Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Deodatus Philip Mwanyika (3 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia kwenye hoja iliyopo mbele yetu inayohusiana na hotuba ya Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, ninamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya njema ili kuweza kusimama hapa leo na kuweza kutoa mchango wangu angalau kwa kifupi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninampongeza sana Waziri wetu Mkuu kwa kuwasilisha bajeti nzuri sana, bajeti ambayo inatoa mwelekeo wa utendaji wa Serikali. Siyo utendaji tu, lakini na makadirio ya matumizi na mapato kwa kipindi cha 2026/2027.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Watu wa Njombe, tumekuwa ni wanufaika wakubwa wa miradi mbalimbali ambayo tumeipata katika kipindi hiki cha bajeti iliyopita, lakini katika kipindi cha miaka mitano ya Serikali ya Awamu ya Sita. Tuna kila sababu ya kumshukuru sana Rais kwa mambo mengi makubwa ambayo ametufanyia wananchi wa Njombe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mambo ambayo yamefanyika katika maombi ya kawaida ya kibajeti, lakini kuna mambo yamefanyika kwa sababu tumemwomba Rais moja kwa moja alipotutembelea Njombe, na tuna mifano mingi ya mambo hayo na ndiyo maana tuna kila sababu ya kusema ahsante kwa mambo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa hatuna Chuo Kikuu Njombe, na tumekuwa na kiu ya muda mrefu sana ya kuwa na Chuo Kikuu, lakini Mheshimiwa Rais alitoa kibali cha haraka, leo tunavyoongelea Chuo Kikuu cha UDOM, campus ya Njombe inajengwa kwa speed kubwa sana, na mwaka huu intake ya kwanza inaingia pale Njombe kwa ajili ya kujifunza masuala ya ujasiriamali yanayoendana na rasilimali zilizopo Njombe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa hatuna uwanja wa ndege wa kisasa, tumemsikia Naibu Waziri, akijibu maswali hapa, akionesha namna gani Wananjombe tuliomba jambo hili na Serikali imelisikiliza na imeamua kulitekeleza, na sasa mchakato upo katika hatua nzuri ya kufanya tathmini ya eneo na kulipa fidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kero yetu kubwa kuliko zote Njombe, na nilisema, ilikuwa ni maji. Tumepata miradi mingi ya maji karibu mitano, uwekezaji wa shilingi bilioni 60 ndani ya Mji wa Njombe. Miradi ipo katika hatua mbalimbali na inaendelea vizuri, na kero ya maji muda siyo mrefu itakuwa historia kwa wananchi wa Njombe. Kwa hiyo, tuna kila sababu ya kuwa na shukrani kwa yanayofanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo yote, bado tuna changamoto ambazo tunaendelea kuzipitia, na wananchi wa Njombe wangependa kuzisikia Mbunge wao waliyemchagua akiziongelea katika ukumbi huu wa Bunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Njombe ni Mkoa wa kiuchumi na wengi wanalifahamu hilo, na waliotembelea Njombe wanafahamu hilo. Njombe ni Mkoa ambao una baraka, Njombe inao mchango mkubwa kwenye uchumi wa Tanzania, Njombe ina potential kubwa sana ya kuchangia mara dufu, mimi nasema siyo maradufu labda mara mia ya kile inachochangia leo; lakini inachangamoto za msingi ambazo zikitatuliwa, tuna uhakika Njombe tunayoiongelea itakuwa ni Njombe tofauti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo barabara yetu ya Itoni – Lusitu yenye urefu wa kilometa 51. Barabara hii tunaendelea kumshukuru Rais, kwa sababu alipokuja katika barabara 14 za kwanza alizosaini ili ziingie kwenye mchakato wa manunuzi, barabara ya Itoni – Lusitu ilikuwemo shilingi bilioni 95, ukiongeza na VAT kama shilingi bilioni 110. