MHE. IBRAHIM M. SHAYO: Mheshimiwa Naibu Spika, ninashukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Mheshimiwa Naibu Waziri, Moshi ni Mji ambao ulikuwa na viwanda vingi sana, lakini viwanda vile sasa hivi vimekufa na vimechukuliwa na wawekezaji na wale wawekezaji hawawekezi wamevichukua tu kama magofu. Ni lini Serikali itaweza kuwanyang’anya viwanda vile na kuvifanyia kazi?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ilivitoa viwanda hivi kwa wawekezaji kwa nia ya uzalishaji. Mkataba wa makabidhiano wa viwanda hivi kwa hao wawekezaji unawataka wauheshimu kwa maana ya kuendelea na shughuli za uzalishaji. Ndiyo maana kwa Moshi kuna Kiwanda cha Kilimanjaro Machine Tools ambacho mimi mwenyewe nilikuwa pale wiki mbili zilizopita kazi za uzalishaji inaendelea.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maeneo mengine ambayo wawekezaji wamepewa viwanda hivi na havizalishi, rai yetu ni moja tu kuwaambia kwamba, aidha warudi kwenye uzalishaji ama Serikali itachukua hatua ya kuwapatia viwanda hivyo wawekezaji ambao wana nia ya dhati ya kushiriki katika ujenzi wa Dira ya 2050 kwenye Uchumi wa Viwanda na Uzalishaji kwa ajili ya shughuli ya kuongeza mnyororo wa thamani wa mazao yetu.