Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Ilemela
Contributions
nil
Answers
nil
Commettees
1
Ministries
nil
MHE. KAFITI W. KAFITI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nimshukuru sana Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema, kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia bajeti hii kutoka kwa Wizara hii ya muhimu sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, kwa niaba ya wananchi wangu wa Jimbo la Ilemela, kwanza kabisa nitoe pongezi sana kwa Rais wetu mpendwa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa mchango wake mkubwa kwa kuhakikisha anamtua mama ndoo. Ninadhani wote ni mashahidi, Mheshimiwa Rais wakati anaingia alisema moja ya ahadi yake kubwa ni kuhakikisha anamtua mama ndoo na hili limedhihirisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi pamoja na wananchi wangu wa Jimbo la Ilemela kiukweli tulikuwa kwenye wakati mgumu, ukiona mtu anaulizia maji ya Ziwa Victoria na wewe upo hapo hapo, lakini hupati maji ilikuwa ni changamoto kubwa. Leo nimpongeze sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa sababu sasa Ilemela inakwenda kung’ara, Ilemela inakwenda kuwa na maji ya uhakika. Kwa hiyo, nimpongeze sana Ndugu yangu, Mheshimiwa Aweso amefanya kazi nzuri sana yeye na wasaidizi wake; Mheshimiwa Kundo na Wizara nzima kwa kweli wanajituma. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii kutoa pongezi kwa dada yangu Nelly wa MWAUWASA anafanya kazi kubwa sana. Kwa hiyo, ninaomba sana kwa nafasi hii niliyopata nitoe pongezi kubwa kwa Wizara hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunafahamu maji ni uhai lakini bila maji binadamu yeyote hawezi kuwa hai na ndiyo maana tunaamini kwamba suala la uwepo wa maji ni suala la muhimu sana katika jamii yetu. Kwa hiyo, nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri, chanzo chetu cha Capri Point amekwenda kukipanua kutoka lita milioni 90 mpaka lita milioni 144, pongezi sana kwa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Mheshimiwa Mwenyekiti, unaweza ukaona Ilemela tulikuwa tuna shida kubwa sana ya maji, lakini kutokana na upanuzi huu wanaokwenda kuufanya katika chanzo chetu cha Capri Point, Wilaya sasa ya Ilemela tunakwenda kuondokana na tatizo la maji. Ninampongeza, mkandarasi aliniambia zaidi ya shilingi bilioni 4.5 tayari zipo Ilemela mkandarasi anaendelea na utekelezaji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo bado ameendelea kusambaza mabomba. Tunafahamu kipindi cha nyuma Ilemela iliendelea kuwa na changamoto kubwa ya maji, lakini ninaamini kwa uwepo wako kwa bajeti na pesa ambazo tunakwenda kumuidhinishia Ilemela sasa tunakwenda kuwa salama katika eneo zima la maji. Ninamwomba sana Mheshimiwa Waziri, bajeti hii ni bajeti kubwa, lakini tumeweza kuangalia hapa bajeti hii kwa mapato ya ndani ni ya zaidi 30%. Sasa nimwombe kama hatutaongeza bajeti hii kwa kutumia vyanzo vya ndani nina mashaka utekelezaji wa bajeti hii. Kwa hiyo, niombe sana Mwenyezi Mungu aendelee kumtia nguvu atafute pesa nyingi zaidi kuweza kutekeleza hii miradi ambayo Watanzania wanaitegemea. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo, sisi watu wa Ilemela tunashukuru ametuletea ule mpango wa maji taka kwa wakazi wale wa mlimani, ametupa zaidi ya shilingi 22,000,000,000 kwa ajili ya wakazi wa Lumala, Kiseke pamoja na Pasiansi. Hilo nimpongeze sana kwa sababu tulikuwa tunapata shida, wakati wa mvua tunasema tunafungulia koki watu wa mlimani, sasa Waziri amekwenda kuboresha maisha ya wakazi wa Jimbo la Ilemela, hilo nimpongeze sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba vilevile nimwambie tu na niendelee kumtia moyo, tunafahamu Idara hii wengi tulikuwa tunalia na kubambikizwa bili za maji lakini sasa unakuja kwako na mpango wa smart meter. Maana yake ni kwamba tatizo la kubambikwa bili za maji linakwenda kuwa historia. Kwenye hilo ninampongeza sana Waziri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, unaona wenzetu wa TANESCO sasa hatulalamiki kubambikiwa bili, kwa sababu sasa wameturahisishia. Kwa hiyo, katika eneo la maji, nimwombe sana Waziri aendelee kuweka mkazo huu wananchi waweze kufurahia huduma ya maji wanayoyapata bila kuwa na ubambikiwaji bili. Umbambikaji wa bili umeleta chuki kwa Serikali, umeleta chuki kwa wananchi, umeleta chuki kwa viongozi, kwa hiyo kupitia usimamizi wake tunaamini suala hili linakwenda kwisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba niendelee kuelezea suala lingine la upotevu wa maji. Tumekuwa tunapambana kwa kiwango kikubwa sana kuhakikisha kwamba tunaongeza speed ya usambazaji wa maji, lakini sijaona mikakati ya kudhibiti upotevu wa maji. Tumeona taasisi kama DAWASA inapoteza maji mengi sana, taasisi kama MWAUWASA inapoteza idadi kubwa ya maji. Kwa hiyo, hii ni hasara kwa Serikali, ni hasara kwa wananchi na inaongeza gharama kwa Serikali, kwa hiyo niendelee kumwomba Mheshimiwa Waziri katika eneo hili tuendelee kulipa mkazo mkubwa sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kingine ni lazima tuwe sasa na mpango, tunasema tuwe na water budget kwa kumalizia. Ni lazima tujue mahitaji yetu ya maji ni kiasi gani, matumizi yetu ni kiasi gani. Kwa historia tunaambiwa kwamba Ziwa Victoria lilishawahi kukauka miaka 400,000 iliyopita. Sasa sisi tumejipangaje katika hili? Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri niendelee kumpongeza Waziri, tupo tayari kuhakikisha tunapitisha bajeti yako ili kuleta ustawi wa maisha bora ya watu wa Ilemela.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa nafasi hiyo na ninaunga mkono hoja. (Makofi)