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kwa furaha mkandarasi amepewa site, ameijenga kwa kipindi cha mwaka mmoja, kutengeneza tuta na kazi inaendelea, lakini kwa masikitiko, kwa kipindi cha miaka miwili barabara hii imesimama, lakini usimamaji wa barabara hii umekuja na maumivu makubwa kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Njombe kwa sababu barabara hiyo inayojengwa ndiyo wanayotumia kupitisha mazao mbalimbali, mazao ya Njombe ya kilimo ni viazi, mazao ya misitu ambayo yanahitaji usafiri. Kwa hiyo, wamepitia vipindi viwili vya mvua ambavyo havikuwa vizuri kwao, ambavyo vimewarudisha nyuma na vingine vimewatia umaskini. Tunaiomba sana Serikali ilitilie maanani suala la barabara ya Itoni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii ndiyo inayokwenda kwenye migodi ya Liganga na Mchuchuma. Huwezi kuongea Liganga na Mchuchuma bila kuongelea barabara ya Itoni – Lusitu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaiomba Serikali, tunafahamu mkandarasi haidai Serikali kwa maana ya kwamba kazi iliyofanyika amelipwa, baada ya sisi kuweka nguvu kubwa, lakini tunachosema, tunaomba itakapoanza ujenzi baada ya hizi mvua kwisha, tunaomba barabara hii isisimame tena, kwa sababu ni barabara kubwa ya kipaumbele, ni barabara ya kiuchumi, na ni barabara inayofungua Liganga na Mchuchuma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niliseme hilo kwa udogo wake. Tuna barabara ya Makambaku – Songea ambayo tunahitaji iweze kukamilishwa. Barabara hii ina miaka 40, Kamati ya Miundombinu imeitembelea, ni barabara kubwa ya Uchumi. Kama ingekuwa ni katika mwili wa binadamu, ni mshipa mkubwa wa damu. Tunaomba sana Serikali ifanye utaratibu wa kutafuta fedha. Tunafahamu inaendelea na mchakato ili tupate barabara hii iweze kuanza kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la barabara za vijijini kwangu ndiyo eneo kubwa na la muhimu sana. Tuna mtandao mkubwa sana wa barabara Njombe, karibu kilometa 1,000 za Barabara, ambapo ni kilometa kama 40 tu za lami. Mazao yote ya viazi, parachichi, mazao ya mbao, mazao ya chai yote yanatoka katika maeneo ya vijiji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Njombe ni Jimbo la Mjini na Vijijini. Mazao yote yanatoka vijijini ambapo kuna uhitaji mkubwa sana wa barabara. Sasa mimi nasema kuna vicious cycle, kwa sababu Mwenyezi Mungu ametubariki na mvua nyingi na mazao mengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mazao hayo yanahitaji magari makubwa yaweze kuyachukua. Magari hayo yanahitaji kuingia vijijini. Magari ya tani 10, tumeshasahau tunaongelea semitrailer tani 32, tani 40 ndiyo yanayokwenda vijijini kuchukua mizigo. Kuwalisha Watanzania sio Wananjombe peke yao, ni Watanzania wa Mikoa karibu yote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulitoa hoja hapa na Wabunge wengi walichangia. Katika mgawanyo wa fedha ya TARURA, kwanza tunaishukuru Serikali kwa kuongeza bajeti kufikia 1.2 trillion, lakini tulidhani kwamba ingekuwa ni busara, yale Majimbo ambayo yana mijini na vijijini yangeangaliwa kwa namna ya pekee ili angalau yaongezewe fedha ili ziweze kukidhi kusaidia kutengeneza hizo barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru sana mwaka 2021/2022 nilijenga hoja kubwa sana hapa ya barabara, tukapata