MHE. OMARY M. MSIGWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, nina swali moja la nyongeza. Mheshimiwa Waziri ninatamani kujua ni lini utatembelea Mradi huo wa Maji wa Mtyangimbole, Ngadinda na Gumbiro ambapo miradi hiyo imekamilika na maji yapo kwenye matanki isipokuwa hayajafika kwa wananchi na maji yanamwagika pale? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda kujibu swali la nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamshukuru sana Mheshimiwa Mbunge kwa ushirikiano mzuri ambao anaendelea kuutoa na ninamshukuru sana kwa kutupa taarifa nzuri za maendeleo ya miradi ndani ya Jimbo lake. Miradi hii imefikia hatua nzuri kabisa mpaka sasa Mradi wa Gumbiro upo 90%. Pia, Mradi wa Ngadinda upo 67%.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimtoe hofu Mheshimiwa Mbunge, Serikali tumejipanga, na mpaka sasa hatuna changamoto ya kifedha ndani ya miradi hii, na ndiyo maana upo katika hatua nzuri kabisa ya utekelezaji. Ninamtoa hofu Serikali ya Awamu ya Sita itaendelea kutekeleza hii miradi na kupeleka fedha ili iweze kukamilika kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge ameendelea kuomba. Ninakushukuru sana.
MHE. OMARY M. MSIGWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Barabara ya Wino - Matumbi iliyopo katika Jimbo langu la Madaba ni barabara muhimu kwa uwekezaji, lakini imekuwa ikijifunga kila wakati. Je, ni lini sasa Serikali itakwenda kuijenga kwa kiwango cha changarawe? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Msigwa amefuatilia kwa karibu sana kuhusiana na miundombinu ya barabara katika Jimbo la Madaba, nami nimhakikishie, yeye mwenyewe ameleta taarifa za uhitaji wa barabara na Meneja wake wa TARURA, ameleta na Ofisi ya Waziri Mkuu, tayari tumeanza utaratibu wa kutafuta fedha kwenda kutekeleza barabara hizo. (Makofi)