MHE. DKT. PAULINA D. NAHATO: Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri katika swali langu. Nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza. Kwa kuwa sasa hivi Serikali imeboresha sana TEHAMA katika vyuo vikuu. Je, imejipangaje kuwajumuisha wafanyakazi wa TEHAMA katika vyuo vikuu ambao sio wataaluma kushiriki katika kuboresha TEHAMA katika vyuo vikuu?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili. Vyuo vikuu vya umma nchini vinaendesha masomo ya masafa (distance learning) kwa wanafunzi walioko mikoa mbalimbali. Je, Serikali imejipangaje kuwasaidia wanafunzi hawa hasa katika upande wa TEHAMA? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, naomba kumpa taarifa Dkt. Nahato kwamba, Serikali tayari imeanza mkakati wa maboresho ya vyuo vikuu vyote nchini, kupitia mradi wetu mkubwa kabisa ujulikanao kama higher education for economic transformation ambao una mawanda karibu sita au maeneo sita ambayo yanafanyiwa kazi. Eneo la kwanza ni ujenzi wa miundombinu mbalimbali ya campus hizi zilizopo pamoja na campus mpya.
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili, ni kusomesha wahadhiri ndani pamoja na nje ya nchi; eneo la tatu, ni kutunga mitaala mipya pamoja na kuboresha ile mitaala iliyopo; eneo la nne, ni ushirikiano baina ya vyuo vyetu vikuu pamoja na viwanda; eneo la tano, ni uwezeshaji wa wenzetu wenye mahitaji maalum; na eneo la sita, ni hili eneo la TEHAMA.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, katika eneo la TEHAMA Serikali imejikita kufanya mambo yafuatayo ili kuboresha mazingira ya TEHAMA katika vyuo vyetu: ambapo eneo la kwanza, tutafanya upanuzi wa miundombinu mbalimbali ya internet kuhakikisha kwamba tunakuwa na smart classes, lakini tunakuwa na smart campus ambazo zitakuwa sasa zinawasiliana siyo tu ndani ya nchi, bali hata kufikia vyuo vingine katika nje ya nchi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili, ni kutengeneza mifumo sasa ya kidijitali ile ya kujifunzia na kusomea. Eneo lingine ni kutengeneza maktaba za kimtandao au maktaba za kidijitali ili kupata ile e-Learning kwa ujumla wake. Eneo la nne ni sasa hiyo elimu iliyozungumzwa kwa njia ya masafa, inazingatiwa kwenye eneo hili, lakini vilevile tunatengeneza sasa studio katika vyuo vyetu vyote vikuu ili kuweza kutengeneza vipindi ambavyo siyo lazima Mwalimu muda wote awepo darasani. Wanafunzi wanaweza ku-access kupitia maktaba zetu, lakini vilevile kuna ununuzi wa vifaa sasa kwa ajili ya kufanya mifumo hii iweze kufanya kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa mambo haya yote yanajumlisha vilevile watumishi wasio wanataaluma ili kuhakikisha kwamba mifumo hii inafanya kazi pamoja na kuwasomesha watumishi hawa wasio wanataaluma ili kuhakikisha mifumo ya TEHAMA inakwenda kufanya kazi sawasawa na kwenye vyuo vyetu. Ninakushukuru sana.