Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Mbulu Vijijini
Contributions
nil
Answers
nil
Commettees
1
Ministries
nil
MHE. DKT. EMANUEL Q. NUWAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia bajeti ya Wizara ya Maji. Awali ya yote, nitoe pongezi kwa Mheshimiwa Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa jinsi ambavyo anaendelea kuwezesha Wizara yetu ya Maji kupata bajeti nzuri ili kuweza kutekeleza miradi ya maji. Vilevile, nimpongeze Mheshimiwa Waziri na Naibu wake pamoja na timu nzima ya Wizara kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya katika kuhakikisha kwamba tunamtua mama ndoo na tunawatua ndoo Watanzania wa maeneo ya vijijini na mijini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nipende kumpongeza pia Meneja wangu wa RUWASA mkoa, lakini pia na wilaya kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya katika kuhakikisha kwamba wananchi wa Jimbo la Mbulu Vijijini wanapata maji safi na salama. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda kuipongeza Wizara kwa maono ambayo hasa yametokana na Mheshimiwa Rais ya kuanzisha Gridi ya Taifa ya Maji. Katika hili tuna uhakika kwamba mahitaji yetu ya maji, ambayo ni takribani cubic meter bilioni 42 ambayo ni sawa na 37% ya maji safi na salama yaliyoko chini ya ardhi, lakini pia na juu ya uso wa ardhi; ambayo kwa kweli tuna uwezo isipokuwa tunachohitaji ni miundombinu na hasa usambazaji na kikubwa ikiwa ni bajeti lakini pia na mpango. Kwa hiyo, ninaomba niitie moyo Wizara kushikilia jambo hili na kulitekeleza kikamilifu. Hata kama itachukua miaka ya kutosha, lakini tuweze kuiona ikitekelezeka. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba niishukuru Wizara kwa miradi ya maji ambayo imeweza kuletwa katika Jimbo la Mbulu Vijijini, lakini miradi mingi bado haijakamilika. Niiombe Wizara ikamilishe miradi hii. Hasa nitangulize kwa kutaja Mradi wa Dambia ambao utahudumia vijiji 21. Mheshimiwa Waziri ametutengea 500,000,000 lakini hadi sasa mkandarasi anadai takribani bilioni 1.7.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli nilitamani nishike shilingi yake, ila kwa kuwa ameongeza bajeti ninaomba nisiishike shilingi yake wala mshahara wake. Ninaomba akamilishe lile deni, tupate na bilioni hizo ili mradi ule uweze kukamilika kwa ajili ya kuhudumia Kata za Bashay, Endamilay, Eshkesh, Dongobesh na Idachini, zikiwa ni vijiji 21. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli nipende kushukuru pia Vijiji vya Laghangesh, Mangisa, Getesh, Esqaroda, Gitultaqao; lakini pia Multuru, Diomat na Endagao vitapata maji. Kwa kweli nipende kuleta shukurani za dhati kutoka wananchi hawa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe Wizara ipeleke fedha hizi ili miradi hii iweze kukamilika na wananchi waweze kupata maji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilete maombi machache kwa ajili ya wananchi wa Jimbo la Mbulu Vijijini. Tuna Kata ya Masyeda ambayo ina Kijiji cha Endanyawish. Ni kijiji kikubwa sana ambacho kina wakulima na wafugaji. Tumechimba takribani visima vitano lakini havina maji. Ninaomba Mheshimiwa Waziri aitazame kata hii na kijiji hiki ili kiweze kupata maji. Tuna maji katika Bonde la Endagichan ambayo ni kata, tunaweza tukayachimba na kupeleka kule. Ninaomba nilete ombi hilo rasmi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mji wa Dongobesh ambayo ni makao makuu ya halmashauri tuna maji ambayo ni machafu kutokana na kutokuwa na chujio na pia bado hayatoshelezi mahitaji ya mji. Niiombe Wizara itusaidie bajeti ili tuweze kupata chujio ili wananchi takribani 20,000 wanaokaa katika Mji wa Dongobesh wapate maji safi na salama.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niishukuru pia Wizara kwa kukubali kuongeza upatikanaji wa maji kwenye mji huu kwa kuleta maji kutoka Mradi wa Dambia na hivyo ninaamini ndani ya miezi mitatu ijayo wananchi wa Dongobesh wataweza kushukuru kupata maji na kubaki salama katika mji huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna Kata ya Maghan ambayo ina chanzo cha maji kilichochimbwa mwaka 1975, wakati huo ikiwa na wakazi kama 500, leo tuna wakazi 15,000 na bado inategemea chanzo hiko kimoja. Niombe tuweze kupata chanzo kingine. Kwa bahati nzuri kata hii ina bonde zuri sana ambalo lina maji mengi. Tukipata visima viwili tayari wananchi hawa ambao ni takribani 15,000 watakuwa wamepata maji safi na salama.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna miradi ya mabwawa. Jimbo langu hili lina takribani kata tano, ambazo Mheshimiwa Waziri akitutengea bajeti maeneo yapo ya kuchimba mabwawa na kuyatengeneza ili wananchi waweze kupata maji. Ninaomba Kata za Masqaroda, Maghang, Gidhim, Eshkesh, Haydom, Masonyagwe, Labay, pamoja na Basoderer wachimbiwe mabwawa ili wapate maji safi na salama kwa ajili ya nyumbani na mifugo yao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nikushukuru sana na ninaomba kuunga mkono hoja kwa asilimia mia moja kwa ajili ya wananchi wetu kupata maji safi na salama. Ahsanteni sana. (Makofi)