fedha za kutosha, shilingi bilioni 3.8 kwa ajili ya ujenzi wa barabara za mji wa Njombe, lakini uhakika ni kwamba shilingi bilioni 1.5 ilikwenda kwenye barabara za mjini na iliyobaki ilikwenda barabara za vijijini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli barabara za vijijini ambazo tulizijenga kwa zile fedha, leo hii ukienda hutaamini kama hizo barabara ni zile tulizotumia fedha nyingi. Kwa hiyo, ninakubaliana na hoja ya Waheshimiwa Wabunge hapa, ni bora twende pole pole kujenga barabara za vijijini kuliko kwenda kupoteza fedha kwa kujenga barabara ambazo zinaondolewa na mvua kila mwaka unapokuja. Ni hasara kwa nchi yetu na kwa Serikali. (Mkaofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho, Waziri Mkuu, hapa aliongelea kuhusu lumbesa, ninamshukuru sana. Ni kero kubwa sana kwa mikoa ya Nyanda za Juu Kusini na mikoa mingine kama Kilimanjaro na Kagera. Maeneo ya mahindi, vitunguu na viazi, wananchi wamekuwa wakinyonywa kwa muda mrefu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunamshukuru Waziri Mkuu, kwa kulisema. Ninaomba nitoe ombi, jambo hili ili lifanikiwe, linahitaji lisimamiwe kwa ukaribu, Halmashauri zote. Wananchi wa Njombe wakiamua kutekeleza suala la lumbesa; kutokuwa na lumbesa, kufunga mizigo kwa kilogramu 100; wananchi wa Chunya wasipofanya, wananchi wa Njombe ndio watakaopata hasara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, linatakiwa lisimamiwe kwa ukamilifu, lifuatiliwe, kuwe na monitoring na wenzetu wa TAMISEMI wahakikishe kuwe na measures kwa Maofisa wa Halmashauri ambao hawatasimamia agizo la Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana kwa kunipa nafasi, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuchangia kwenye bajeti hii ya Wizara ya Kilimo. Awali ya yote ninamshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa hotuba nzuri sana aliyoitoa hapa inayotupa matumaini makubwa kwenye kilimo. Kwa kweli Wizara hii imefanya kazi kubwa na inafanya kazi kubwa kuendeleza kilimo. Mambo yanayofanyika ni mengi na tunawapongeza sana kwa kazi nzuri wanayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, kuna maeneo machache ambayo niliona niyazungumze, ambayo mengi tumeyaongelea kwenye Kamati, lakini nime-pick machache ambayo ni muhimu kwangu na kwa Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia uzalishaji wa mazao ya asili ya biashara, Wizara inafanya vizuri sana kwa ujumla, hasa kwenye uzalishaji. Masuala ya bei yana complications zake na bei zinapanda na kushuka, lakini kiuzalishaji, mazao mengi yanafanya vizuri sana. Ukienda kwenye korosho, inafanya vizuri sana kiuzalishaji, kahawa, mkonge unafanya vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaposema vizuri, ni malengo waliyojiwekea ukilinganisha na walipofikia. Kwa kiasi kikubwa, haya mazao kama korosho yapo 80%, kahawa 90%, mkonge 90%, pamba 60%, tumbaku wako 95%, hata sukari wako 70%.

