Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Mwantumu Mzamilu Zodo (2 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwa kunipa nafasi jioni hii ya leo. Kwanza kabisa ninaomba nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya njema na kuniwezesha kusimama hapa jioni ya leo. Pia, ninaomba nimshukuru Rais wangu, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambaye ni Mwenyekiti wetu wa Chama Cha Mapinduzi Taifa kwa kupitisha jina langu na hatimaye kuwa Mbunge. Kwa hiyo, ninaomba nimshukuru sana Dkt. Samia Suluhu Hassan pamoja na Wajumbe wote wa Kamati Kuu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya shukrani hizo sasa, ninaomba nimpongeze Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa dhamira yake ya dhati ya kutaka kuona kuwa sekta yetu ya kilimo inaendelea kusonga mbele. Dhamira hii ya dhati kwa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan inajidhihirisha kupitia bajeti za kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati wa kipindi cha bajeti ya 2021 bajeti yetu ya kilimo ilikuwa ni shilingi bilioni 294, lakini kipindi cha mwaka wa fedha 2024/2025, wakati wa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, bajeti hii tumeona imeongezeka kutoka zaidi ya shilingi bilioni 200 mpaka shilingi trilioni 1.2 na ushee. Hii ni wazi kuwa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ana dhamira ya dhati ya kutaka kuwakomboa wananchi kwenye kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati ninampongeza Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, nitakuwa mchoyo wa fadhila kama sitampongeza Waziri wetu wa Kilimo, ndugu yangu Mheshimiwa Chongolo. Wote tunamfahamu Mheshimiwa Chongolo ni mchapa kazi na ni mtu rahimu. Tunamfahamu ameongea sana hapa Kibajaji, alikuwa Katibu wetu wa Chama Taifa. Hii miradi hapa tunayoililia na mingine tunayoipigania yeye anaifahamu yote, kwa hiyo nimefurahi sana kuwekwa kwenye Wizara hii kwa sababu atakwenda kuisimamia vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata wakati Waziri Mkuu anahitimisha bajeti yake, Mheshimiwa Chongolo alisimama hapa akaongea. Kati ya mambo aliyoongea jambo mojawapo lililonifurahisha ni lile alilosema kuwa anakwenda kuweka nguvu kwenye uzalishaji wa mbegu na anakwenda kuziongezea zile taasisi bajeti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bila kuweka nguvu kwenye uzalishaji wa mbegu, hii bajeti yote na hizi jitihada za Mheshimiwa Rais zitakuwa ni kazi bure. Kwa sababu kipindi cha nyuma wakati wa 2021 uzalishaji wa mbegu ulikuwa ni takriban tani 30,167 lakini kipindi cha Mwaka wa Fedha 2025/2026 ambacho na Mheshimiwa Chongolo ndiyo amekuwa Waziri, wameanza kutekeleza hiyo bajeti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipindi hiki ambacho sisi tumekuwa hapa uzalishaji wa mbegu umeongezeka kutoka tani 30,000 mpaka tani 54,000. Kati ya hizo tani 54,000, tani 47,000 zinazalishwa na sekta binafsi na tani 7,000 zinazalishwa na taasisi yetu ya mbegu ya ASA. Tafsiri yake ni nini? Tafsiri yake ni kuwaongezea nguvu hawa wazalishaji binafsi wa mbegu ili tuweze kusogea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bila kuwapa nguvu hatuwezi kupata uhakika wa mbegu. Ninamwomba kaka yangu, Mheshimiwa Chongolo tunaweka nguvu kwenye uzalishaji. Nilimsikia hapa asubuhi amesema kuhusu miundombinu. Kuna baadhi ya mashamba yana miundombinu, lakini mengi hayana. Twende tukaboreshe miundombinu kwenye mashamba yetu ya mbegu ili yaweze kuzalisha mbegu mwaka mzima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tusipoboresha miundombinu wakulima watategemea mvua, mashamba ya mbegu yatategemea mvua, mvua isiponyesha mashamba ya mbegu hayatazalisha, wakulima hawatakuwa na mbegu. Ninaomba twende pia tukaweke nguvu kwenye miundombinu, tukaongeze spidi kwenye miundombinu ya haya mashamba. Wakati huo tunapambana na miradi hii ya umwagiliaji kwenye majimbo yetu, lakini tuyaangalie na mashamba haya ya mbegu kuendelea kuweka miundombinu ili tupate uhakika wa mbegu bora. