Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

Hon. Dr. Lazaro Killiani Komba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Peramiho

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

MHE. DKT. LAZARO K. KOMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa nafasi, lakini nitumie pia nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijaalia zawadi hii ya uhai.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano mama yetu Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoifanya katika kuimarisha sekta hii ya kilimo. Kazi hii si ndogo na pongezi hizi ninazozitoa nitazitoa kwa takwimu ili tujue kabisa kwamba kazi kubwa anayoifanya Mheshimiwa Rais inaonekana pia katika maisha ya kawaida na vilevile iko vizuri katika takwimu tulizonazo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri, kaka yangu ambaye sisi tunaomfahamu tunamfahamu kwa ufanisi wake mkubwa katika kazi anazozifanya na hajawahi kushindwa mahali popote alipopata kufanya kazi. Hongera sana kwa Mheshimiwa Waziri, wananchi wa jimbo la Peramiho huwa wanaamini sasa shamba limepata mkulima, kwa hiyo mazao lazima yaongezeke kupitia Mheshimiwa Waziri na timu yake yote akisaidiana na Naibu Waziri ndugu yangu Mheshimiwa Silinde.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimetoa pongezi hizi nikiwa nina takwimu zinazopelekea tutoe pongezi hizi. Tutakumbuka Mwaka wa Fedha 2021/2022 uzalishaji wa mahindi katika nchi hii ulikuwa ni tani 6,950,000, wakati mahitaji ya chakula ndani ya nchi ilikuwa ni tani milioni 5,900,000, na hivyo tukawa na ziada ya tani 950,000, ziko pembeni. Miaka michache baadaye, ni miaka miwili tu baadaye uzalishaji uliongezeka kwa kiwango kikubwa kutoka tani milioni sita mpaka kufika tani milioni 10,925,000 kwa mwaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati huo huo matumizi yetu pia yalikuwa yameongezeka kwa sababu ya ongezeko pia la idadi ya watu. Tukawa tunahitaji kutumia ndani ya nchi tani 7,300,000. Hivyo kupelekea kuwa na ziada ya chakula kwa takribani tani 3,600,000. Hizi zipo zinahitaji kutoka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, takwimu hizi hazijaja kwa bahati mbaya. Takwimu hizi zimekuja kutokana na kazi kubwa inayofanywa na Wizara ya Kilimo kwa maelekezo ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye amepanga kuimarisha na kukuza sekta ya kilimo ambayo kimsingi inaajiri kwa kiwango kikubwa katika nchi hii ukilinganisha na sekta nyingine tulizonazo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme jambo moja; ongezeko hili limesababishwa na ongezeko la pembejeo zile za ruzuku; kwa maana ya mbolea, mbegu, pamoja na madawa. Mwaka wa Fedha 2021/2022 tulikuwa tuna uwezo wa kununua mbolea tani 7,241, lakini miaka miwili, mitatu baadaye ongezeko limekuwa kubwa sana. Tunapata sasa mbolea ya ruzuku kwa tani 21,457 kwa mwaka mmoja. Ongezeko hili ukilitazama ni mara tatu ndani ya kipindi cha miaka miwili. Si jambo dogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa, maendeleo yoyote yana tabia ya kuzalisha matatizo. Tumeongeza uzalishaji kwa kiwango kikubwa lakini uzalishaji huu umezalisha tatizo la upatikanaji wa masoko. Sisi wakulima wa mahindi wa Jimbo la Peramiho soko letu kubwa lenye uhakika ni NFRA; na NFRA ukiitazama imekuwa inaongeza kiwango cha kununua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2022 ilikuwa imenunua tani takribani 58,000, lakini hivi tunavyozungumza kwa msimu uliopita NFRA wameongeza na wakanunua tani 457,000. Ongezeko ni kubwa, lakini ongezeko hili haliendani na ongezeko la uzalishaji wa mahindi na hivyo kutengeneza uhaba wa soko kwa kiwango kikubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii kuishauri Serikali katika mambo yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza, niishauri Serikali, juhudi kubwa inayofanya katika kuhakikisha sekta ya kilimo inaimarika na kuongeza uzalishaji, juhudi ile ile itumike katika kutafuta masoko ya nje kwa sababu ndani tayari pamekwishajaa na hatuwezi kuuziana wenyewe kwa wenyewe wakati wote tunazalisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wa pili kwa Serikali; ukitazama katika takwimu nilizozitoa tuna akiba ya tani 3,600,000. Ukitoa ile inayonunuliwa na NFRA ambayo ni tani 445,000 na ile inayouzwa nje ya nchi, kwa maana ya mahindi kutoka nje ya tani 665,000, bado tunabaki ndani ya nchi na akiba ambayo haijakwenda kokote ya tani 2,500,000, ambazo kimsingi hizi ziko katika maeneo mawili. Either ziko kwa wananchi na zimeshindwa kufika sokoni au zimeharibika kwa sababu wamekosa maghala ya kuhifadhia mazao haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ushauri wangu wa tatu kwa Serikali, tuiombe sana Serikali. Sisi wananchi wa Jimbo la Peramiho tunazalisha kwa kiwango kikubwa mahindi; na kwa sababu tunashindwa kuyauza yote kwa wakati, yale yanayobaki tunaomba sana tujengewe maghala katika maeneo manne nitakayoyataja. Tunaomba kujengewa ghala katika Kata za Ndongosi, Kata ya Mbinga Mhalule, Kata ya Magagula na Kata ya Kilagano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukifanya hivi tutakuwa tumesaidia sana maeneo mawili. Jambo la kwanza tutaimarisha uzalishaji na jambo la pili tutashawishi vijana ambao wanapaswa kuingia katika sekta hii kama sehemu ya maisha yao kuwa na fursa na kuona kilimo ni sehemu ya biashara na kwamba biashara hii inakwenda kuimarisha maisha yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikaona nitumie nafasi hii kutoa ushauri katika maeneo haya. Nikushukuru sana kwa nafasi. Niendelee pia kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Naibu Waziri kwa kazi kubwa wanayoifanya na sisi wananchi wa Jimbo la Peramiho tuna imani sana na Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana na ninaunga mkono hoja. (Makofi)