MHE. HIJA HASSAN HIJA aliuliza:-
Je, lini Serikali itapeleka vifaa tiba vya kutosha, hususan vifaa vya kujifungulia, katika hospitali zote nchini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. RAJAB S. JAFAR) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kwa kumshukuru Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuniteua kuwa Naibu Waziri ninayeshughulikia masuala ya afya, TAMISEMI. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, TAMISEMI, ninapenda kujibu swali la Mheshimiwa Hija Hassan Hija, Mbunge wa Kiwani.
Mheshimiwa Spika, Serikali imekuwa ikitenga fedha, kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba kwenye vituo vya kutolea huduma za afya ya msingi vinavyoendelea kujengwa kote nchini. Aidha, katika kipindi cha miaka mitano, 2021/2022 hadi 2024/2025, Serikali imetoa jumla ya shilingi bilioni 285.6, kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba vikiwemo vifaa vya kujifungulia kwenye vituo vya kutolea huduma za afya ngazi ya msingi.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka wa Fedha 2025/2026 shilingi bilioni 32 imetolewa, kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba kwenye vituo vya kutolea huduma za afya, ngazi ya msingi. Shilingi bilioni 9.6 imetolewa, kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba katika hospitali za halmashauri kote nchini.