MHE. SAASHISHA E. MAFUWE aliuliza:-
Je, lini Serikali itakarabati Kituo cha Afya Masama pamoja na nyumba za watumishi wa Kituo hicho?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. JAFAR R. SEIF) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, TAMISEMI, ninaomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge Saashisha kutoka Jimbo la Hai.
Mheshimiwa Naibu Spika, Kituo cha Afya cha Masama kilijengwa Mwaka 1979, hali inayosababisha kuwa na miundombinu michache na chakavu. Kituo hicho kinahitaji miundombinu muhimu, ikiwa ni pamoja na jengo la huduma za wagonjwa wa nje (OPD), maabara, jengo la huduma za uzazi, jengo la upasuaji, jengo la kufulia, kichomea taka, vyoo vya nje na nyumba za watumishi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imefanya tathmini na kuainisha vituo vya afya kongwe 532 kote nchini, ambavyo vinahitaji kuongezewa na kukarabatiwa miundombinu yake. Aidha, jumla ya shilingi bilioni 102.08 zinahitajika, kwa ajili ya uboreshaji wa vituo hivyo. Serikali itaendelea kutenga fedha, kwa ajili ya ukarabati wa vituo vya afya kongwe kote nchini, kikiwemo Kituo cha Afya Masama. (Makofi)