Mheshimiwa Mwenyekiti, matokeo yake ni kwamba kwa ujumla, amesema kwenye ripoti yake, mpango ulikuwa ni kuzalisha tani milioni 2.2 kwa ujumla kwa mazao hayo yote, lakini wameweza kufikia tani milioni 1.5. Kwa hiyo, progress ni nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, kuna baadhi ya mazao ambayo kwa kweli ni tatizo kubwa sana. Zao ambalo linaongoza na lenye changamoto kubwa kwenye Wizara hii ni zao la chai. Zao la chai, tunavyoongelea sasa, uzalishaji wake umeendelea kuporomoka siku hadi siku. Malengo yalikuwa ni kuzalisha angalau tani 30,000, lakini mpaka Februari walikuwa tani 9,000 na ilikuwa inaonyesha wapo tani 10,000. Hali hii siyo nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia kwa karibu sana, utagundua kinachosababisha zao la chai kuporomoka, sababu kubwa ni viwanda kutozalisha, na viwanda kufungwa. Kuna viwanda nane ambavyo vimefungwa. Kama kiwanda kinazalisha chini ya asilimia tano ni sawa na kama kimefungwa, lakini kuna vile ambavyo vimefungwa kabisa havifunguliwi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda ukaangalia viwanda vilivyofungwa, mfano Rungwe kuna viwanda kama vitatu vimefungwa. Ukija Njombe kuna viwanda vitatu vimefungwa, na Mufindi kuna viwanda viwili vimefungwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda ukaangalia zaidi vimefungwa kwa sababu gani? Cha kwanza utagundua kwamba vimefungwa kwa sababu kuna mwekezaji ambaye au hana uwezo ama hana nia ya kuendeleza zao la chai. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninaongea nikiwa nimeongozwa na data za uzalishaji wa viwanda hivyo. Ukiangalia hivi viwanda nilivyovitaja, vyote kwa pamoja, kimoja kinazalisha tani 8,000, kimoja 6,000, kimoja 2,000. Kuna uzalishaji wa viwanda vinne au vitano vya mwekezaji mmoja ambaye ni DL Group, hawa peke yao wana uwezo wa kuzalisha tani 17,800.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa masikitiko sana, uzalishaji wao sasa hivi ni tani 320, chini ya asilimia tatu. Sasa hili siyo jambo la kufumbia macho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi Watanzania tuna jambo letu. jambo letu ni Dira. Dira inatuambia kwamba 2025 kwenda 2050, tunataka private sector ichangie 70% kwenye hiyo dola trilioni moja ambayo tunatakiwa tuwe nayo au tuizalishe na pato la mtu liwe dola 7,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mwendo huu ambao tunakwenda kwenye viwanda, nchi yetu lazima iwe tayari kufanya maamuzi magumu. Nilikuwa ninatafuta neno zuri, “maamuzi magumu.” Katika maamuzi magumu ni pamoja na kufanya evaluation ya aina ya uwekezaji ambao tunao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yetu inavutia wawekezaji, lakini tunapovutia wawekezaji kuna baadhi ya wawekezaji hawatufai. Ninalisema hili kwa sababu nimeongea ndani ya Bunge hili kwa miaka mitano pamoja na wenzangu kuhusiana na zao la chai kwenye maeneo ya Mufindi, Njombe mpaka Rungwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukweli ni kwamba tuna mwekezaji ambaye alipewa viwanda kwa nia njema na Serikali kupitia benki, lakini uwezo wake umeonesha kwamba ni mdogo kuendesha hivyo viwanda. Kama tunataka kufikia lengo letu la private sector kuwa ndiyo engine ya kutusaidia kule mbele ni lazima tuwe tayari kufanya maamuzi sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2021 mwezi Machi, Mheshimiwa Majaliwa Majaliwa akiwa Waziri Mkuu alitembelea Njombe, akakaa na wadau wa chai na yaliyojitokeza yalikuwa wazi kwamba, mwekezaji huyu tunayemwongelea ambaye ni DL Group kutoka nchi ya mbele ya Mlima wa Kilimanjaro. Mwekezaji huyu ilionekana wazi na haya siyo maneno yangu ni maneno ya Mheshimiwa Waziri Mkuu wa wakati ule kwamba, anatuhujumu. Ni mhujumu uchumi hapa nchini, kwa sababu hawezi kuendesha viwanda, wafanyakazi wengi kule wamepunguzwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, …

MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa Mheshimiwa Edwin Swalle.

