Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Jonas William Mbunda (1 total)

MHE. JONAS W. MBUNDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa Serikali inaendelea na ujenzi wa Bandari ya Mbamba Bay, lakini pia kuna usafirishaji mkubwa wa makaa ya mawe kutoka Nyasa na Mbinga kwenda Mtwara; lakini pia tunategemea Mradi mkubwa wa Liganga na Mchuchuma. Katika majibu ya msingi ya Naibu Waziri amesema kwamba upembuzi yakinifu wa kutekeleza Mradi wa Ujenzi wa SGR kutoka Mtwara kwenda Mbamba Bay umeanza kutekelezwa. Je, itachukua muda gani kukamilisha upembuzi yakinifu na mradi huo ukaanza kutekelezwa?
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ninafahamu swali hili linagusa takriban Wabunge wote wa Kusini; na pengine wangesimama kutaka kuuliza reli ya kusini itaanza kutekelezwa lini?

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba nitoe maelezo kwa ufupi sana. Serikali inatambua umuhimu wa reli ya kusini, kwanza kama kiunganishi cha Bandari ya Mbamba Bay na Bandari ya Mtwara, kwa sababu hizi mbili zikiungana unarahisisha usafirishaji; na nini kimekifanyika?

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hatua za awali Serikali imekwishaanza kujenga Bandari ya Kisiwa Mgao pale Mtwara bandari ya pili ambayo itakuwa maalum kwa ajili ya kusafirisha dirty cargo; yaani cement, makaa ya mawe na kadhalika; zaidi ya bilioni 435 zimeelekezwa pale. Pia ujenzi wa bandari ya Mbamba Bay ambao utagharimu zaidi ya bilioni 70, ni hatua muhimu kuelekea kwenye jambo hilo. Tatu, fidia imelipwa kule Ludewa kwa wananchi waliopo kwenye maeneo ya Liganga na Mchuchuma, hiyo ni hatua pia. Nne sasa, tumekwishafanya usanifu. Kama nilivyosema, tunatafuta wawekezaji binafsi ambao tutashirikiana nao ili tuanze kujenga. Ninatoa rai tena kwa watu wote wa ndani na nje ya nchi ambao wapo tayari kushirikiana na Serikali, twendeni tukajenge reli hii ambayo ni muhimu sana kwa uchumi wa Taifa letu.