Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Sex
Female
Party
CCM
Constituent
Special Seats
Contributions
nil
Answers
nil
Commettees
1
Ministries
nil
MHE. GHATI Z. CHOMELE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwa nafasi ya kuchangia. Nami pia nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa na nzuri anayoifanya katika nchi yetu na hasa kwa kuhakikisha anaendelea kumtua mwanamke wa Kitanzania ndoo kichwani kama dhamira yake inavyojieleza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ninampongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Maji, Jumaa Aweso, kwa kazi nzuri anayoifanya katika kumsaidia Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwenye Wizara hii ya Maji yeye pamoja na Naibu Waziri na Katibu Mkuu wetu wa Maji, dada yetu mahiri sana, mchapa kazi Eng. Mwajuma na Watendaji wote wa Wizara hii kwa kazi nzuri wanayoifanya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nami pia sitaacha kuwapongeza sana Watendaji wa Wizara hii katika Mkoa wangu wa Mara kwa namna wanavyopambana kuhakikisha wanamtua ndoo mwanamke wa Mkoa wa Mara. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi hizo, bado kuna changamoto katika Mkoa wetu wa Mara. Tunashukuru sana kwa miradi ambayo imeletwa katika Mkoa wetu wa Mara, tumepata miradi 77 ya maji lakini miradi hiyo ina thamani ya shilingi bilioni 265 ambayo itaenda kuwanufaisha wananchi 985 katika Mkoa wetu wa Mara. Pia, tumepata miradi sita mipya ya maji yenye thamani ya shilingi bilioni 1.6. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi tunapokea, tatizo kubwa tulilonalo katika Mkoa wetu wa Mara ni kutokukamilika kwa miradi. Mimi ninaomba Waziri utakapokuja kuhitimisha hoja yake atuambie miradi hii ambayo ametupatia Mkoa wa Mara itakamilika lini? Hili ni tatizo kubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2024 tulisaini mradi wa maji wa miji 28 wa shilingi bilioni 134. Fedha hizo mpaka sasa mradi wa maji wa miji 28 haujakamilika, uko 15%.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna ambao tulisaini nao mradi huu, wao wako 80% na wengine 70%, lakini sisi 15%. Hii ni aibu kubwa sana. Tumezunguka kwa wananchi wa Mkoa wa Mara, akinamama wa Mkoa wa Mara tumewaambia dhamira njema ya Rais ya kuwatua ndoo kichwani, lakini mpaka sasa mradi ule mkandarasi hayupo site, mradi haujakamilika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo Wana-Mara tutaondoka na shilingi ya Mheshimiwa Waziri ili kusudi aje atuambie ule mradi utakamilika lini? Mkandarasi atalipwa lini? Mradi ule ukikamilika utaenda kuwasaidia mama zangu wa Wilaya ya Rorya, wa Wilaya ya Tarime Mjini na Jimbo la Tarime Vijijini baadaye na Serengeti. Hizi ni Wilaya ambazo zinateseka sana suala la upatikanaji wa maji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna vijiji vingi havina maji. Mheshimiwa Waziri, ametembelea Mkoa wa Mara, amejionea namna gani akina mama wanateseka, lakini kuna sehemu tunashukuru amezigusa, ninaomba atakapokuja hapa atuambie ni lini mkandarasi wa mradi ule atapewa fedha ili aweze kukamilisha ule mradi? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kuipongeza Wizara hii. Tuliwahi kupata shilingi bilioni 70 kwa ajili ya kutekeleza mradi wa Mgango - Kiabakari na sasa ule mradi unaendelea kufanya vizuri, ila kuna kata moja ambayo ndiyo ule mradi umepita, Kata ya Tegeruka. Jamani changamoto ya pale ni mabomba. Ninaomba mradi ule mabomba yapelekwe ili Kata na vijiji vile ambavyo viko pale viweze kupata maji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru, ninaunga mkono hoja. (Makofi)