Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Nyamizi Simon Mhoja (1 total)

Mpango Elekezi wa Maendeleo wa Muda Mrefu 2026/2027–2050/2051, Mapendekezo ya Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2026/2027–2030/2031 na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Mwaka 2026/2027; na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali Katika Muda wa Kati ya 2026/2027 hadi 2028/2029.
MHE. NYAMIZI S. MHOJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa fursa hii. kwanza ninamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya njema siku hii ya leo. Kingine nitoe pole kwa Chama Cha Mapinduzi hasa Wanatabora kwa kuondokewa na aliyekuwa Mjumbe wa Halmashauri kuu ya CCM Taifa Mzee Nassoro Hamdani na mpendwa wetu Dada Munde Tambwe, Mbunge Mstaafu, Viti Maalum, Mkoa wa Tabora, wapumzike kwa amani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi watu wenye ulemavu kwenye Dira ya Taifa ambayo iko mezani inajadiliwa tunamshukuru sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kuweza kutujumuisha katika dira hii. Dira inaelekeza kuwa na Taifa jumuishi lenye ustawi haki na linalojitegemea. Nitajikita katika mambo mawili; uchumi imara jumuishi na shindani, lakini pia maisha bora na ustawi kwa wote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunamshukuru Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kutujali sana sisi watu wenye ulemavu, si tu kutujali yaani anaonyesha utu na sisi wote ni mashahidi. Nikianza kwenye masuala ya afya, watoto chini ya miaka mitano. Ukienda kwenye field ya kawaida watoto wanatibiwa bure chini ya miaka mitano. Hata hivyo, ninaiomba Wizara, kuna watoto wa usonji na watoto wenye vichwa vikubwa, hawa watoto wasiishie tu miaka mitano waendelee kupata huduma mpaka pale watakapokaa sawa, nina imani hili liko ndani ya uwezo wa Wizara ya Afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo kuna ulemavu wa afya ya akili, hawa watu wanahitaji dawa maisha yao yote, ninaomba zitolewe bure ili kujenga jamii jumuishi kama dira inavyotuelekeza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, si hivyo tu, tunaishukuru Ofisi ya Waziri Mkuu kwa sisi watu wenye ulemavu kuendelea kuwa chini ya Waziri Mkuu, inamaanisha mambo yetu wenye ulemavu ni mambo mtambuka yana-cut across kwenye kila Wizara. Kwa hiyo, Waziri Mkuu ana uwezo wa kutoa maelekezo katika Wizara tofauti tofauti ili kuleta maendeleo jumuishi kwa watu wenye ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hii Awamu ya Sita tunamshukuru Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kitendo cha kuboresha vyuo vya ufundi kwa watu wenye ulemavu na hii ni namna ya kupambana na ajira kwa vijana wenye ulemavu. Ninaomba nivitaje hivi vyuo viko 10 vingine vimekarabatiwa na kutengenezwa, vingine vimejengwa upya chini ya Mfuko wa Watu Wenye Ulemavu ambao uko chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge na Wenye Ulemavu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vyuo hivyo ninaomba nivitaje wananchi wavielewe ili waweze kuwapeleka vijana wao kwa ajili ya maendeleo ya vijana, kuzalisha ajira na vijana pia watajiajiri. Vyuo hivyo kuna Chuo cha Rwanzari, mkoani Tabora; Chuo kiko Milongo, Mwanza; Chuo cha Masiwani, Tanga na Mtapika, Masasi, Mtwara. Chuo cha Ufundi, hivi vya watu wenye ulemavu Sabasaba, Singida; Yombo, Dar es Salaam; Ruvuma; Mbozi, Songwe; Kasulu, Kigoma; na Kisesa, Mwanza. Hivi vyuo ni vya watu wenye ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba Wizara ya Elimu hili suala lichukuliwe kama emergence, kuna Chuo mfano kile cha Rwanzari havina mkalimani wa lugha ya alama ambapo wanafunzi wenye uziwi wanakosa mawasiliano kati ya mwalimu na mwanafunzi. Kwa hiyo, ninaomba tuangalie namna ya kupeleka wakalimani, hiyo Rwanzali nimetolea tu mfano kwa sababu nimekitembelea, lakini