TAARIFA

MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Ninataka nimpe taarifa Mheshimiwa Deo Philip Mwanyika anayechangia vizuri sana kuhusu zao la chai. Amerejea hotuba ya Waziri Mkuu Mstaafu, Mheshimiwa Majaliwa Kassim Majaliwa ya tarehe 9 Machi, 2021 Njombe na mimi nilikuwepo. Waziri Mkuu alisema mwekezaji anayemiliki viwanda hivi vya Kibena, Lupembe na Luponde inaonekana kama anafanya sabotaging kwenye zao la chai hapa nchini. Hivyo ndiyo taarifa ambayo nilitaka nimwongezee Mheshimiwa Deo Mwanyika. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Deo Mwanyika, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaipokea taarifa hiyo. Ninamshukuru sana mdogo wangu Wakili Enosy Swalle. Matokeo ya jambo hili ni kwamba mapato ya Taifa, ya Serikali na halmashauri yameporomoka kwenye maeneo hayo yote, ajira zimepotea, fedha za kigeni tulizozitegemea hazipo tena, migomo ya wafanyakazi ni jambo la kawaida inaendelea, ilianza Mufindi baadaye imehamia Njombe, lakini pensheni za wafanyakazi hazilipwi na huyu mtu. Sisi tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kutambua nia nzuri ya kumwita mwekezaji, aliruhusu Wizara ifanye utaratibu wa kutafuta fedha angalau kumsaidia mwekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, alipewa shilingi 10,000,000,000 siku za karibuni, mwaka jana. Pamoja na kupewa shilingi 10,000,000,000 hali bado ni mbaya, hakuna mwanga. Hizi fedha siyo fedha za kutoka huko anakotoka, hizi ni fedha za nchi yetu, za Benki yetu hapa ya CRDB. Kwa hiyo, niseme kwamba aina ya huu uwekezaji ni lazima tukubaliane. Ndiyo mambo aliyosema Profesa Kitila lets try to do business unusual, let’s do business unusual. Tunataka wawekezaji ni kweli na sisi hatutaki kupeleka meseji mbaya kwa wawekezaji, lakini mwekezaji anayeturudisha nyuma, mwekezaji ambaye anarudisha umaskini kwa wananchi! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, chai ni zao ambalo linaongeza ajira kwa watu wa kawaida. Chai ni zao ambalo watu wanauza, wanapata hela ya kwenda kulipa ada. Chai ni zao ambalo wanalipa hela ya matibabu. Leo hii watu hawawezi kufanya hayo mambo kwa sababu mwekezaji amefunga viwanda, hata chai yake anashindwa kuhudumia. Hawezi kuweka mbolea, hawezi kubadilisha mashine, hawezi kununua spare, hata umeme anashindwa kulipa. Hivi huyu mwekezaji wa aina hiyo, kwa nini Serikali isifanye maamuzi magumu ya kutatufa njia ya kuachana naye? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wazo letu na wazo langu. Ni wakati sasa wa kutafuta wawekezaji wengine wa uhakika maana wapo. Wapo na tuombe sana benki ya CRDB itusaidie kwenye hilo, kwa sababu wao wame-finance, siamini kama wanaona mwanga kwenye jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huhitaji kuwa financial guru kujua kwamba this is a failure business, huhitaji, unaona namba zinajionesha wazi kabisa. Ukizalisha kwa uzalishaji huu na migomo inayoendelea deni la pensheni peke yake la wafanyakazi ni shilingi bilioni 4.7. Hata hivyo, analipa mishahara kwa kusuasua na hapeleki hata hizo pensheni bado kwa wafanyakazi. Kwa hiyo, hatuwezi kuendelea na hii hali, we have to make a decision.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe sana Mheshimiwa Waziri, nina matumaini makubwa kwamba analifahamu na nina uhakika sana kwamba Waziri wetu ana uwezo wa kutusukuma tukafika mahali pazuri kwenye jambo hili. Nimwombe sana Mheshimiwa Waziri, sisi tuna matumaini makubwa naye, tunakutegemea sana kwenye jambo la chai. Bahati nzuri na yeye ni mkulima wa chai, ninayoyasema haya na yeye anayapitia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nilipenda niongelee chai kwa uzito huo na niombe sana Serikali ifanye maamuzi. Wakati ninamshukuru Mheshimiwa Dkt. Samia kwa kusababisha hawa wamepata pesa, lakini hizo pesa hawazitumii kama inavyotakiwa. Hata hivyo, wanafanya vizuri kwenye mazao mengi na zao la parachichi pamoja na mbogamboga, Wizara hii imelisimamia vizuri sana na linafanya vizuri sana. Tumeona hapa linakwenda vizuri, production iko above the target wanaongelea 108%. