Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

Hon. Dr. Lazaro Killiani Komba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Peramiho

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

MHE. DKT. LAZARO K. KOMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana kwa kunipatia nafasi niweze kuchangia katika hotuba hii ya Bajeti ya Wizara ya Maji. Ninaanza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa zawadi hii ya uhai na afya njema aliyonipatia iliyoniwezesha kupata kibali cha kusimama hapa kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Peraminho, ambao kimsingi wamenituma nije nizungumze habari ya maji katika vijiji vyao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mama yetu kipenzi cha Watanzania, kwa kazi kubwa aliyoifanya katika Jimbo la Peramiho. Miaka mitano iliyopita sisi wananchi wa Jimbo la Peraminho tulikuwa tunapata maji kwa 67.7%, lakini leo tunavyozungumza mpaka sasa tumefika 79.3%. Haya ni mafanikio makubwa na tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Jimbo la Peramiho wana utamaduni wa kushukuru, lakini huwa wanaamini kushukuru ni kuomba tena. Sisi tunaomba tena katika maeneo matatu; eneo la kwanza, tunaomba miradi ile ambayo tayari ilikuwa imepatiwa fedha zaidi ya shilingi 4,451,000,000 ilianza utekelezaji na iko katika vijiji sita, lakini imesimama kwa sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaiomba Serikali na kwa bahati nzuri ndugu yangu Mheshimiwa Waziri yuko hapa ananisikia. Miradi iliyoko katika Kijiji cha Mpandangindo, Kijiji cha Makwaya, Kijiji cha Maleta, Kijiji cha Liweta na Kijiji cha Mdunduwaro, maeneo haya yamekuwa na changamoto kwa muda mrefu, lakini ipo miradi ambayo utekelezaji wake ulikuwa umesogeasogea kwa kiwango kikubwa, ukiwemo wa Kijiji cha Kitulo. Ninaomba sana, Mheshimiwa Waziri, Serikali iweze kutupatia katika bajeti hii fedha iliyobaki, ili kukamilisha, maji yaliyo safi na salama yaweze kupatikana kwa wananchi takribani 17,565 katika vijiji hivi sita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, viko vijiji viwili vilivyokuwa na miradi ya maji. Miradi ile chakavu kwa sababu, vijiji hivi vipo tangu mwaka 1960 na miradi hii ilikuwepo tangu wakati huo, kabla hatujapata uhuru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kiko Kijiji cha Mpitimbi A na kiko Kijiji cha Magazini. Vijiji hivi idadi ya watu imeongezeka, imekuwa kubwa sana. Ninaomba sana sasa Wizara yetu ya Maji itusaidie kufanya ukarabati katika maeneo haya ili wananchi hawa waweze kupata maji yaliyo safi na salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninasema tu ninakushukuru sana kwa nafasi na ninaunga mkono hoja. (Makofi)