sijajua hivi vyuo vingine pia Wizara wanaweza wakachukua muda kuvitembelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, kwenye Wizara ya Uchukuzi sisi watu wenye ulemavu ninaomba tuondoe mentality kwamba tunapenda kusaidiwa, hapana. Sisi tuondolewe vikwazo ili tuweze kupambana katika maendeleo, kwa sababu kuwa mwenye ulemavu hakuniondolei kwamba nitakuwa na nchi yangu peke yangu, hapana. Huduma wanazozipata watu wengine na sisi tunaenda huko huko. Kama kwenye mabasi tunapanda na sisi tunapanda huko huko, hakuna jamii nyingine. Mfano, kuna usumbufu unaojitokeza kwa sisi watu wenye ulemavu kwenye Wizara ya Uchukuzi hasa SGR, vituo vya mwendo kasi, uwanja wa ndege na stendi za mabasi mfano pale kwa Magufuli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimetoka kusema kwamba na sisi ni wapambanaji tunachangia pato la Taifa, lakini kuna usumbufu ambao hauna hata, yaani usumbufu siyo wa lazima. Tumewekewa viti mwendo vile tumewekewa mazingira mazuri sawa mfano, pale kwenye SGR, lakini vile vitimwendo mimi mwenyewe ni shahidi unakaa pale nusu saa nzima saa nyingine unaletewa kitimwendo na vitimwendo vingi vimeharibika inamaanisha havifanyiwi service. Tunapotezewa muda katika hivi vituo. Huu ni usumbufu usio wa lazima. Ninaomba tusaidiwe kwa sababu tunapoteza muda mwingi na tunashindwa kuchangia maendeleo kama watu wengine. Tunapenda tufike kwa wakati twende katika maeneo yetu kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi watu wenye ulemavu tunahudumiwa na ustawi wa jamii kwa ngazi ya halmashauri na hiki kitengo cha ustawi wa jamii kinahudumia si watu wenye ulemavu tu, wanahudumia wazee, watoto wa mitaani, kutatua migogoro ya ndoa, yaani mambo mengi hii Wizara imeyabeba; inapitia changamoto nyingi. Sisi wenye ulemavu changamoto zetu wao ndiyo wanazifahamu. Hawa ndiyo wanaofahamu idadi ya wenye ulemavu kuanzia ngazi ya kata mpaka kwenye wilaya mpaka mkoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaiomba na kuishauri Wizara kama itapendeza iongeze idadi ya Maafisa Ustawi wa Jamii. Wawepo angalau kila kata, kwa sababu sasa hivi kazi ya ustawi wa jamii kwenye kata wanafanya pia Maafisa Maendeleo ya Jamii. Pia, ianzishwe Idara ya Ustawi wa Jamii kwenye kila Halmashauri. Kwa sasa muundo wa halmashauri hii ustawi wa jamii ni kitengo kiko chini ya Mganga Mkuu Wizara ya Afya kwenye ngazi ya halmashauri. Ndiyo maana tunakutana na changamoto utakuta vifaa saidizi hatuna, mafuta ya wenye ualbino hayatoshi kwa sababu hawana bajeti maalum ambayo inayowawezesha kutekeleza majukumu yao ipasavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba iwe idara katika ngazi ya halmashauri na ngazi ya mkoa. Itasaidia sana kutatua changamoto zetu wenye ulemavu na hii kama ikishindikana basi wazo la pili ni kwamba bajeti ya ustawi wa jamii kwa upande wa watu wenye ulemavu basi ipelekwe kwenye Wizara inayohusu watu wenye ulemavu ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge na Wenye Ulemavu ili mambo yetu yaweze kutatulika kule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumalizia ninahitimisha kwa kusema kwamba ukimpa mtu chakula kila siku. Leo umempa chakula na kesho unampa chakula, huyu unamtengeneza awe tegemezi maisha yake yote. Tukumbuke sisi watu wenye ulemavu kwenye sensa ya hivi karibuni tuko zaidi ya milioni tano ni sawa na 11.2% ya Watanzania wote. Kwa hiyo, tuangalie tusipoweka mikakati madhubuti ya kuondoa vikwazo kwa hili kundi la watu wenye ulemavu tunatengeneza Taifa kubwa ambalo ni tegemezi na tunavyoangalia kwamba dira yetu inasema tutengeneze jamii jumuishi na yenye kujitegemea. Kwa hiyo, ndugu zangu, Wizara hizi ziwasiliane juu ya namna ya kuondoa vikwazo ili tusitengeneze Taifa tegemezi katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaunga mkono hoja na ninaomba kuwasilisha, ahsante sana. (Makofi)