Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Happiness Daniel Ngwando (1 total)

Mpango Elekezi wa Maendeleo wa Muda Mrefu 2026/2027–2050/2051, Mapendekezo ya Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2026/2027–2030/2031 na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Mwaka 2026/2027; na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali Katika Muda wa Kati ya 2026/2027 hadi 2028/2029.
MHE. HAPPINESS D. NGWANDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii. Awali ya yote, napenda kumshukuru Mungu kwa kuniwezesha kuwa mahali hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza kusimama kwenye Bunge lako Tukufu, ninapenda kumshukuru sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kuniteua kuwa mwakilishi wa wanawake wa Mkoa wa Ruvuma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna ya kipekee sana niwashukuru wanawake wa Mkoa wa Ruvuma kwa kunichagua kwa kura zao ili niweze kuwawakilisha katika Bunge hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, pamoja na Mheshimiwa Dkt. Emmanuel Nchimbi, Makamu wa Rais, kwa kuchaguliwa kwa kura nyingi za kishindo Oktoba 29. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nipo hapa leo niseme mawili matatu ambayo Rais wetu ametufanyia. Kama inavyosemwa mara zote, moyo usio na shukrani hukausha mema. Sisi wanawake wa Mkoa wa Ruvuma, Mheshimiwa Rais ametufanyia mengi sana ndani ya miaka minne iliyopita toka aingie madarakani ametupa zahanati, vituo vya afya, kwenye sekta ya elimu, maji na hapa nitapenda niseme vichache tu ambavyo wajue kwamba Mheshimiwa Rais anafanya kazi sio tukisema tunasema hewani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais ametupatia Halmashauri ya Mbinga Vijijini, hospitali ya wanawake yenye thamani ya shilingi bilioni 2.9; zahanati 17 zenye thamani ya shilingi bilioni 1.7; vituo vya afya vitano vyenye thamani ya shilingi bilioni 2.7; vituo vya afya kule Wilaya ya Tunduru; Kituo cha Malumba kinaendelea na kazi, Kituo cha Afya cha Kata ya Mbaa Wilaya ya Nyasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye sekta ya maji ametupatia vitu vingi. Kwa kuwa mimi ni kiungo mchezeshaji namba sita nitataja wilaya zote ambazo amefanya vitu hivi kwa macho. Mheshimiwa Rais alitupa shilingi milioni 900 Hospitali ya Wilaya ya Mbinga ambayo kwa kweli ile hospitali ni kongwe alitupa tufanye ukarabati wa hospitali ile. Tuliweza kufanikisha kutengeneza OPD, emergency nzuri sana ipo pale, tulitengeneza theatre, tukatengeneza na maabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo hivyo alitoa fedha hospitali ya Wilaya ya Tunduru, shilingi milioni 900, tulitengeneza OPD nzuri sana, tukatengeneza theatre. Siku zote wanasema ukisema ahsante maana yake unaomba tena.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mazuri haya, bado niwakumbushe kwenye bajeti ambayo itakuja tunahitaji au tunaomba mtujengee wodi za akinamama (maternity ward) kwa kuwa hospitali hizi ni kongwe na zinapokea wamama wengi sana. Kwa mwezi wanajifungua wanawake takribani 400 - 500 kwa Tunduru, lakini pia wanajifungua akinamama 700 - 1,000 kwa Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga Mjini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende moja kwa moja kwenye suala la maji. Ninamaanisha kwamba tunaposema uzalishaji na mpango wa ukuwaji wa uchumi kwa jamii, tunaangalia zaidi afya ya watu hawa. Jamii ikikosa afya, ikikosa huduma za jamii maana yake uchumi huu hautakua. Ndiyo maana nimempa hongera nyingi Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kukumbuka kuwa uchumi unaendana na afya ya jamii na mazingira mazuri. Tunasema ahsante sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Mheshimiwa Rais bado anajua unapotakiwa kuwa na uchumi mwanamke anatakiwa asikae bombani au asitafute maji masaa manne hadi matano ameendelea kutupatia maji Wilaya ya Mbinga shilingi bilioni 4.6. Pia amekwenda kutupatia mradi mkubwa wa maji Halmashauri ya Tunduru shilingi bilioni 3.4, tunasema ahsante sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hapa sasa ningeomba nijielekeze kwenye ushauri wa mpango na sera wa mwaka 2027/2028. Kwanza ninapenda kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu pamoja na Mawaziri mwenye dhamana walipotuambia kuhusu suala la wanaopata kazi wasihame kwenye maeneo yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hili ninapenda kuishauri Serikali, niseme kuwa kama Mheshimiwa Waziri Mkuu alivyosema kuwa inatakiwa watu wasihame, tunaomba iwekwe sheria ili kuilinda kauli za viongozi walizosema zitekelezwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano watu wakienda kuripoti kwenye vituo vyao, unakuta kuna wakati wanakuja na barua moja kwa moja wanasema wasainiwe ili wahame. Tunaomba, kuwalinda Wakurugenzi na watu wenye mamlaka husika basi waweke sheria ambayo ita-cement hii kauli ya kuwa watu wasihame ili watu wetu waendelee kupata huduma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ninaomba nishauri jambo lingine kwenye suala la elimu. Tunasema hawa watu wanaopelekwa kwenye vijiji mbalimbali, wanaokwenda kufanya kazi, ajira za vijijini, ningependa kushauri tuwape motivation, kwani kijijini kuna mazingira fulani ambayo sisi wote tunayafahamu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tungetamani sana waajiriwa hawa wanaokwenda vijijini wapewe motisha. Kwa mfano, tuna ile Mei Mosi ambayo inasema, mtu Mei Mosi ndiyo anatambulika. Asitambulike Mei Mosi peke yake, kuwe na utaratibu, idara husika kama ni walimu, kama ni afya, waishi kule wakiwa wanajua wanajaliwa na wanapendwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama mtu akifanya vizuri, labda tunasema anunuliwe bati, labda atakayefanya vizuri atanunuliwa hiki, itamfanya yule mtu aone kuwa inawezekana kubaki pale. Kama Mheshimiwa Rais alivyoanzisha kuanza kuwatengenezea nyumba zaidi ya 70 kwenye maeneo yao, na sisi kama watendaji na wataalam na Serikali, tuwape motivation hawa watu badala ya kuona tu kuwa wanakosea wapi? Kwa nini wanataka kuhama? Tuwatengenezee mazingira ya wao kupenda kukaa kwenye maeneo yao ya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikifika hapo, ninaunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)