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo la mbegu ni tatizo kubwa. Nilishuhudia mwaka huu 2026 ambao wakulima ndiyo wanasubiri kuvuna hapa Dodoma, Kata ya Itiso kwa kaka yangu Deo, wakulima walipanda mbegu zao za alizeti, walikuwa wamenunua kwa mdau mmoja Manyara, mbegu zile hazikuota zote. Walirudia kupanda tena mara ya pili. Hata akitaka idadi ya wakulima wale, wenye uwezo walirudia kupanda, ambao hawana uwezo hawakurudia, kwa hiyo wakulima walipata hasara. Kwa hiyo, sina mashaka na Waziri na nilipata nguvu sana baada ya kusikia anakwenda kuweka nguvu kwenye uzalishaji wa mbegu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri akienda kuweka nguvu kwenye eneo hili dhamira ya Mheshimiwa Rais itafikia malengo, lakini bila kuwa na mbegu za uhakika hatutakuwa na mazao ya uhakika na ziada ya chakula. Wakulima wetu wanategemea ziada ya chakula kama kipato chao. Wanalima ili kupata chakula, lakini wanalima ili kufanya biashara wapate pesa. Kwa hiyo, ninamwomba sana Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kule Mkoani kwetu Tanga tuna zao la mkonge. Ninaipongeza sana Wizara wanafanya vizuri, lakini changamoto ndogo ni wakulima wale wadogo wadogo wanapata tabu na zile korona. Hakuna korona za kutosha za kuchakata mkonge. Wakati mwingine mkonge wao unaharibika unakuta umeshakomaa, yule mnunuaji mkubwa haendi kununua kule, kwa hiyo hiyo ni changamoto kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati mwingine nimeona, mara nyingi, mashamba mengi ya mkonge yanaungua…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa kwa mchango wako.

MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo langu la mwisho. Mheshimiwa Waziri ajaribu kutuangalia kule Tanga kwenye zao letu lile la machungwa. Ajaribu kutuangalia sana, atupelekee kiwanda kule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana na ninaomba kuunga mkono hoja ya Wizara hii ya Kilimo. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa, ninaomba nimshukuru Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa dhamira yake ya dhati ya kutaka kumtua mwanamke ndoo kichwani, na dhamira hiyo tunaiona. Ninaomba nimpongeze Mheshimiwa Waziri pamoja na timu yake yote, akiwepo Katibu Mkuu, dada yangu Mwajuma, kwa kweli tunawaona Wizara hii wanavyokimbizana, na wote ni mashahidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa muda ni mfupi sana leo, ninaomba niende moja kwa moja tu kwenye miradi michache, ambayo ninataka kuiongelea, hasa ya mkoa wetu wa Tanga. Sisi kwenye Mkoa wetu wa Tanga, mradi mkubwa ambao unaenda kuwa mkombozi wa maeneo mengi, ni ule mradi wa miji 28.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kwenye mkoa wetu, maeneo ambayo yana changamoto kubwa za maji hasa, ni Kilindi, Handeni, Muheza na Korogwe. Kupitia mradi huu wa miji 28, ambao sasa hivi uko takribani 77% unaenda kuwa mkombozi kwa maeneo haya niliyoyataja, mpaka kwenye Jimbo lile la Mheshimiwa Waziri, Pangani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaiomba Wizara kuongeza nguvu kwenye mradi huu. Mradi huu upo katika hatua nzuri, kubwa zaidi ni fedha. Wote tutakuwa mashahidi, tangu jana kila mtu anayesimama hapa kuongea, na ndiyo maana nikasema nianze kumshukuru