jimbo la Mvomero akiambatana na Waziri wa Mipango na Uwekezaji. Walitembelea maeneo ya uwekezaji ya viwanda vya sukari na mashamba ya miwa, walipata fursa ya kuona changamoto za viwanda ambavyo vinazalisha kwa kiwango kikubwa zaidi ya malengo, lakini changamoto ipo kwa wakulima wa miwa, miwa yao haivunwi kwa wakati na hivyo wanapata hasara kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na masuala ya kuingiza sukari na Mheshimiwa Waziri kwa pamoja walisema watalishughulikia hili. Salamu za wananchi wa Mvomero wana imani kubwa na Mheshimiwa Waziri, ninaamini hakutakuwa tena na kuharibika kwa miwa ya wakulima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee kabisa ninakushukuru sana Mheshimiwa Waziri na Serikali, Jimbo la Mvomero lina skimu za umwagiliaji 10 na skimu hizi 50% tayari Serikali imefanya usanifu bado fedha, lakini kwa kipekee tunashukuru kwamba zipo skimu ambazo Serikali imeshatoa fedha. Skimu za Lukenge, Mgongola, Misufini, mkandarasi amepatikana. Skimu ya Dakawa tayari hekta 3,000 zinafanya uzalishaji wa 100%, tunashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijikite kwenye changamoto za kusuasua kasi ndogo ya uwekezaji kwenye miundombinu hii hasa kwenye skimu ambazo Serikali imeshatoa fedha. Tunayo Skimu ya Mgongola, skimu hii imeanza ujenzi tangu mwaka 2021, mkandarasi akaleta changamoto zake, mradi ukasimama wa shilingi bilioni 5.6, Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan alitupa fedha, mkandarasi akalipwa bilioni 1.7, akapotea akaishia mitini, kwa hiyo skimu ile ipo tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaishukuru sana Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa kipindi cha muda mfupi alichokaa ofisini kwake, ameweza kutoa ushauri wa namna ya kuachana na huyu mkandarasi, mkandarasi huyu sisi ametushinda. Serikali ya Wilaya, Serikali ya Mkoa, Tume ya Umwagiliaji wamehangaika naye imeshindikana fedha zetu amechukua 1.7 bilioni na fedha iliyobaki ni pungufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba ushauri alioutoa Mwanasheria Mkuu wa Serikali, basi tuiombe Tume ya Umwagiliaji tuna Mkurugenzi Mkuu mchapakazi pale, masuala ya kisheria yamekwisha ili sasa tuachane na mkandarasi, tukamalizie. Nishauri kwa sababu muda umeenda ni zaidi ya miaka mitatu sasa tangu fedha zitolewe na Serikali na mradi umesimama, niiombe Tume ya Umwagiliaji ikafanye mradi ule kwa force account ili sasa wananchi wale wa Jimbo la Mvomero hasa eneo la Tulia ambapo kuna mafuriko waweze kunufaika na miradi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunao pia mradi mwingine ambao Mheshimiwa Waziri ametuahidi, ni Mradi wa Lukenge ambao Serikali imewekeza 1.4 billion, mradi umekamilika kwenye miundombinu bado pampu. Mheshimiwa Waziri na Serikali wametuahidi kwamba tarehe 30 mwezi huu ambao ni keshokutwa watakuwa wametununulia pampu ya shilingi milioni 800 ili wananchi wale wakafanye uzalishaji. Sasa kwa sababu miundombinu imekamilika miaka miwili iliyopita, ilibaki pampu ambayo Mheshimiwa Waziri ametuahidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine niombe ndani ya skimu zetu za Jimbo la Mvomero, tuna hekta 41,883 uwekezaji uliofanywa na Serikali ni 19% tu sawasawa na hekta 8,002. Kama wenzangu walivyoongea na Wabunge na Kamati ya Bunge ilivyoshauri tunahitaji mapinduzi ya kilimo kwenye kilimo cha umwagiliaji kwa sababu kinakopesheka, tuna uhakika wa kuvuna na tuna uhakika wa masoko. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaiomba Benki ya Kilimo, Tume ya Umwagiliaji na Serikali wakae waone namna ya kuleta mapinduzi kwenye sekta ya kilimo hasa kwenye kilimo cha umwagiliaji chenye uhakika ili sekta ambayo imeelekeza kwenye Jimbo langu kwenye 19% tu tuweze tukawekeze kwenye 100% ili tuweze kuzalisha kwa tija. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni mbolea wameongea wenzangu. Tunavyo viwanda vya ndani vya mbolea, Serikali ione namna ya kusaidia viwanda hivi vikopesheke viweze kuzalisha mbolea ya kutosha na ya uhakika ili wakulima wasipate tabu ya mbolea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, ninashukuru sana na ninaunga mkono hoja. (Makofi)