Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

Hon. Hemed Sumry Haidary

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

MHE. HAIDARY H. SUMRY: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote ninamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya na uhai. Niendelee kumpongeza na kumshukuru sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa ambayo ameifanya kwenye eneo hili la sekta ya maji kwenye nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakuwa mchoyo wa fadhila kama nisipomshukuru Mheshimiwa Waziri wa Maji na Mheshimiwa Naibu wake na wataalamu wote wa Wizara hii kwa kazi kubwa na nzuri wanayoifanya kwenye eneo hili la kuwahudumia wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mji wa Mpanda uko miongoni mwa miji ambayo ina miradi ya miji 28. Mradi huu ukikamilika utakwenda kupunguza kabisa changamoto ya maji tuliyonayo kwa sababu Mji wa Mpanda kwa sasa unapata lita milioni sita, lakini mradi huu ukikamilika, utatuongezea upatikanaji wa maji kutoka lita milioni sita mpaka lita milioni 18.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunaona kabisa mradi huu utaenda kuwa mkombozi kwa wananchi wa Jimbo la Mpanda mjini. Ombi langu kwa Wizara ni kwamba itusaidie kusukuma huu mradi kwa sababu mradi huu ulikuwa ukamilike Oktoba, 2025 lakini kuna ahadi ya Wizara kwamba mradi huu utakamilika mwezi wa Saba mwaka 2025, lakini kinachoendelea kule site kinatutia mashaka kwamba mradi huu utaenda kukamilika huu mwezi wa Saba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamwomba sana ndugu yangu Mheshimiwa Aweso, kaka yangu, twende atusaidie ku-push hawa wakandarasi ili mwezi wa Saba kweli maji yatiririke Mpanda na changamoto ya maji iondoke kwenye Mji wetu wa Mpanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja yangu ya pili, tuna kata za pembezoni ambazo zilikuwa zinahudumiwa na RUWASA, lakini kwa kuwa mji wetu ni Manispaa, miji yote ile ya pembezoni imerudishwa kuhudumiwa na Mamlaka ya Maji Mpanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna miradi mfano kwenye Kata ya Mwamkulu, Kata ya Kakese, Kata ya Misunkumilo na Kata ya Magamba; kwenye kata hizi za pembezoni kuna miradi ambayo ilikuwa inafanywa na RUWASA, lakini sasa hivi imekuwa kama imesimama kwa sababu ukienda Mamlaka ya Maji hamna bajeti yake. Ukienda RUWASA, wameshaikabidhi Mamlaka ya Maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamwomba ndugu yangu, kaka yangu Mheshimiwa Aweso aende akaiamshe hii miradi. Wananchi wa Kakese na Mwamkulu wanasubiria hii miradi ikamilike ili waweze kupata maji kama yeye alivyosema, maji hayana mbadala, na ni ukweli usiyopingika kwamba maji hayana mbadala. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba hii miradi iende ikakamilike ili iweze kuwahudumia wananchi wangu wa Jimbo la Mpanda Mjini. Ninaamini huko waliko wananisikia, ninaongea Mheshimiwa Mbunge wao hapa, message imefika na ninaomba kama kuna uwezekano, kama ni Waziri au Naibu Waziri, basi waende wakatembelee kwenye hizi kata ili wakaone adha ambazo wananchi wanazipata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna ya pekee ninamshukuru Mheshimiwa Waziri. Kipindi cha kampeni, yeye na Mheshimiwa Mgombea wa Urais walikuja kwenye jimbo langu, na mimi kama mgombea kipindi kile nilimwomba sana aende akaitembelee Kata ya Magamba, lakini akaniambia ndugu yangu Sumry, mimi sasa hivi siyo Waziri, hapa nimemsindikiza tu Mheshimiwa Rais kuja kuhakikisha kwamba tunapata kura za kutosha, lakini ninakuahidi baada ya Mheshimiwa Rais kuchaguliwa, na Mungu akijalia nikawa Waziri wa Maji, nitahakikisha hiyo Kata ya Magamba tunakwenda kupeleka maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninamwomba sana Mheshimiwa Waziri kwenye jimbo langu, hii Kata ya Magamba na ilikuwa commitment yangu kwa wananchi kwamba nitapambana usiku na mchana, nitashawishi kuhakikisha kwamba wanapelekewa maji. Ziko dalili, nimeongea na Mkurugenzi wa Mamlaka ya Maji Mpanda ameniambia ziko dalili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, dalili peke yake hazitoshi. Ninamwomba sana Mheshimiwa Waziri, kwenye bajeti hii awapelekee maji wananchi wa Kata ya Magamba na watamwandika kwenye historia kwa sababu kata hii ni kata kubwa, lakini kuna kisima kimoja na wananchi wote wanaenda kuteka hapo maji kwenye kisima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri akienda kukitembelea hiki kisima anaweza akakuta ndoo zaidi ya 2,000 zinasubiria huduma ya maji. Kwa hiyo, ninaomba sana chondechonde Mheshimiwa Aweso anisaidie, aniokoe kwenye hili eneo, wananchi wa Kata ya Magamba nao waweze kupata maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamshukuru sana Mheshimiwa Waziri amekuja kwenye Mkoa wa Katavi mimi nikiwa Meya na Waheshimiwa Wabunge wa Mkoa wa Katavi tukamsukuma kuhakikisha kwamba...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa malizia kwa kuunga mkono hoja.

MHE. HAIDARY H. SUMRY: Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naongelea mradi ule wa gridi ya Taifa, nafikiri Mheshimiwa Waziri amenielewa, tumeona na tunaomba a-push ili mradi huu uanze.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana, ninaunga mkono hoja. (Makofi)