MHE. DEODATUS P. MWANYIKA aliuliza:-
Je, kwa nini, Serikali isianzishe eneo mahsusi la viwanda vya kuongeza thamani kwenye mazao ya misitu litakalohudumia masoko mbalimbali?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MIPANGO NA UWEKEZAJI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, ninaomba kujibu swali la Mheshimiwa Deodatus Philip Mwanyika, Mbunge wa Njombe Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu mkubwa wa sekta ya mazao ya misitu katika kukuza uchumi wa nchi, kuongeza thamani ya mazao, kuchangia upatikanaji wa ajira, pamoja na kuchangia katika pato la Taifa. Mkoa wa Njombe, Serikali ina mkakati wa kuanzisha eneo maalum la kiuchumi litakalovutia uwekezaji wa viwanda vya kuongeza thamani mazao ya misitu pamoja na mazao mengine ya kimkakati ikiwemo parachichi. Hatua mbalimbali tayari zimeanza kuchukuliwa, ikiwemo uchambuzi na utambuzi na upatikanaji wa maeneo ya ardhi kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, kupitia kampeni ya kitaifa ya kuhamasisha uwekezaji wa ndani, Serikali kupitia TISEZA inaendelea kushirikiana na Sekretarieti za Mikoa ya Tanzania Bara, katika kuhamaisha utengaji wa maeneo mahsusi kwa ajili ya kuanzisha kongani za viwanda, ikiwemo viwanda vya kuongeza thamani mazao ya misitu siyo tu kwa Mkoa wa Njombe na hata Mikoa mingine kama Iringa, Katavi na Tabora.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kuwasilisha. (Makofi)