Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Mbulu Vijijini
Contributions
nil
Answers
nil
Commettees
1
Ministries
nil
MHE. DKT. EMANUEL Q. NUWAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote ninamshukuru Mwenyezi Mungu kwa uhai, hadi kupata nafasi hii ya kuchangia bajeti hii ya Wizara ya Kilimo. Ninapenda kumpongeza Mheshimiwa Rais pamoja na Mheshimiwa Waziri wetu wa Kilimo kwa mpango mzuri ambao amewasilisha kwa ajili ya maendeleo ya kilimo hapa nchini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunasema kilimo ni mama na baba wa Wizara zote; kwa sababu katika kilimo tuna ajira, tunapata nishati, biashara, afya, maana madawa yote nayo yanatokana na mimea, lakini vilevile katika kilimo tunapata lishe pamoja na chakula. Kwa maana ya ajira, tunaona zaidi ya 80% ya wananchi wetu wanapata ajira kupitia sekta hii ya kilimo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda kusema mambo mawili; la kwanza, hii Wizara ni Wizara ya kimkakati kama ilivyo Wizara za Uchukuzi na Nishati. Ningeomba Mheshimiwa Waziri ahakikishe anaongea na hawa, kwa sababu tunapojenga SGR, tunapoboresha bandari, ni lazima tuhakikishe kwamba bidhaa zitakazopita katika barabara, katika SGR na bandarini ziwe ni bidhaa zinazotokana na kilimo chetu. Kwa hiyo hii Wizara ni Wizara muhimu sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama walivyosema Waheshimiwa Wabunge, ninapenda kuishauri Serikali kwamba, bajeti ya upande wa umwagiliaji itoke nje ya bajeti ya kawaida kwa sababu ni eneo la kimkakati. Vilevile, eneo la uzalishaji wa mbolea, tunaona uzalishaji upatikanaji wa mbolea ni kiasi cha 83% ambacho si kiwango kinachotakiwa; lakini bado zaidi ya 60% inatoka nje ya nchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunajua kwamba kule duniani tuna mgogoro wa kivita kati ya nchi nyingine; hivyo kutakuwa na changamoto ya upatikanaji wa mbolea katika mwaka unaokuja kama ambavyo tunaona kwenye mafuta. Kwa hiyo, tunaiomba Wizara iweze kuweka mpango mkakati wa mapema wa kuhakikisha kwamba mbolea zitaendelea kupatikana katika msimu unaokuja kwa ajili ya kilimo chetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, upande pia wa uzalishaji wa mbegu, bado pia mbegu zetu haziwi za kutosha. Ningeomba Wizara nayo itenge fedha maalum kwa ajili ya kuongeza uzalishaji wa mbegu. Moja ya eneo ambalo ninapenda kuchangia, amechangia Mheshimiwa Mbunge mmoja; tuna tatizo la uwepo wa mbegu feki katika majira yale ya kilimo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, inaumiza sana mkulima pale ambapo ananunua mbegu 15,000 au elfu kumi na ngapi, anapokwenda kupanda acre zote zinakuwa haziwezi kuota. Lazima udhibiti uwepo na namna ya pekee ni kuongeza uzalishaji wetu wa ndani kwa upande wa mbegu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande pia wa mbolea, tunajua kwamba mbolea ambayo tunayo hapa nchini bado katika nyakati za kilimo kuna wafanyabiashara wachache wanatumia zile fursa. Ninaishauri Serikali kwamba, wale wauzaji na wale mawakala wawe wanaweka bei za mbegu na bei za mbolea kwenye milango, ili mkulima anapofika aone kabisa haitaji kuuliza na iwe ya wazi. Hii itajenga uwazi katika kupata mbolea, lakini pia mbegu kwa bei nzuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nichangie kwenye eneo la mazao machache. Zao moja ni dengu ambalo liko kwenye stakabadhi ghalani. Hakika imekuwa changamoto kwa wakulima wengi. Kwanza, hawapati mbegu nzuri, wanatumia zile zile ambazo walipanda mwaka jana; lakini pili, masoko yao si ya hakika kwa sababu maghala yako machache sana na wakulima hutumia umbali mrefu sana kusafirisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba na ninashauri tuweke soko huria, lakini hao wanaonunua miongoni mwa wakulima waishie kwenye sehemu ya stakabadhi ghalani. Tusitengeneze mazingira ya changamoto kwa wakulima wetu ambao wengi ni wadogo wadogo na wengi wanatumia gharama kubwa sana. Ninaomba tutengeneze soko huria kwenye eneo hilo. Wale wanaotaka kuuza kwa mfumo wa uhuru wauze lakini wote waishie kwenye stakabadhi ghalani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda kuchangia kwenye eneo la zao la vitunguu maji pamoja na karoti ambalo bado ni changamoto, wengi wanauza kwa mfumo wa lumbesa. Hata leo ukienda kwenye soko la mazao haya kwenye mkoa wowote, bado lumbesa ni changamoto. Mheshimiwa Waziri Mkuu ametoa maelekezo, ninaomba Mheshimiwa Waziri wetu alisimamie hili kikamilifu ili wakulima wapate faida ya mazao yao wanayoyapata. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, zao la mahindi ambalo hakika linalimwa sana katika mkoa wangu na katika jimbo langu ambalo ninaliongoza; mahindi mwaka huu tumepata bahati na tunaona tutapata mazao ya kutosha. Tunamshukuru Mwenyezi Mungu. Tunaomba Serikali itusaidie kupitia NFRA, kwanza kuweza kutoa bei nzuri ili kuwasaidia wakulima ambao wamenunua mbegu na pia wamenunua mbolea. Vilevile, kufungua mipaka mapema ili tupate bei nzuri ambayo itatusaidia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo langu la mwisho ni eneo la umwagiliaji. Tunamshukuru Mheshimiwa Rais Samia, tumepata skimu tatu, tumepata mabwawa mawili. Ninaomba Serikali iweze kukamilisha mradi huu. Tumepata pia visima sita katika kata zetu na zitaenda kusaidia kuongeza wigo wa kilimo cha umwagiliaji ambacho ni kilimo cha hakika sana. Nipende kumpongeza Mheshimiwa Rais Samia kwa ajili ya mradi huo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la mwisho ni eneo la mradi wa BBT. Tunaomba BBT ishuke katika halmashauri ambako ndiko vijana wako na ndiko mashamba yaliko. Tushushe chini ili vijana wengi wakajiajiri kule ili waweze kuzalisha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nizungumze kwamba, kilimo bila vifaa na teknolojia haiwezekani. Matrekta na power tiller tunashukuru tumesikia kwamba yatakuwepo na yatakopeshwa. Masharti yawe nafuu na yaweze kusambazwa hasa katika maeneo ya vijijini ambako ndiko wakulima waliko. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, ninaomba kukushukuru sana na kusema ninaunga mkono hoja kwa asilimia mia kwa mia. (Makofi)