MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, ninawashukuru. Barabara ya kutoka Omugakorongo – Kituntu – Rwambaizi – Igurwa – Murongo ipo katika Ilani ya Chama Cha Mapinduzi, imekuwa kwenye manunuzi kwa muda mrefu, ni barabara muhimu kwani inaunganisha nchi yetu na nchi za Afrika Mashariki; na kujengwa kwa kiwango cha lami kutainua uchumi wa Kagera pamoja na Taifa letu. Je, ni lini barabara hii itajengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, ninaomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba barabara hii ni kati ya zile barabara zetu kuu, inaunganisha Uganda na Tanzania kupitia Daraja la Murongo. Mheshimiwa Mbunge atakubaliana nami kwamba hii barabara ilikuwa imetangazwa na tulipata mkandarasi, lakini tukashindwana naye kimkataba. Hivyo, hii barabara imetangazwa tena, iko kwenye hatua za manunuzi kuanza kuijenga kwa kiwango cha lami. Tunaanzia Murongo kuja Omugakorongo. Ahsante. (Makofi)