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaombe sana bado kuna changamoto. Zao la parachichi ni very delicate, lakini linaweza lika-transform uchumi wa nchi hii. Unaposema ni green gold, it’s real means green gold. Lina uwezo mkubwa wa ku-transform uchumi wa nchi hii na kubadilisha maisha ya wananchi wa kawaida. Niwaombe sana, kuna changamoto ndogondogo pale na ninawapongeza sana watu wa COPRA wamekuwa mstari wa mbele kushirikiana na wakulima kutatua changamoto, kwa hiyo, tuwatie moyo waendelee. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwenye chai tuwaambie watu wa Bodi ya Chai wapo, kazi yao ni kusimamia zao hili. Tunapiga kelele miaka yote hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe Waziri akiweza aanze na kubadilisha hiyo bodi. Hatuwezi kuwa na bodi ambayo hatuoni mwanga kwa miaka mitano. Ni vema tukatafuta watu wenye uwezo na walio na commitment ya kubadilisha zao la chai ambalo lina watu wa kawaida wengi sana wanaolitegemea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu umwagiliaji. Tumesema hapa kwamba kwa kweli fedha zinakwenda kidogo kidogo na sisi tuombe, ukiangalia statistics za success kwa maeneo ambayo yameshapata umwagiliaji. Niwaombe Wabunge pamoja na kwamba tuna matatizo kwenye umwagiliaji, lakini tukumbuke kwamba umwagiliaji ndiyo utakaotutoa nchi hii. Kwa statistics za haraka haraka, kwa kiasi ambacho tume-invest kwenye umwagiliaji kwa maeneo yale mpaka muda huu, tumeongeza eneo la umwagiliaji mpaka kufika hekta 800,000 kutoka hekta 400,000 mwaka 2015, lakini lengo letu ni kufika hekta milioni 1.5.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tija imeanza kusikika, mpunga, mahindi na vitunguu zote kwa pamoja zimeongeza uzalishaji kwa tani kwa kila hekta. Ukiangalia mpunga tulikuwa 1.5 tons per hectare, tupo five mpaka seven. Mahindi tulikuwa 1.5 tons per hectare tupo 3.7 mpaka 5.0. Nyanya tulikuwa 5.0 tons per hectare tupo 18 tons per hectare kwa sababu ya umwagiliaji. Vitunguu vilikuwa 13 tons tuko 26 tons per hectare. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niombe sana bado tuna matumaini makubwa kwamba ni vizuri fedha zikatolewa. Tuombe kuna miradi mikubwa ambayo tunaweza kusema ni game changer. Miradi hii ni miradi ambayo itatusaidia sana na miradi hii, kwa vile ceiling yetu ya Wizara ni ndogo, tukiendelea kuiweka kwenye hiyo hatutaweza kufanikiwa, tuiweke kama miradi ya kimkakati ili tupate financing kutoka Serikalini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana kwa nafasi ya kuchangia katika hoja iliyo mbele yetu. Awali ya yote, nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa hotuba yake nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme, kwamba sisi Wananjombe Mjini tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais, tumekuwa na miradi mingi kwa mara ya kwanza. Njombe haikuwa na miradi mikubwa ya maji, lakini katika kipindi cha miaka mitano tumepata takriban shilingi 58,000,000,000 kwa miradi mikubwa mitatu ya maji kwa ajili ya Mji wa Njombe unaokua kwa haraka sana. Kwa hiyo tunaishukuru sana Wizara kwa utekelezaji mzuri, tunawashukuru sana NJUWASA ambao wamefanya kazi nzuri wakiongozwa na viongozi wa NJUWASA pale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo yote Njombe Mjini bado haijaeleweka kwa Wizara ya Maji. Njombe Mjini ni halmashauri ambayo ina mji