Mheshimiwa Rais, kwani kila mtu kwenye jimbo lake kuna mradi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, kuna mradi umekamilika au kuna mradi unaendelea, lakini miradi ipo inatekelezwa. Tutakuwa mashahidi wote, kwa Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri, pamoja na timu yake yote ya Wizara, tunawaona kwanza wanavyokimbizana, pili ni wasikivu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto kubwa iliyopo hapa ni upatikanaji wa fedha. Tuiombe Serikali ipeleke fedha kwenye miradi hii ya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimemwona hapa Mkurugenzi wa Mfuko ule wa Maji, tukaongeze nguvu kwenye mfuko huu. Niwaombe Wizara ya Fedha tuongeze nguvu kwenye Mfuko wa Maji, tukaongeze hata shilingi 50 tu. Mfuko huu utakwenda kutusaidia, kwa sababu moja ya kazi za mfuko huu pia unasaidia kutatua ile miradi chechefu, ile ambayo imekwama. Mfano mzuri ni ule Mradi wa Same - Mwanga - Korogwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi ule umeenda kukamilishwa kupitia fedha hizi za Mfuko huu wa Maji. Niwaombe wenzetu wa Wizara ya Fedha tujaribu kuangalia mfuko huu na kuuongezea fedha hata kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaombe pia Wizara kujaribu kuongea na mamlaka nyingine za maji huku kwenye mikoa na huku kwenye halmashauri, waende wakajifunze Tanga kwenye ile green bond, maana lazima tutafute sasa vyanzo vingi vya fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi hii ni mingi, hatuwezi kumaliza tu hivi kwa kusubiria hizi fedha bila sisi wenyewe kuanza kubuni vyanzo vingine. Kwa ile green bond, sisi Tanga tumefanikiwa. Uzuri hata gawio sasa hivi linaenda vizuri. Wameshagawiwa takribani mara nne. Kwa hiyo, tutangaze zile, watu wawekeze, tumalize miradi, halafu watu watapata gawio. Kwa hiyo, sasa na wengine waende wakajifunze pale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nimshauri kaka yangu, Mheshimiwa Waziri Aweso, tumeona pia hapa Waheshimiwa Wabunge wengi wameongea kuhusu kubambikiwa bili za maji na utatuzi mkubwa wa kuondoa kubambikiwa bili za maji, ni hizi mita za kulipia kabla ya matumizi (prepaid meters). Mita hizi ni nzuri, lakini kuna baadhi ya maeneo tutakwenda kukwama kwa sababu ya mitandao. Kwa hiyo, ninaiomba Wizara ya Maji wakae na Wizara ya Mawasiliano kuhakikisha tunapata mawasiliano ya uhakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi tu pale Tanga nilikuwa na hii mita ya prepaid, Engineer Hill mwenyewe ni shahidi, na mimi niko kilometa sita kutoka pale mjini kabisa katikati ya mji na hakuna mtandao. Kwa hiyo, nikawa nashindwa kuweka, lakini pia Mheshimiwa Engineer Ulenge naye pia hivyo hivyo alikuwa na hii mita, imebidi waje wazifungue.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, sasa tuombe Wizara ya Maji wakae na Wizara ya Mawasiliano kuhakikisha mawasiliano yanakuwa sawasawa ili tusije tukakwama kwenye hizi mita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamwomba kaka yangu Mheshimiwa Waziri, ule mradi wa Mkinga - Horohoro sasa hivi uko hatua nzuri na wakati ule Mheshimiwa Rais anapita kwenye zile siku 100 aliahidi tabasamu kwa wananchi wale. Ninawapongeza pia kuna kijiji kimoja pale cha Mtimbwani tayari wameanza kupata maji kama Mheshimiwa Rais alivyoelekeza, ninawashukuru wametekeleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ninawashukuru kwa jitihada walizochukua kwa sababu sasa hivi wamenunua mabomba yote ya mradi mzima shilingi bilioni saba. Kwa hiyo, ninawaomba Wizara twende tukakamilishe ule mradi tuweke nguvu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, ninaunga mkono hoja. (Makofi)