MHE. SAIDI SALIM HAMAD aliuliza: -
Je, Serikali ina mpango gani wa kukuza na kuhifadhi Miti ya Mikoko ili kukabiliana na mabadiliko ya Tabianchi?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI K.n.y. WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA alijibu: -
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, ninaomba kujibu swali namba 172 la Mheshimiwa Saidi Salim Hamad kama ifuatavyo: -
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeendelea kuchukua hatua mbalimbali katika kukuza na kuimarisha uhifadhi wa mifumo-ikolojia ya mikoko nchini ili kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi. Hatua hizo ni pamoja na: -
(1) Kuweka misitu ya mikoko katika mojawapo ya maeneo ya vipaumbele vya uzalishaji wa viwango vya Kaboni ili kuwezesha jamii za pwani kunufaika na biashara ya kaboni;
(2) Kuwezesha jamii za pwani kutekeleza miradi na shughuli mbadala za kiuchumi ikiwemo ufugaji nyuki, kilimo cha mwani, uvuvi endelevu, ufugaji/uboreshaji wa kaa ili kupunguza utegemezi wa jamii kwenye misitu ya mikoko;
(3) Kuhamasisha upandaji na urejeshaji wa mikoko ili kuhifadhi mifumo ikolojia ya misitu ya mikoko; na
(4) Kujenga uwezo wa Kamati za Uhifadhi za Mazingira na vikundi vya usimamizi wa maeneo ya fukwe ili kuongeza usimamizi na utekelezaji wa Sheria zinazosimamia rasilimali za pwani na bahari.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba kuwasilisha.