na vijiji. Tuna vijiji 44; lakini katika vijiji hivyo 44 tuna tatizo kubwa sana la maji. Nimelisema hapa, nimelirudia na kulirudia kila mwaka. Niombe Mheshimiwa Waziri atuangalie sana Njombe Mjini, kwa maana ya Njombe Vijijini. Katika miaka mitatu iliyopita yote hatujawa na mradi wowote uliotekelezwa katika maeneo ya vijiji. Mwaka jana nilisema hapa kwamba tumeondolewa mpango mzima wa P4R kwa sababu tunaonekana tupo mjini lakini tuna vijiji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunashukuru mwaka jana tukapewa Mradi wa Kifanya, tukaingia kwenye makaratasi. Mradi huo ukafanyiwa usanifu, tenda zikatayarishwa, mikataba ikawa tayari kusainiwa, lakini ikasimamishwa; hata huo nao haukuendelea. Nimwombe sana Mheshimiwa Aweso sana, ninaomba atumie kila uwezo alionao angalau tuwe na mradi Njombe Vijijini katika kipindi hiki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninatambua kwamba tuna Mradi mwingine mkubwa wa Igongwi. Nimeongea kwa muda mrefu sana na Mheshimiwa Aweso anaufahamu huo mradi. Mradi wa Igongwi ni mradi mdogo wa bilioni 4.7; cha kusikitisha ni kwamba mradi huu una miaka 10 haujakamilika. Mradi una lot nne, lot ya kwanza imekamilika, lot ya pili imekamilika, lakini tuna lot ya tatu na ya nne, ndiyo juzi, juzi. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Waziri baada ya kumlilia akam-authorise Katibu Mkuu atupatie angalau fedha kidogo, tunashukuru kwa hilo limesukuma. Hata hivyo tunaomba huu Mradi wa Igongwi upewe kipaumbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninafahamu kuwa upo kwenye mpango; lakini kuwekwa kwenye mpango ni jambo moja na kupata fedha za utekelezaji ni jambo lingine. Niombe sana upewe kipaumbele. Haiwezekani mradi wa 4.7 billion ukakaa miaka 10. Niombe sana wananchi wa vijiji vinavyohusiana na mradi huu wapate hiyo haki yao ambayo kweli wanastahili kwa maana ni wa muda mrefu. Tuna Vijiji vya Kitulila, Madobole, Luponde, Buwemba, Njomlole, Magoda na Ikisa. Vijiji vyote hivi havina maji; na Kijiji cha Uwemba ndicho ninachotoka mimi, hakina maji. Nimwombe sana Mheshimiwa Aweso atusaidie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mradi wa Kifanya ambao umeondolewa kwa sababu za kitaalam pengine, mimi sizijui; lakini niseme mradi huu ni mradi ambao Mheshimiwa Rais marehemu Magufuli alipita eneo la Kifanya akiwa na Waziri wa Maji Mheshimiwa Mnyaa Mbarawa, wakawaahidi wananchi, wakawaambia kwamba utatekelezwa ndani ya miaka miwili, lakini hadi leo mradi huu haujatekelezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika usanifu wananchi wamehusishwa, kwa hiyo wanaufahamu vizuri, wanauongelea lakini hawajaona huo mradi. Niombe sana, mradi wa Kifanya ninajua hajauweka kwenye bajeti kwa sababu anasema ni mradi mpya; lakini in fairness mradi huu ulitakiwa uwepo, kwa sababu hatujapata mradi vijijini katika miaka mitatu; hata huu uliowekwa umetolewa. Kwa hiyo nimwombe sana atuangalie kwa jicho la pekee sana watu wa Halmashauri ya Njombe Mjini na maeneo ya vijijini ambayo yanahitaji jicho la kipekee ili yaweze kuangaliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nishukuru tuna mradi wa majitaka; mradi huu unakwenda vizuri lakini unahitaji kukamilishwa. Njombe imefikia mahali ambapo inatakiwa iwe manispaa, haiwezi kuwa kama hakuna mradi wa majitaka. Tuombe sana mradi huu wa maji taka nao ukamilishwe kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa tuna mradi mdogo sana ambao niliomba nao uangaliwe. Tuna jengo la ofisi pale mjini la NJUWASA, tuombe sana nao uangaliwe kwa sababu pale Njombe tunatumia ofisi za mkoloni hadi leo. Tuombe kwamba angalau tuangaliwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, ninaunga mkono hoja. (Makofi)